Monday, July 18, 2016

WAZIRI MBARAWA AITAKA TPA KUJENGA GATI

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemuagiza  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA), kuanza ujenzi wa maegesho ya meli katika bandari ambazo meli mbili mpya zinazojengwa na Mamlaka hiyo katika bandari ya Itungi Wilayani Kyela, zitatoa huduma ya usafiri baada ya kukamilika.

Waziri Prof. Mbarawa ametoa agizo hilo alipokagua bandari ya Mbambabay iliyopo Wilayani Nyasa ambayo ni miongoni mwa bandari ambazo meli hizo zitatoa huduma na kubaini kuwa bado bandari hiyo haina maegesho kwa ajili ya meli hizo.

"Nataka kuona maegesho ya meli yanakamilika haraka ili kuwezesha meli mpya kupakua na kupakia mizigo katika bandari hii", amesema Waziri Prof Mbarawa.

Ameeleza kuwa meli hizo mbili za mizigo ambazo zinatarajiwa kukamilika mwezi Agosti na Oktoba zitaongeza kasi ya utoaji wa huduma katika bandari hiyo na kuwa chachu ya maendeleo hususan katika shughuli za biashara na kiuchumi katika mkoa wa Ruvuma na nchi jirani.

Aidha, Waziri Prof. Mbarawa amemtaka Meneja wa Bandari ya Kyela kuisimamia kampuni ya M/s Songoro Marine Transport Boart Yard inayojenga meli hizo ili zijengwe kwa ubora na viwango vinavyotakiwa kulingana na thamani ya fedha ambazo zinatokana na kodi za wananchi.

Katika Hatua nyingine Waziri Prof. Mbarawa amekagua barabara ya Mbinga- Mbambabay yenye urefu wa Km 66 ambayo Serikali iko katika hatua ya kumtafuta mkandarasi atakayejenga kwa kiwango cha lami.

Ameongeza kuwa kukamilika kwa barabara hiyo kutaimarisha huduma ya bandari ya Mbambabay na kupunguza adha ya usafiri kwa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa Ruvuma Eng. Lazeck Alinanuswe amesema kuwa kwa sasa wakala unakamilisha zoezi la kulipa fidia kwa wananchi waliopo katika hifadhi ya barabara wakati hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa zinakamilishwa.

Naye Meneja wa Bandari ya Kyela Percival Salama amemueleza Waziri kuwa pamoja na changamoto ya kukosa wa chombo cha usafiri majini kinachotoa huduma katika bandari hiyo pia ameomba kuboresha huduma za miundombinu ya barabara kwa kiwango cha lami ili kuwezesha ufanisi wa bandari.

"Kuimarika kwa barabara ya  mbinga-mbambabay na barabara nyingine za maingiliano katika bandari hii  kutaongeza ufanisi katika utendaji kazi na kuongeza fursa za uwekezaji na biashara na Mkoa na nchi jirani", Waziri Prof. akame Mbarawa, yuko katika ziara ya Kikazi Mkoani Ruvuma kukagua miradi ya Sekta ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Meneja wa Bandari ya Kyela, Percival Salama (wa kwanza kushoto) akitoa maelezo kwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) ya namna shughuli za biashara ya makaa ya Mawe zinavyoweza kuongeza pato kwa bandari ya Bambabay Mkoani Ruvuma.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa kwanza kulia) akisalimiana na baadhi ya Madereva wa Malori wanaosafirisha makaa ya mawe Mkoani Ruvuma.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akizungumza na watendaji wa taasisi zilizo chini ya Wizara hiyo, Mkoani Ruvuma.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) akiongea jambo na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma,Dkt. Binilith Mahenge (wa pili kushoto) wakati alipokagua uwanja wa Songea Mkoani Ruvuma.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa pili kulia) akiongea jambo na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma,Dkt. Binilith Mahenge (wa pili kushoto) wakati alipokagua uwanja wa Songea Mkoani Ruvuma.
Muonekano wa uwanja wa ndege wa Songea Mkoa ni Ruvuma, ambao uko kwenye mradi wa upanuzi wa viwanja kumi na moja.
Waziri wa Ujenzi, Uchuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa (wa tano kushoto) akitoa maelekezo kwa Meneja wa kiwanja cha ndege cha Songea, Valentine Fasha (wan ne kulia) wakati alipokagua barabara ya kutua na kuruka ndege katika uwanja huo Mkoani Ruvuma.
Muonekano wa Barabara ya Mbinga-Mbambabay KM 66 ambayo ujenzi wake kwa kiwango cha Lami unatarajiwa kuanza hivi karibuni. Kukamilika kwa barabara hiyo kutachochea uchumi wa Mkoa wa Ruvuma kupitia bandari ya Mbambabay.

No comments: