Tuesday, November 8, 2016

MATUMIZI YA TOVUTI YAZIDI KUPANUA WIGO WA UTOAJI WA HUDUMA ZA SERIKALI KWA WANANCHI

Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO Bw. Hassan Abbas akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu taasisi za Serikali kutekeleza agizo la kuhuisha taarifa na huduma katika Tovuti zao mapema kabla ya mwisho wa mwezi huu katika mkutano uliofanyika Ofisi za Wakala ya Serikali Mtandao (EGA) hivi karibuni Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao Bibi. Susan Mshakangoto.
Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao Bibi. Susan Mshakangoto akifafanua jambo kwa waandishi wa habari wakati wa mkutano na waandishi hao hivi karibuni jijini Dar es Salaam, kuhusu taasisi za umma kuhuisha taarifa katika Tovuti zao. Kushoto ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO Bw. Hassan Abbas.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari, MAELEZO Bw. Hassan Abbas akiwaonyesha waandishi wa habari mwongozo wa utengenezaji wa Tovuti za Serikali wakati wa mkutano wake na waandishi hao hivi karibuni Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao Bibi. Susan Mshakangoto.

Na Ismail Ngayonga, Dar es Salaam.

SERA ya Taifa ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ya mwaka 2003, pamoja na mambo mengine inasisitiza umuhimu wa  Serikali kutumia fursa za TEHAMA katika utendaji kazi wa kila siku na utoaji huduma kwa wananchi.

Katika kutekeleza sera hiyo, mwaka 2004 Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma (OR-MUU) ilianza kuchukua hatua mbalimbali kuongeza matumizi ya TEHAMA katika kuimarisha mifumo ya utoaji habari na huduma kwa wananchi. 

Moja ya maeneo ya TEHAMA ambayo Serikali imewekeza na kupata mafanikio makubwa ni pamoja na eneo la tovuti ambapo hadi kufikia mwaka 2010 takribani Taasisi zote za Serikali zilikuwa na tovuti.

Katika kipindi cha mwaka mmoja wa Serikali ya Awamu ya Tano, kumekuwepo na mapinduzi makubwa   katika mfumo wa upashanaji wa habari na utoaji wa huduma kwa umma kupitia tovuti. 
Mtendaji Mkuu wa Serikali Mtandao, Dkt. Jabiri Bakari anasema taasisi za umma zinapaswa kuwa na tovuti zitakazosaidia wananchi kupata kwa urahisi taarifa zinazohusu shughuli na huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi hizo.

“Tovuti za Serikali zinatakiwa kuwa kwa lugha ya Kiswahili na Kiingereza na  mwananchi anapofungua tovuti hizo lugha itakayoonekana kwanza iwe ni  Kiswahili na muda wowote mwananchi huyo anaweza kubadili kwenda kwenye lugha ya Kiingereza”.

Dkt. Bakari amesema kuwa Wakala imetoa miongozo ya  kusimamia na kuendesha tovuti hizo na unapatikana kwenye tovuti ya Wakala www.ega.go.tz sehemu ya Miongozo na Viwango.

Akizungumzia mafanikio ya Wakala hiyo, Dkt. Jabiri anasema Wakala imetengeneza mifumo mbalimbali na kuweka miundombinu ya kuwezesha taasisi za umma kutumia Tehama katika utoaji wa  huduma kwa wananchi. 

“Tovuti Kuu ya Serikali ni zao la kwanza la Wakala na ilibuniwa na kusanifiwa na wataalam wa ndani. Katika tovuti hiyo ambayo pia ni mfumo, ina taarifa za baadhi ya taasisi za umma, sekta mbalimbali na huduma zake pamoja na balozi zilizoko nchini na zile za kwetu zilizoko nje ya nchi”, anasema Dkt. Bakari. 

Anaongeza kuwa mfumo mwingine uliotengenezwa na Wakala hiyo ni Tovuti Kuu ya Ajira ambayo humwezesha mwananchi kuona ajira mbalimbali zinazotangazwa na Serikali ambapo muombaji wa ajira anaweza kutuma  wasifu wake  kwa njia ya mtandao na nafasi zinapotangazwa zenye kuhitaji mtu mwenye sifa hizo.

Kwa mujibu wa Dkt Jabiri anasema jitihada   mbalimbali zinatekelezwa na  Wakala ili kuwezesha taasisi za umma kutoa huduma zao kwa njia ya mtandao kwa kuongeza uwezo wa wataalam wa Tehama  kwa kuwapa maarifa na ustadi wa kubuni.

Dkt. Jabiri anasema Wakala imetoa mafunzo kuhusu usimamizi na Ujenzi wa Mtandao wa Mawasiliano Serikalini kwa taasisi za umma 149 wakiwemo Maofisa TEHAMA 226, Mafunzo ya uendeshaji wa Vituo vya data kwa Taasisi za umma 91 wakiwemo Maofisa TEHAMA 162.

Aidha Mafunzo ya Usimamizi wa Mfumo wa Barua Pepe Serikalini yametolewa kwa taasisi 157 pamoja na Mafunzo ya usimamizi wa taarifa tovuti za serikali yametolewa kwa taasisi 71.

“Mafunzo ya uwekaji taarifa katika tovuti kuu yametolewa kwa taasisi 86 na Mafunzo hayo yanaendelea kutolewa kwa kila taasisi ambayo inatengenezewa Tovuti na Wakala” anasema Dkt. Jabiri.

Kwa upande wake Meneja Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala wa Serikali Mtandao, Suzan Mshakangoto anasema mbali na kuanzisha mtandao huo Serikali imeziagiza taasisi zote za umma kuhuisha taarifa katika tovuti zake na Tovuti Kuu ya Serikali (www.tanzania.go.tz). 

Anaongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa tovuti hizo kumesaidia kuongeza kasi ya utendaji, uwazi, ufanisi, uwajibikaji na tija katika utoaji wa taarifa na huduma kwa wananchi, pamoja na changamoto kadhaa zilizojitokeza katika usimamizi wa tovuti hizo. 

Akifafanua zaidi anasema miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na tovuti za taasisi za umma kutokuwa na taarifa mpya na za mara kwa mara, na kutofuatwa kwa mwongozo  uliowekwa unaosisitiza usanifu wa tovuti hizo.

Naye Mkurugenzi wa Habari, Hassan Abbas anasema ofisi yake kwa kushirikiana na e-GA tayari imezisaidia Halmashauri 93 kuhuisha taarifa zilizopo katika tovuti zao ili kuwawezesha wananchi kufahamu huduma mbalimbali zinazotolewa na Serikali katika maeneo yao.

Abbas anasema tovuti ni mojawapo ya nyenzo na njia rahisi na ya haraka ya kutoa taarifa na kufikisha huduma kwa umma kwani  miaka ya nyuma taarifa na huduma za Serikali zilitolewa kwa njia ya kutembelea ofisi husika au kwa kupitia vyombo vya habari. 

Anasema Serikali imetoa mafunzo kwa Maafisa Habari katika Wizara, Idara, Wakala na Taasisi mbalimbali jinsi ya kuboresha taarifa katika tovuti zao,  na kuanzia sasa ofisi yake itaanza kufanya tathimini ili kufahamu Wizara ambazo hazijaanza kuhuisha taarifa zake.

Kwa mujibu wa Abbas anasema Serikali imekusudia kupanua wigo wa mawasiliano katika Wizara, Idara, na Taasisi zake kwa kuwahimiza Maafisa Habari kutumia zaidi mitandao ya kijamii kwa ajili ya kujibu na kutoa ufafanuzi wa hoja mbalimbali zinazoelekezwa kwa Serikali.

Katika kuboresha mfumo wa mawasiliano Serikalini, ofisi yake imeanzisha akaunti ya twitter ya; msemaji wa Serikali@TZ_Msemaji Mkuu ambayo mwananchi anaweza kuifuata akaunti hiyo kwa kutafuta Msemaji Mkuu wa Serikali on Twitter.

Anasema wananchi wengi kwa sasa wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuendesha mijadala mbalimbali ambayo baadhi yao imekuwa ikipotosha ukweli kuhusu utelekezaji wa sera mbalimbali za Serikali.

Abbas anasema jukumu la kuboresha mawasiliano kati ya Serikali na Wananchi ni suala mtambuka, na hivyo ni wajibu wa Maafisa Habari wa Wizara, Idara, Taasisi, Wakala za Serikali kutoogopa kutoa taarifa muhimu kwa waandishi wa habari.

“Waandishi wa habari wasitoe taarifa zisizofanyiwa utafiti wa kutosha kwa wananchi, ni vyema sote tushirikiane katika kutoa taarifa sahihi kwa wananchi kuhusu sera na mikakati ya serikali ili kuleta maisha bora kwa watanzania wote” anasema Abbas.

Kwa kutambua umuhimu wa tovuti kama nyenzo kuu ya mawasiliano, Serikali kupitia Mradi wa Uimarishaji wa Mifumo ya Umma (PS3) unaofadhiliwa na shirika la misaada la Marekani iliunda kikosi kazi kwa ajili ya uhuishaji wa tovuti za Mamlaka ya Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Kikosi kazi hicho kinahusisha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), na Wakala wa Serikali Mtandao (E-GA).

Msimamizi wa Mifumo ya Taarifa wa PS3, Bunto Mbozi anasema tovuti nyingi za TAMISEMI zimetengenezwa, zinasimamiwa na kuendeshwa bila kuwepo na utaratibu unaofanana,  hali hiyo inasababisha uwepo wa tovuti zisizokidhi viwango  na  ubora kufuatana na mahitaji ya watumiaji.


Anaongeza kupitia mradi, PSE3 imekusudia kuhuisha taarifa zote za tovuti za Serikali, ambapo kwa sasa wataanza na Halmashauri 93 nchini na baadae katika Wizara, Idara, Taasisi nyingine za Umma.

Bunto anasema mradi huo ulizinduliwa mapema mwaka huu mkoani Iringa ambapo hadi kufikia mwezi Agosti mwaka huu, jumla ya mikoa 13 ilifikiwa na taasisi hiyo na kuendesha mahojiano na Watendaji Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Idara na vitengo mbalimbali.

Anaitaja mikoa hiyo kuwa ni Iringa, Shinyanga, Dodoma, Mbeya, Mwanza, Kagera, Mara, Rukwa, Kigoma, Lindi, Mtwara na Morogoro.

Akifafanua zaidi anasema katika utafiti uliofanyika ulibaini kuwa mikoa mingi ilianza kutengezeza tovuti zao lakini hazikikuwa na taarifa muhimu  zinazohitajika na wananchi wa kawaida.

“Tovuti ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inatembelewa na watu zaidi ya 500,000 kwa siku, hii inatokana na mahitaji ya huduma inazotoa TRA kwa wananchi, hivyo mradi huu pia umekusudia kuzifanya tovuti za Mikoa na Halmashauri kutembelewa na wananchi wengi zaidi” anasema Bunto. 

Kwa mujibu wa Bunto anasema, mradi huo uliichagua TAMISEMI kutokana na Ofisi hiyo kutoa  huduma muhimu zinazomgusa wananchi wa kawaida ikiwemo afya, maji, elimu, mazingira, uvuvi, ufugaji na kadhalika, ambapo wananchi wengi wanapenda kufuatilia taarifa na huduma hizo katika ofisi za umma.

Anaongeza uhuishaji wa taarifa za tovuti utasaidia kutangaza fursa na rasilimali za kiuchumi zilizopo katika mikoa, hatua itayoziwezesha halmashauri nyingi kuibua vivutio vya uwekezaji sambamba na kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.

No comments: