Saturday, December 31, 2016

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, MHANDISI RAMO MAKANI AUNDA KAMATI YA KUSULUHISHA MGOGORO WA MUDA MREFU WA PORI TENGEFU LA LOLIONDO, ATOA UFAFANUZI WA TAARIFA ZA FARU JOHN


NA HAMZA TEMBA -WMU.

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani amesema hakuna mamlaka nyingine ya Serikali chini ya ofisi ya waziri mkuu yenye mamlaka ya kutoa tamko au ufafanuzi kuhusiana na Faru John kwa sasa kwakua jambo hilo bado lipo kwenye uchunguzi.

Amesema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari katika tarafa ya Loliondo, Wilaya ya Ngorongoro Mkoani Arusha akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya siku mbili wialayani humo kwa ajili ya kufuatilia changamoto za uhifadhi pamoja na utekelezaji wa maagizo wa Waziri Mkuu aliyoyatoa hivi karibuni akiwa ziarani mkoani Arusha.

Amesema miongoni mwa maagizo aliyoyatoa Waziri Mkuu katika ziara hiyo ni kuwasilishwa kwa taarifa ya inayoelezea utaratibu uliotumika kumuhamisha Faru John kutoka Hifadhi ya Ngorongoro kwenda Sasakwa Black Rhino Sanctuary iliyoko kwenye Hifadhi ya Grumeti pamoja na kuwasilishwa kwa pembe zake ambapo baadae aliunda tume ya kuthibitisha ukweli wa taarifa hiyo.
.
"Ripoti hii ya uchunguzi ni mali ya Waziri Mkuu atakayeweza kutoa ripoti hii nje kwa ajili ya matumizi  ya kila mmoja wetu ni Waziri Mkuu, kwa maana ya mamlaka, kwa hiyo hakuna mamlaka nyingine yeyote ya Serikali chini ya Waziri Mkuu yenye uhalali wa kutoa tamko au ufafanuzi wa jambo hili, mpaka pale Waziri Mkuu atakapokamilisha kusoma ripoti kwa kina kwa kutumia wataalam wake, kufanya vipimo kama ambavyo tunasikia amevipeleka kwa mkemia mkuu wa Serikali, pamoja na udadavuzi wa ripoti.

"Kwa kipindi hiki nnapozungumza, zaidi ya kwamba tunasubiri maagizo au maelekezo au muelekeo sasa juu ya jambo hili kutoka ofisi ya Waziri Mkuu, hakuna jambo jingine ambalo Wizara inaweza kufanya wala kusema kuhusiana na suala la Faru John, hatuna mamlaka hiyo", amesema.

Akizungumzia tukio la hivi karibuni la baadhi ya watumishi wa wizara kuonekana kwenye chombo kimoja cha habari wakitoa ufafanuzi juu ya jambo hilo amesema "Mimi kwa sasa nnachoweza kusema kwa chochote kilichofanyika kama kuna utaratibu umetumika kuwafanya waweze kwenda mbele ya vyombo vya habari, kwenda kutoa taarifa hizo, lakini pia tukijua kabisa kwamba wao sio wasemaji wa wizara na wala kwa level  (hatua) ya jambo lenyewe pale lilipofikia wao hawana mamlaka ya kuweza kutosha kulizungumzia jambo hilo, sasa kwanini limekua hivo jana ni jambo ambalo tunalifanyia kazi, bila shaka walipoitwa pengine hawakuambiwa sawasawa wanaenda kuzungumzia nini",.

"Kama wizara tutachukua sasa muda wa kuweza kuzungumza nao tujue nini kilitokea lakini kimsingi baada ya hiki nnachokisema hapa sasahivi ieleweke hivo na taifa zima kwa ujumla kuwa hakuna tunachoweza kusema sasa hakuna tunachoweza kufanya sasa mpaka uchunguzi unaofanyika chini ya ofisi ya waziri mkuu ukamilike mpaka waziri mkuu asome aridhike na taarifa yetu na aweze kuina taarifa ile inafaa kwa namna gani na kama kuna maagizo mengine atayatoa baada ya hatua hiyo.

Wakati huo huo ametoa wito kwa wananchi kuwa na subira juu ya taarifa sahihi za faru John "Unaweza kusikiliza habari kutoka vyanzo vingi tu, lakini ukishapata habari usiifanyie kazi haraka haraka bila ya kujiridhisha juu ya ubora wa taarifa unayoipata, wawe na subira, wananchi waendelee kusubiri, si waliapata taarifa ya faru John kupitia kwa Waziri Mkuu?, busara ya kawaida inasema kwamba wangesubiri kutoka kwa Waziri Mkuu au mtu atakayekasimiwa madaraka na Waziri Mkuu atasema kitu kingine kinachofuatia baada ya pale na si vinginevyo".

Katika hatua nyingine Naibu Waziri Makani ameunda kamati maalum ya kuushulikia mgogoro wa muda mrefu katika  pori tengefu la Loliondo baina ya wananchi, wawekezaji na hifadhi hiyo. Hatua hiyo imekuja ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya waziri mkuu ya kuwakutanisha wadau katika eneo hilo kumaliza mgogoro huo.

Kamati hiyo imehusisha taasisi za serikali, asasi za kiraia, viongozi wa dini, wazee wa kimila (Leigwanan), viongozi wa vijiji, wajumbe wa kamati teule za vijiji, wawakilishi wa wanawake na vijana. Ameunda pia kamati ya kuandaa kanuni za kundesha vikao  vya kamati hiyo.

"Kuna watu humu ndani na hata nje ambao hawataki tumalize migogoro Loliondo, nitoe rai kwao, waache chokochoko. Wananchi muone umuhimu wa jitihada za Serikali kumaliza changamoto hii na kutuunga mkono", alisema Makani.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani (kulia) akizungumza katika kikao cha wadau wanaohusika na mgogoro wa pori tengefu la Loliondo alichokiitisha katika ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro, katika tarafa ya Loliondo wilaya ya Ngorongoro mkoani Arusha jana. Kupitia kikao hicho aliunda kamati maalum ya kutatua mgogoro wa muda mrefu wa pori tengefu la Loliondo. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Mfaume Taka.
 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhandisi Ramo Makani (kulia) akizungumza katika kikao hicho.

Baadhi ya wadau wanaohusika na mgogoro wa pori tengefu la Loliondo wakiwa kwenye mkutano huo.

No comments: