Wednesday, November 16, 2016

Dkt Kalemani azindua mradi wa Umeme (kW 430) mkoani Njombe.

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani akifunua kitambaa kuashiria uzinduzi rasmi wa Mradi wa Umeme wa Maji wa Kilowati 430 katika Kata ya Ikondo mkoani Njombe.  Wengine katika picha ni Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchimbi (wa kwanza kushoto), Mbunge wa Lupembe,  Joram Hongoli (wa pili kushoto),  Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya (EU), Jane Nunes (wa Tatu kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Dkt Gideon Kaunda (wa pili kulia) na Balozi wa Italia nchini, Roberto Mengoni (wa Nne kulia).
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (wa pili kutoka kulia) akipiga makofi mara baada ya uzinduzi rasmi wa Mradi wa Umeme wa Maji wa Kilowati 430 katika Kata ya Ikondo mkoani Njombe.  Wengine katika picha ni Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchimbi (wa kwanza kushoto), Mbunge wa Lupembe,  Joram Hongoli (wa Tatu kushoto),  Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya (EU), Jane Nunes (wa Nne kushoto) na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Dkt Gideon Kaunda (wa pili kushoto). 
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (wa pili kushoto) akiangalia moja ya mitambo ya kuzalisha umeme  Umeme wa Maji wa Kilowati 430 katika Kata ya Ikondo mkoani Njombe.  Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema na wa kwanza kulia ni Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini, Mhandisi Gissima Nyamo-Hanga.


Na Teresia Mhagama
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani amezindua mradi wa umeme wa Kilowati 430 unaotokana na maporomoko ya maji katika Kata ya Ikondo mkoani Njombe ambapo mpaka sasa zaidi ya wateja 1140 wameunganishiwa umeme huku zoezi hilo likiwa ni endelevu.

Uzinduzi huo uliofanyika katika Kata  hiyo ulihudhuriwa na Balozi wa Italia nchini Tanzania, Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya (EU), Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa wilaya ya Njombe, wananchi wa Kata ya Ikondo, Shirika lililotekeleza mradi huo la CEFA, watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO).
Dkt. Kalemani alisema kuwa mradi huo umetekelezwa na Taasisi isiyo ya kiserikali ya CEFA  kutoka Italia     na kugharamiwa kwa pamoja kati ya Jumuiya ya Ulaya na Serikali ya Tanzania kwa jumla ya Dola za Marekani 110,209.
Aliongeza kuwa mradi huo wa umeme utasambazwa katika vijiji vilivyoko kata za Ikondo, Matembwe na Lupembe na ziada itakayobaki inaingizwa kwenye gridi ya Taifa.
" Habari njema ni kuwa tayari vijiji Saba vimeunganishiwa umeme kupitia mradi huu, hii inatimiza moja ya malengo ya Serikali ya kuhamasisha na kuwezesha upatikanaji wa nishati bora katika maeneo ya vijijini kupitia asasi za kiraia," alisema Dkt. Kalemani.

Alisema kuwa, hadi kufikia mwezi Juni, 2016 idadi ya wananchi wanaopata huduma ya umeme imefikia asilimia 40 huku vijijini ikiwa ni asilimia 24 na kueleza   kuwa juhudi zaidi zinafanyika ili kufikia lengo la kuunganisha umeme kwa asilimia 75 ya wananchi ifikapo mwaka 2025.
Aidha, Dkt. Kalemani aliwasisitiza wananchi wanaoishi karibu na vyanzo vya maji, kuhakikisha kuwa wanavitunza vyanzo hivyo na mazingira kwa ujumla ili kuweza kuwa na miradi ya mafanikio kama huo wa Ikondo.

Awali Meneja Mradi kutoka CEFA, Jacopo Pendezza alisema kuwa Taasisi hiyo ipo nchini kutoka mwaka 1976 na imejikita katika miradi ya umeme vijijini na ina miradi mbali mbali ya umeme inayofanya kazi katika Kata ya Matembwe, Boma la Ng'ombe na Ikondo mkoani Njombe.

Alisema kuwa awali mradi huo wa umeme wa Ikondo ulikuwa unazalisha Kilowati 80 za umeme lakini kutokana na mahitaji ya wananchi kuongezeka, CEFA kwa kushirikiana na kampuni ya kijiji cha Matembwe (MVP) inayosimamia mradi huo, waliamua kuongeza mtambo wa Kilowati 350 na hivyo kupelekea mradi huo kuzalisha jumla ya kilowati 430 za umeme.

Alisema kuwa umeme huo umeleta faida mbalimbali ikiwemo uanzishwaji wa miradi mbalimbali ambayo inawaletea wananchi kipato ikiwemo kiwanda cha kutengeneza chakula cha mifugo, soseji, mafuta ya kupikia, na kutumika katika shughuli za useremala na ushonaji wa nguo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa EU katika uzinduzi huo,  Jenny Nunes alisema kuwa mradi huo utakuwa na manufaa mbalimbali ikiwemo kuboresha maisha ya wananchi kiuchumi, kusaidia wanafunzi katika masomo na huduma nyingine muhimu za kijamii, na kusaidia juhudi za kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.

Alisema kuwa EU itaendelea kusaidia miradi ya umeme nchini ili wananchi wengi wapate nishati hiyo muhimu na kwamba zaidi ya shilingi  bilioni 400 zitatumika  kwa ajili ya sekta husika.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Rehema Nchimbi alisema kuwa makao makuu ya wilaya zote mkoani Njombe, yameunganishwa na  huduma ya umeme na kwamba vijiji 250 kati ya 384 katika Mkoa huo tayari vinapata huduma ya umeme.

Alisema kuwa mkoa huo unazalisha mazao mbalimbali ikiwemo Chai, ambapo ili kuongezea thamani ya mazao hayo, lazima kuwe na umeme wa uhakika utakaosambazwa katika vijiji vyote vya Mkoa husika.

No comments: