Tuesday, November 29, 2016

Watanzania Washauriwa Kutumia Nishati Mbadala.

Na Lilian Lundo

Serikali itaendelea kuzuia matumizi ya mkaa na kuni ili kuendelea kutunza mazingira na kuhifadhi uoto wa asili wa nchi yetu. 

Hayo yamesemwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe alipokuwa akisoma hotuba kwa niaba ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa leo Jijini Dar es Salaam katika warsha ya wadau kujadili namna na njia bora ya kupunguza matumizi ya mkaa kwa usimamizi endelevu wa mazingira nchini. 

Prof. Maghembe amesema kuwa Serikali itaendelea kurekebisha sheria ya gharama ya uzalishaji wa mkaa, ili nishati hiyo iwe na gharama ya juu na kuwafanya watanzania wahamie kwenye nishati nyingine kama vile gesi ambayo gharama yake ni rahisi. 

“Uchomaji wa mkaa unaharibu mazingira kwa kiwango kikubwa, ambapo miti inapokatwa joto huongezeka, kipindi hiki mvua za vuli zilitakiwa kuwa zinanyesha lakini mvua hizo hazinyeshi kutokana na ukataji miti uliokithili,” alifafanua Prof. Maghembe. 

Aliendelea kwa kusema kuwa ukataji wa miti umesababisha wanyamapori kuhama maeneo yao ya asili kwa ajili ya kutafuta maji na chakula.
Kwa upande wake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba amesema kuwa nishati ya mkaa inaonekana kama nishati ambayo gharama yakeiko chini ukilinganisha na nishaati nyingine. Lakini mtu wa kipato ch chini anaweza kutumia mpaka shilingi 4,000 kwa siku kwa kununua mkaa gharama ambayo ni kubwa ukilinganisha na gharama za gesi. 

Nae Mkurugenzi wa kampuni ya ORXY -Tanzania Nick McAleer amesema kwamba watumiaji wa gesi wanaongezeka kila siku na mpaka sasa kampuni hiyo ina mawakala wapatao 1,000 wanaouza nishati hiyo. 

Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa nishati ya gesi gharama yake ni nafuu ukilinganisha na mkaa, vilevile utumiaji wa gesi unahifadhi mazingira na kuwaepushia watanzania magonjwa ya mapafu na kansa ambayo yanasababishwa na moshi wa mkaa na kuni. 

Aidha ameiomba Serikali kuondoa baadhi ya kodi hasa kwa mawakala ambao wanataka kuuza gesi kwani kwa kufanya hivyo kutaongeza idadi ya wauzaji na upatikanaji wa gesi kuwa ni wa rahisi nchi nzima.

No comments: