Wednesday, January 11, 2017

Wapuuzeni wanaoendesha siasa zilizopitwa na wakati - Rais Dkt Magufuli

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 11 Januari, 2017 ameanza ziara ya siku mbili mkoani Simiyu kwa kuwataka wananchi wa mkoa huo na Tanzania kwa ujumla kuwapuuza  watu wanaoendesha siasa alizozitaja kupitwa na wakati kwa kutumia baadhi ya vyombo vya habari kutangaza kuwa Tanzania inakabiliwa na njaa badala ya kuwahamasisha wananchi kufanya kazi.
Dakta Magufuli amesema hayo wakati akizungumza na wananchi katika uwanja wa Shule ya Msingi Somanda mara baada ya kuweka jiwe la Msingi katika  Hospitali ya Mkoa wa Simiyu na kufungua barabara ya Lamadi hadi Bariadi yenye urefu wa kilomita 71.8 iliyogharimu zaidi ya shilingi Bilioni 90.
Amesema kumekuwepo na baadhi ya wanasiasa na wafanyabiashara ambao wamekuwa wakiwahamisisha wananchi na kutumia baadhi ya vyombo vya habari kutangaza baa la njaa wakati wanasiasa hao hao ndio waliopitisha Bungeni kutaka nchi iuze chakula nje ya nchi na sasa hao hao wanatangaza baa la njaa.
'' Baadhi ya wanasisa walizungumza Bungeni kutaka wananchi waruhusiwe kuuza chakula nje ya nchibkwa kuwa kuna chakula cha kutosha... leo hii hao hao wanatumia baadhi ya vyombo vya habari kutanga baa la njaa''  
Akizungumzia gharama za  ujenzi wa Hospitali ya mkoa wa Simiyu, Rais Magufuli ameutaka uongozi wa mkoa wa Simiyu, Wizara ya Ujenzi na Wakala wa majengo nchini TBA kukaa na kurejea gharama za ujenzi wa Hospitali hiyo wa Shilingi Bilioni 46 kuwa hauendani na hali halisi ya aina ya jengo linalotakiwa kujengwa.Rais Magufuli ametoa Shilingi bilioni 10 ili kukamilisha ujenzi wa hospitali hiyo. 
''Haiwezekani  majengo ya ghorofa ishirini lijengwe kwa shilingi Bilioni Kumi wakati jengo la ghorofa moja moja lijengwe kwa gharama ya shilingi Bilioni 46''
Rais Magufuli pia ameutaka uongozi wa mkoa wa Simiyu kuendelea na ujenzi wa mradi wa tenki la maji katika mlima Ngasamo ili wananchi wa mkoa wa Simiyu ikiwemo wilaya ya Bariadi kupata huduma ya maji badala ya kukwama kutokana na mwekezaji mmoja kutaka kuchimba madini ya Nikeli katika mlima huo.
Amesema haiwezekani wananchi zaidi ya milioni moja wakose maji kutokana na mwekezaji mmoja ni kukosa muelekeo na kumkosea Mwenyezi Mungu kitu kisichokubalika hivyo Waziri wa Nishati na Madini afute leseni ya mwekezaji huyo ili wananchi wa Simiyu wapate huduma ya maji.
Rais Magufuli amewataka wananchi wa Mkoa wa Simiyu na Watanzania kwa ujumla kutumia mvua chache zinazonyesha kulima mazao yanayostahamili ukame kama vile Mtama,viazi na Uwele ili kuweza kujikimu kwa chakula badala ya kutegemea chakula cha msaada kutoka Serikali. 
Jaffar Haniu
Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Simiyu
11 Januari, 2017

No comments: