Wednesday, August 17, 2016

DC MTATURU AKEMEA SIASA TAKA ZINAZOCHANGIA KURUDISHA NYUMA MAENDELEO YA WANANCHI


Baadhi ya wagonjwa wakiwa katika hali ya ahueni mara baada ya kulazwa katika Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu iliyopo katika Kijiji cha Puma
Dc Mtaturu Mtaturu akiwasisitiza watumishi wa Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu kujiunga na mfuko wa Bima ya Afya ili wawe mabalozi katika kuwashawishi wananchi nao kujiunga katika mfuko huo
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akiwa katika picha ya pamoja na watumishi ngazi ya juu katika Hospitali ya teule ya Makiungu pamoja na baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya
Dc Mtaturu akisisitiza jambo kuhusu utoaji bora wa huduma za afya
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akiwasalimu baadhi ya wagonjwa ambao wamefikakupatiwa tiba hospitalini
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika ofisi za Mganga Mkuu wa Hospitali Teuli ya Makiungu
Baadhi ya watumishi wakisikiliza kwa makini hotuba ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akiwasisitiza wanawake wajawazito kuhudhuria Kliniki wiki 12 za mwanzo mara baada ya kuhisi kuwa ni wajawazito sawia na kuwashauri kufika Hospitalini wakiwa wameambatana na waume zao


Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akizungumza na watumishi wa Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu iliyopo Kijiji na Kata ya Puma
Dc Mtaturu akizungumza na viongozi wa ngazi ya juu katika Hospitali Teule ya Wilaya ya ikungi Makiungu mara baada ya kuwasili katika Hospitali hiyo
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akikagua jengo jipya linalojengwa kwa ajili ya wodi na baadhi ya Ofisi za Hospitali ya Malkia wa ulimwengu
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Hospitali ya Malkia wa ulimwengu, Na baadhi ya wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama Wilaya
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu akikagua Mtambo wa oxygen jinsi unavyofanya kazi mara baada ya kuzuru katika Hospitali Teuli ya Wilaya


Na Mathias Canal, Singida
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Miraji Jumanne Mtaturu ametoa onyo kwa wanasiasa wanaotumia vibaya madaraka yao kwa kushindwa kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa uchangiaji huduma za afya na badala yake kuwafanya kudumaa kifikra na hatimaye kushindwa kufika hospitalini kupatiwa matibabu hivyo kupelekea vifo vya baadhi ya wananchi ambao wameamini maneno ya kisiasa kuliko kauli za watendaji za kufika Hospitalini kwa ajili ya matibabu.

Ametoa onyo hilo hii leo wakati alipotembelea na kuzungumza na watumishi wa Hospitali teuli ya Makiungu Wilaya ya Ikungi, Mkoani Singida pamoja na Hospitali ya Misheni Cathoric Malkia wa Ulimwengu inayomilikiwa na Shirika la Mothers of the Holy Cross an Missionaries of the Holy Cross.

Mtaturu amesema kuwa serikali inatambua umuhimu na huduma bora zinazotolewa na taasisi za dini katika Wilaya ya Ikungi kwani sekta ya afya ni sehemu muhimu kusukuma maendeleo ya nchi endapo wananchi watakuwa na afya bora itakuwa nguzo yao ya kufanya kazi na kuendana na falsafa ya Serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt John Pombe Magufuli ya Hapa Kazi Tu.

Kauli ya watumishi wa umma ambao wanatumia vyeo vyao vibaya ikiwemo kuzuia wananchi kuchangia shughuli za maendeleo kama vile ujenzi wa Vituo vya afya na Dispensari jambo ambalo linajikita zaidi katika kudhoofisha afya za watanzania waishio katika maeneo ambayo hayana huduma za afya karibu.
Mtaturu amesema kuwa serikali kwa kushirikiana na hospitali hizo ili kuhakikisha kuwa changamoto mbalimbali zinatatuliwa ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vifaa tiba, uwepo wa madaktari bingwa lakini ni muhimu wananchi kuchangia huduma za kijamii hususani sekta ya afya ili kuimarisha afya zao na kupunguza vifo visivyokuwa vya lazima.

Hospitali ya Makiungu ilianzishwa na Masista Wamisionari wa huduma ya tiba mnamo mwaka 1954 kwa mwaliko wa Baba Askofu Winters aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Singida wakati ule na ndio ilikuwa Taasisi ya kwanza kutoa huduma za afya katika Mkoa wa Singida.

Pamoja na huduma za tiba katika Hospitali ya Makiungu pia inatoa huduma za kinga kwa vijiji vilivyo karibu na hospitali katika vituo vitano kwa njia ya kiliniki tembezi walengwa wakuu wakiwa ni wajawazito na watoto wenye umri chini ya Miaka mitano.

Dc Mtaturu amesema kuwa katika Wilaya ya Ikungi kuna jumla ya Zahanati 34 katika Vijiji 34 pekee kati ya Vijiji 101 vilivyopo Wilayani humo kinyume kabisa na sera ya Taifa inavyoelekeza ya kuwa na Zahanati kwa kila Kijiji ili kupunguza kadhia wanazokumbana nazo madaktari bingwa kwa kuwahudumia wagonjwa wenye mafua badala ya magonjwa sugu na makubwa.

Amesema kuwa uchache na kusuasua kwa ujenzi na upatikanaji wa huduma za afya umechagizwa na kauli za kisiasa za kuzuia wananchi kuchangia shughuli za maendeleo jambo ambalo linazidi kurudisha nyuma maendeleo ya Vijiji, Tarafa, Wilaya, Mkoa na Taifa kwa ujumla.

Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu inahudumia wagonjwa wa ndani ya Wilaya ya Ikungi na Wilaya nyingine za Mkoa wa Singida na hata nje ya Mkoa wa Singida kama Shinyanga, Manyara, Tanga, Dodoma, Mwanza, Arusha na hata nchi jirani kama vile Kenya na Malawi.

"Changamoto zote mlizo nazo tumezichukua na serikali itazifanyia kazi haraka iwezekanavyo ili kuinua huduma za afya na kuokoa vifo vya wananchi kisa matamko ya kisiasa, Lakini pia nataka niwakumbushe kuwa siasa zilishamalizika Tarehe 25 mwezi Octoba mwaka jana baada ya wananchi kufanya maamuzi yao kwenye uchaguzi Mkuu hivyo huu ni muda wa kufanya kazi kama ambavyo tumekuwa tukimsikia Rais akisema, Kwahiyo kuanzia leo sitaki siasa taka zenye kurudisha nyuma shughuli za maendeleo" Alisema Mtaturu

Aidha Dc Mtaturu amewapongeza watumishi wote katika Hospitali hizo mbili kwa jinsi ambavyo wanawahudumia wananchi kwa moyo mkunjufu pamoja na uchache wa vifaa tiba pamoja na uchache wa madaktari na Wauguzi lakini ameziomba Hospitali hizo kupunguza gharama za Dawa kwani kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi juu ya gharama kubwa zinazotakiwa baada ya matibabu sawia na kuwataka watumishi wote kutumia lugha nzuri kwa wagonjwa ili wagonjwa hao kupata tiba kwa amani na upendo.

Akisoma risala kwa mgeni rasmi kwa ajili ya Hospitali Teule ya Wilaya ya Makiungu Afisa utumishi katika hospitali hiyo, Mary Shirima ameiomba serikali kusaidia upatikanaji wa gari la wagonjwa katika Hospitali hiyo ambalo litafanya kazi masaa 24 ili kusaidia kupunguza vifo vya akina mama wajawazito ambao wengi wao wanaathirika kutokana na umbali wanaotoka kwa ajili ya kufika hospitalini kupatiwa tiba.

Shirima alisema kuwa mbali na gari la kubeba wagonjwa pia Hospitali hiyo inaidai serikali jumla ya shilingi milioni 466,072,500/= ikiwa ni fedha za serikali na baadhi ya watumishi ambao serikali imeshindwa kuwalipa watumishi katika kipindi cha mwaka mzima baada ya kusaini mkataba na Askofu wa Jimbo katoliki la Singida wa Hospitali ya Makiungu kuwa teule mwaka 2008.

Kwa upande wake Diwani wa Viti maalumu Tarafa ya Ihanja Rabeka Ntandu Chaimbo Amempongeza Mkuu huyo wa Wilaya kwa kuzuru katika Taasisi hizo zinazotoa huduma za afya kwa wananchi kwani zimekuwa msaada mkubwa kwa Wilaya ya Ikungi sambamba na Wilaya na Mikoa mingine nchini.

Naye Mkurugenzi wa Hospitali ya Malkia wa Ulimwengu Padri Manoel Tsino amesema kuwa wananchi wanapaswa kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya (CHF) ili kuwa na uhakika wa huduma bora ili pindi wanapoenda kupatiwa matibabu iwe rahisi kwao.

Sawia na ushauri huo kwa wanachi Padri Tsino pia amewashauri watumishi wote wa Hospitali hiyo kujiunga na mfuko wa Bima ya Afya kufikia mwishoni mwa mwezi huu ili kuwa mfano bora kwa wananchi ambao hawajajiunga na mfuko huo.

Ziara ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu hii leo ni ziara ya kwanza kuzitembelea Taasisi hizo tangu alipoteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo.

No comments: