Wednesday, October 26, 2016

NEEC yawataka Wadau kutoa maoni kupata sera mpya

Katibu Mtendaji wa Baraza Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ((NEEC), Bi. Beng’i Issa, akifungua Jijini Dar es Salaam majadiliano ya tathimi ya Ripoti juu ya Sera ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya Mwaka 2004. (Kushoto) ni Afisa Mchambuzi wa Miradi (Program Analyst UN Women’s Economic Empowerment), Bi.Tertula Swai na (kulia) ni afisa kutoka baraza hilo, Bw. Edward Kessy.
Wadau kutoka taasisi za serikali na asasi za kiraia wakifuatilia taarifa ya tathimini ya Ripoti juu ya Sera Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya 2004 ya Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ((NEEC) katika mkutano wao Jijini Dar es Salaam jana. Tathimini hiyo iliwasilishwa na mwezeshaji wa Mkutano, Mchumi Mwandamizi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma,Bw. Elias Luvanda (hayuko pichani).

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wanchi Kiuchumi (NEEC) limetangaza Jijini Dar es Salaam kwamba linaandaa sera mpya ya uwezeshaji wananchi kiuchumi  na limealika wadau kutoa maoni ili kupata sera itakayokidhi matakwa ya makundi yote katika jamii.

Akifungua mkutano wa majadiliaono tathimi ya Ripoti ya Sera ya Uwezeshaji Wananchi kiuchumi ya mwaka 2004 ya Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ((NEEC),Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Bi. Beng’i Issa, amesema baraza linawaalima wadau  kutoa mapendekezo yatakayosaidi kuandaa sera mpya badala ya sera ya sasa ya 2004.

“Tunahitaji kuwa na sera mpya na inayozingatia maoni ya wananchi, hivyo maoni ya wadau ni muhimu.  Tutaanza na maoni ya wajumbe wa mkutano huu,” amesema Bi. Issa akishangiliwa na wajumbe.

Wajumbe wanajadili ripoti ya tathimini juu ya Sera ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ya 2004 ambayo imeandaliwa na wataalamu wateule ambao wamekutana na wananchi na taasisi mbali mbali katika mikoa 12 ikiwemo ya Jombe, Ruvuma, Mbeya, Manyara, Arusha, Geita, Kilimanjaro,Tanga Mwanza, Kigoma na Dodoma.

Katibu Mtendaji ameeleza kuwa sera ya sasa imeleta mafaniko makubwa katika sekta mbalimbali zikiwemo za barabara, mawasiliano, nishati, miundombinu, ujuzi au maarifa), uwekezaji, na kuongeza kwamba   sera mpya itazingatia na kuboresha masuala iliyonayo na kuingiza mapya yakiwemo ya jinsia.

Amesema  dhamira ya kuwa na sera mpya  ni kusaidia wananchi wote kushiriki katika uchumi wa taifa  na kuharakisha shughuli za maendeleo. Ofisa Mipango (Programme Officer) wa Tanzania Forest Fund, Bi. Patricia Manonga, alisema mila na desturi za Tanzania vinamnyima mwanamke  haki ya kumiliki mali pamoja na serikali  kuweka mkazo katika jambo hili.

“Tumeona vyama vya ushirika vikiwakomboa wanawake kupitia vikundi kama vya VICOBA. Tunatarajia sera mpya itoe msukumo zaidi wa kuwawezesha mwanamke kujikomboa”,amesema,Bi. Manonga.

Mwenyekiti wa Tanzania Informal Microfinance Association of Practitioners (TIMAP),Bw. Ramadhan Ahunga amesema baada ya sera mpya kupitishwa baraza lijipange   kuielimisha jamii kutambua fursa za kiuchumi. “Sera na sheria huwa zinatungwa lakini wananchi wengi wanakuwa hawazifahamu na  kwa hiyo hushindwa kuzitambua  fursa mbalimbaili za kuwasaidia kushinda umasikini,” amesema Bw Ahunga.

Mwezeshaji wa Mkutano,  ambaye ni Mchumi Mwandamizi,  Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma,Bw. Elias Luvanda, amesema wakati wa kukusanya maoni wananchi wengi wamesema kuwa hawaridhiki na sera ya sasa. “Wananchi  wanataka sera na mifumo ya sheria vinafanyiwe marekebisho ili kupanua fursa za kupata maendeleo,” amesema Bw Luvanda.

Wataalamu wametumia fursa hiyo kuwashauri  vijijini kuirasimisha ardhi yao na kupata hati ili watumie ardhi yao kwa tija katika shughuli za kimaendeleo. Mkutano umeshirikisha zaidi ya wadau 100 na mapendekezo yao yatazingatiwa katika kupata sera mpya.

No comments: