Saturday, January 21, 2017

TUMETOA SH. BILIONI 1.4 UJENZI WA HOSPITALI YA MKOA WA NJOMBE, BARABARA YA NJOMBE-MAKETE KUJENGWA KWA KIWANGO CHA LAMI -WAZIRI MKUU

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga sh. bilioni 19 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Njombe-Makete yenye urefu wa kilomita 109.4 kwa kiwango cha lami.

Ametoa kauli hiyo jana  (Ijumaa, Januari 20, 2017) wakati akizungumza na viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Makete alipowasili katika kata ya Mtamba wilayani hapa akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Njombe.

Waziri Mkuu amesema usanifu wa kina wa barabara ya Njombe-Makete kwa ujenzi wa kiwango cha lami umekamilika hivyo amewataka wananchi waendelee kuwa na subira.

Amesema barabara nyingine inayotarajiwa kujengwa ni ya kutoka Makete hadi Mbeya kupitia Isyonji yenye urefu wa kilomita 96 ambayo imetengewa sh. milioni 50 kwa ajili ya kufanyiwa usanifu.

Waziri Mkuu amesema wananchi waendelee kushirikiana na Serikali kwani imedhamiria kuwatumikia kwa kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maeneo yao.

Aidha, Waziri Mkuu amewataka wahandisi wa wilaya hiyo kuhakikisha wanawasimamia vizuri wakandarasi wanaojenga miradi mbalimbali katika halmashauri zao kuhakikisha kama viwango vinalingana na thamani halisi ya fedha zinazotolewa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliwataka wakuu wa Idara katika halmashauri kupambana na vitendo vya rushwa na wahakikishe watumishi hawatowi huduma kwa kuomba rushwa.

“Kwanza watumishi watambue kwamba rushwa ni dhambi. Pia kiutumishi ni makosa makubwa hivyo wajiepushe na vitemdo hivyo,” amesema.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Makete Bi. Veronica Kessy amesema kujengwa kwa barabara hizo kwa kiwango cha lami kutaimarisha ukuaji wa uchumi wa wilaya hiyo na Mkoa wa Njombe kiujumla hivyo wananchi kupata tija.

“Mfano barabara ya kutoka Makete hadi Mbeya kupitia Bulongwa, Iniho, Kikondo na Isyonje itasaidia wilaya kufunguka hivyo kurahisisha usafirishaji wa mazao ya misitu kama mbao,” amesema.

Hata hivyo Mkuu huyo wa Wilaya amesema barabara hii pia itaunganisha Wilaya hiyo na kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Songwe hivyo watapata fursa ya kuanzisha kilimo cha maua. Awali walishindwa kulima maua kwa sababu hakukuwa na usafiri wa uhakika.

Awali Waziri Mkuu alitembelea shamba la mifugo la Kitulo linalomilikiwa na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi lenye jumla ya Ng’ombe 750 wakiwemo ndama 61, majike 212, mitamba 273, madume 21, na madume wadogo 183.

Shamba hilo linazalisha wastani wa lita 450,000 za maziwa kwa mwaka kutokana na ng’ombe 123 wanaokamuliwa. 


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali imetoa sh. bilioni 1.4 kati ya sh. bilioni 1.8 zilizotengwa katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya uendelezwaji wa mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe.

Amesema ujenzi wa hospitali hiyo ni utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015/2020 ya kuwa na zahanati katika kila kijiji, kituo cha afya katika kila kata, hospitali katika wilaya na hospitali za rufaa kwa kila mkoa.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumamosi, Januari 21, 2017) wakati alipotembelea eneo la mtaa wa Wikichi inapojengwa hospitali hiyo akiwa katika siku ya tatu ya ziara yake ya kikazi mkoani Njombe.

Amesema lengo la ujenzi wa hospitali hiyo ni kuhakikisha mwananchi anaanza kupata huduma za afya katika eneo lake na anapokuwa na tatizo kubwa ndipo atakwenda hospitali ya wilaya na kisha hospitali ya rufaa ya mkoa.

“Hospitali hii ikikamilika itawapunguzia wananchi gharama za kusafiri umbali mrefu kwa ajili ya kufuata huduma za rufaa. Sasa hakutakuwa na sababu ya kwenda Iringa, Mbeya wala Ruvuma huduma zote zitakuwa zinapatikana hapa hapa Njombe,” amesema.

Amesema ujenzi huo utakapokamilika Serikali itapeleka fedha za ununuzi wa dawa na vifaa tiba. “Hatuwezi kukosa fedha za kununulia vifaa tiba na dawa kwani ni moja ya majukumu yetu,”.

“Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli ameahidi kuwahudumia na kuwatumikia wananchi wote bila ya kujali uwezo wao, itikadi zao za kidini na kisiasa na hapa ndiyo maana ya ahadi hiyo ya Serikali ya kuwahudumia. Watu wote watakuja kutibiwa hapa,” amesema.

Akitoa taarifa ya ujenzi mradi wa hospitali hiyo, Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe, Bw Jackson Saitabau amesema kukamilika kwa ujenzi wa hospitali hiyo kutawapunguzia wananchi gharama kubwa za kufuata huduma za rufaa katika mikoa ya jirani.

Amesema ujenzi wa hospitali hiyo ulianza katika eneo hilo lenye ukubwa wa takribani ekari 70 katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, ambapo kiasi cha sh. 953.705 zilitengwa kati yake sh. milioni 236.575 zilitumika kwa ajili ya ulipaji wa fidia.

“Hospitali hii inajengwa kwa awamu na tulianza na jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambapo gharama za mradi ni sh. bilioni 3.2 huku gharama za mtaalamu mshauri ni sh. milioni 114.160. Mradi ulianza Julai 23, 2016 na unatarajiwa kukamilika Januari 26, 2018,” amesema.

Amesema kuwa hadi sasa kazi ya ujenzi huo imekamilika kwa asilimia 40 na mkandarasi ameshalipwa sh. milioni 892.963 sawa na asilimia 28 ya gharama za mradi na mtaalam mshauri amelipwa sh. milioni 51.50.

Naye Mbunge wa Jimbo la Njombe, Mheshimiwa Edward Mwalongo ameishukuru Serikali kwa kuwawezesha kupata hospitali ya Rufaa ya mkoa huo na amewaomba wananchi waendelee kuiunga mkono Serikali na washiriki kikamilifu katika kuilinda miundombinu hiyo.

Pia Waziri Mkuu amezindua Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Wanging’ombe iliyojengwa katika Kata ya Igwachanya pamoja na kupokea taarifa ya ujenzi wa Ofisi hiyo pamoja na kuweka jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe.

Aidha, Waziri Mkuu amewataka watumishi wa halmashauri hiyo ambao wananshi nje ya eneo wilaya hiyo wawe wamehamia ifikapo Februari 15 mwaka huu.

No comments: