Friday, September 30, 2016

WIZARA YA AFYA YAUPONGEZA MKOA WA SINGIDA KWA KUTOA HUDUMA ZA KIBINGWA KATIKA NGAZI YA HALMASHAURI..

 Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J Mtigumwe (katikati) akizungumza na wagonjwa, kulia kwake ni Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki na kushoto ni Mkurugenzi wa tiba kutoka wizara ya afya Dokta Magreth Mhando.
 Wagonjwa waliofanyiwa operesheni ya macho na madaktari bingwa wakizungumza na Mkuu wa Mkoa (hayupo).
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J Mtigumwe (katikati) akizungumza na mgonjwa (hayupo pichani), kushoto kwake ni Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki.
 Wagonjwa wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa alipowatembelea na kuona huduma za mkoba za kibingwa zikiendelea kutolewa, wagonjwa hao walikuwa wakisubiri kuonana na daktari bingwa wa magonjwa ya akina mama.
 Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J Mtigumwe akitembelea na kukagua huduma wanazopatiwa wagonjwa wa huduma za kibingwa katika hospitali ya Mt calorus Mtinko, kulia kwake ni Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki na kushoto ni Mkurugenzi wa tiba kutoka wizara ya afya Dokta Magreth Mhando.
.Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew J Mtigumwe akisikiliza maoni ya wagonjwa waliokuwa wakisubiri kupata huduma za kibingwa kushoto kwake ni  Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki na  anayefuata wa kwanza ni Mkurugenzi wa tiba kutoka wizara ya afya Dokta Magreth Mhando.

Grace Singida.

Wizara ya afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee imeishauri mikoa yote ya Tanzania bara kuiga mfano wa mkoa wa Singida wa kuanzisha huduma za kibingwa za mkoba kwa ngazi za wilaya ili kuwafikia watanzania wengi wenye uhitaji.

Mkurugenzi wa tiba kutoka wizara hiyo Dokta Magreth Mhando ametoa ushauri huo katika hospitali ya Mtakatifu Calorus Mtinko Singida Vijijini alipotembelea kujionea awamu ya pili ya zoezi la huduma za kibingwa za Mkoba. Dokta Mhando amesema kumekuwa na huduma za kibingwa za mkoba ila hazikufanyika vizuri kama ambavyo mkoa wa Singida umekuwa ukifanya na kutoa pongezi za Wizara kwa Mkuu wa mkoa na Mganga mkuu wa mkoa kwa ubunifu huo.

Amesema huduma za kibingwa za mkoba zimekuwa zikiratibiwa na taasisi au hospital kubwa kama Muhimbili ambapo madaktari bingwa wamekuwa wakitoa huduma kwa ugonjwa fulani na kwa ngazi ya hospitali za Mkoa tofauti na zoezi linaloendelea Mkoani Singida la kutoa huduma za kibingwa kwa magonjwa mbalimbali.

Dokta Mhando ameongeza kuwa kutokana na uhaba wa madaktari bingwa nchini wizara imetenga fedha kwa ajili ya kuwasomesha madaktari na kuwashauri waajiri ambao ni makatibu tawala wa mikoa na wakurugenzi wa halmashauri kutenga fedha kwa ajili ya kuwasomesha madaktari hao kwakwuwa wizara pekee haitaweza.

Amesema utaratibu ni kuwa na madaktri bingwa angalau watano kila Mkoa lakini mikoa mingi haina idadi hiyo huku akiongeza kuwa lengo la kutembelea zoezi hilo Singida nikujionea hali halisi na sio kusubiria taarifa.

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhandisi Mathew John Mtigumwe mara baada ya kutembelea wodi zote na kuzungumza na wagonjwa waliopata huduma za kibingwa amemtaka Mganga Mkuu wa Mkoa kuongeza muda wa kutoa huduma hiyo kutoka siku tano hadi nane kutokana na wingi wa wagonjwa waliojitokeza.

Mhandisi Mtigumwe amesema huduma hiyo inasaidia kutambua magonjwa na kuyatibu kabla hayajawa sugu lakini pia gharama zikiwa nafuu kutokana na kusogezwa kwa ngazi za halmashauri. Ameongeza kuwa lengo la ofisi yake ni kuhakikisha huduma za kibingwa za mkoba zinapelekwa kwa kila halmashauri na endapo zoezi likikamilika na kukiwa na uhitaji mkubwa kuna uwezekano mkubwa wa kurudia zoezi hilo.

Mhandisi Mtigumwe amesema kuelekea Tanzania ya viwanda afya bora ni muhimu na wazalishaji wakubwa ni wananchi wa ngazi za chini hivyo huduma hiyo itasaidia kuimarisha afya ili waweze kuzalisha bidhaa kwa wingi na zenye ubora.

Amesema kwa wale wagonjwa watakaopewa rufaa kwenda nje ya Mkoa utaratibu utaangalia wa kuwapatia usafiri wa Mkoa ili kuwapeleka hasa wale wasiojiweza. Naye Mganga Mkuu wa Mkoa Dokta John Mwombeki amesema kwa muda wa siku tano wagonjwa zaidi ya 800 wameonana na madaktari bingwa huku idadi ikitarajiwa kuongezeka kutokana nakuongezwa kwa siku za klutoa huduma.

Dokta Mwombeki amesema wagonjwa wengi wanaofika wanatoka maeneo mbalimbali hasa maeneo ya kijijini na wenye hali duni ya maisha hivyo zoezi hilo limesaidia wananchi hasa wwenye kipato cha chini. Amesema madaktari bingwa wanaotoa huduma za kibingwa za mkoba ni madaktari bingwa wa magonjwa ya akina mama, watoto, macho, meno, magonjwa ya ndani na daktari bingwa wa upasuaji.

Wagonjwa waliopata huduma wameushukuru uongozi wa mkoa kwa kubuni utaratibu wa kuwafuata wagonjwa karibu ili kuwapatia huduma za kibingwa kwakuwa inawasaidia kupata matibabu mapema kabla magonjwa hayajawa sugu na kushauri huduma iwe endelevu angalau kila mwaka.

No comments: