Thursday, October 13, 2016

WANANCHI WAASWA KUTOA TAARIFA WANAPOPATWA NA MADHARA YA DAWA.

Na Ally Daud-MAELEZO

WANANCHI waaswa kutoa taarifa pale wanapohisi wamepata madhara ya dawa wanazozitumia ili kuirahisishia Wizara ya Afya kupitia Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kuchukua hatua stahiki zidi ya watengenezaji wa dawa hizo ili zisiendelee kuwadhuru wananchi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu kwenye hafla ya uzinduzi wa mfumo wa kielektroniki wa utoaji wa taarifa za madhara ya dawa uliofanyika jijini Dar es salaam.

Waziri Ummy amesema kuwa wananchi wawe mstari wa mbele katika kutoa taarifa pindi wanapohisi kupatwa na madhara ya dawa wanazozitumia ili kuirahishia TFDA kuchukua hatua stahiki kutokana na taratibu na sheria zilizopo za kuondoa madawa feki nchini.

“Napenda kusisitiza kwa wananchi wote kutoa taarifa pale wanapohisi wamepata madhara ya dawa ili kuirahishia TFDA kuchukua hatua stahiki kutokana na utaratibu na sheria zilizowekwa” alisema Waziri Ummy.

Aidha Waziri Ummy amesema kuwa bila taarifa hizi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia TFDA itashindwa kuchukua hatua muafaka na za haraka katika kudhibiti madhara yanayotokana na matumizi ya dawa na hivyo kuendelea kusababisha athari kwa watumiaji.

Waziri Ummy amesema kuwa wataalam wa afya na wananchi wote kwa ujumla wanatakiwa kutoa taarifa za madhara ya dawa kwa wakati, kwa wale wenye simu zilizounganishwa kwenye “internet” watumie simu hizo kutoa taarifa za madhara ya dawa, na wale wenye kompyuta zilizounganishwa kwenye “internet” watumie kompyuta hizo na wale wasio na simu wala kompyuta zilizounganishwa kwenye “internet “waendelee kutoa taarifa kwa kutumia fomu za njano na kijani.

Mbali na hayo Mkurugenzi Mkuu wa TFDA Bw. Hiiti Sillo amesema kuwa ujazaji wa taarifa hizo kwa kutumia njia za kielektroniki kunasaidia kujua dawa zipi ni sahihi na zipi si sahihi kwa matumizi ya binadamu na hivyo kuchukua hatua inayostahili.

“Napenda kuwaambia wananchi wajaze fomu hizo ili kutoa taarifa za madhara ya dawa wanazozitumia ili kufahamu dawa zipi ni sahihi kwa matumizi ya binadamu na kama sio sahihi basi tuzichukulie hatua zinazostahili” alisema Bw. Sillo.

Aidha Bw. Sillo amesema kuwa moja ya hatua ambayo zitachukuliwa pindi taarifa za madhara ya dawa zinapotolewa ni kufungia kiwanda kinachotengeneza aina hiyo ya dawa au kusimamisha matumizi yake ili kuondoa dawa zinazoleta madhara kwa watanzania.
Afisa wa Uthibiti wa Majaribio na Usalama wa Dawa (TFDA)Dkt. Alex Nkayamba kushoto akimpa maelekezo Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu kuhusu mfumo wa wa kielektroniki wa utoaji wa taarifa za madhara ya dawa unavyopatikana kwenye simu za mkononi wakati wa hafla yauzinduzi wa huduma hiyo uliofanyika jijini Dar es salaam, Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa TFDA Bw. Hiiti Sillo.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wa kwanza kushoto akiangalia jinsi mfumo wa wa kielektroniki wa utoaji wa taarifa za madhara ya dawa unavyofanya kazi katika kutoa tarifa wakati wa hafla ya uzinduzi wa huduma hiyo, wa pili kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa TFDA Bw. Hiiti Sillo.
Wadau mbalimbali wa vyakula na dawa wakifuatilia kwa makini maelezo ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu hayupo pichani wakati wa uzinduzi wa mfumo wa wa kielektroniki wa utoaji wa taarifa za madhara ya dawa uliyofanyika hivi karibuni Jijini Dar es salaam.

No comments: