Monday, July 25, 2016

Serikali yafanya mazungumzo na Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu nchini.

Kaimu Mkurgenzi, Idara ya Maendeleo ya Sanaa, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bi. Leah Kihimbi (kulia) akiongea na baadhi ya Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu Tanzania (hawapo pichani) kuhusu maendeleo ya sekta ya sanaa nchini wakati alipokutana nao hivi karibuni Wizarani hapo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu wa Bodi ya Filamu Tanzania, Bi. Joyce Fissoo.
Katibu wa Bodi ya Filamu Tanzania, Bi. Joyce Fissoo (kulia) akisistiza jambo mbele ya baadhi ya Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu Tanzania (hawapo pichani) kuhusu maendeleo ya sekta ya sanaa nchini wakati wa kikao hicho Wizarani hapo jijini Dar es Salaam.

Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Bw. Simon Mwakifwamba akieleza jambo mbele ya Viongozi wa Serikali pamoja na baadhi ya Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu Tanzania (hawapo pichani) kuhusu masuala ya sanaa nchini wakati wa kikao hicho Wizarani hapo jijini Dar es Salaam.


Baadhi ya Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu Tanzania wakichangia mada kuhusu maendeleo ya sekya ta Sanaa nchini wakati wa Kikao na Viongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa upande wa Sekta ya Sanaa kilichofanyika hivi karibuni Wizarani hapo.

 (Picha/Habari na Benedict Liwenga-WHUSM)


Serikali imekutana na kufanya mazungumzo na baadhi ya Viongozi wa Mashirikisho ya Filamu nchini ikiwa ni sehemu ya kubaini changamoto mbalimbali zinazoyakabili Mashirikisho hayo.

Akiongea hivi karibuni jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Sanaa, Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bi. Leah Kihimbi alisema kwamba, Mashirikisho yanayounda Shirikisho la Filamu nchini hayanabudi kushirikiana kwa karibu na Serikali ili kubaini changamoto na namna ya kuzitatua kwa manufaa ya Wasanii na Taifa kwa ujumla.

Alieeleza kuwa, Wasanii wanapaswa kuzingatia maadili wakati wanapofanya kazi zao za sanaa ili waweze kujijengea heshima kwao, kwa jamii ambayo ndio mlaji wa kazi zao za kisanaa na kwa Taifa kwa ujumla.

“Mnapofanya kazi zenu za sanaa, jitahidini kufuata miiko ya kazi zenu, tumieni vipaji vyenu vizuri kwa kufuata maadili ya Kitanzania, lakini pia jitahidini kuwainua wale wasanii wanaochipukia ama wale wadogo ili waweze kuwa na hamasa ya kuendeleza kazi zao za sanaa”, alisema, Bi. Kihimbi.

Bi. Kihimbi aligusia suala la fursa ya kazi za sanaa inayodhaminiwa na Taasisi ya British Council Tanzania na kuwataka wasanii kuchangamkia fursa hiyo kwa kuhakikisha kuwa kila msanii au kikundi kinaandika Pendekezo (Proposal) kuhusu fursa hiyo ili kujiwekea nafasi kubwa kwa wasanii wa Tanzania kushinda fursa hiyo na kuweza kupata fedha za kuendesha kazi za sanaa kulingana na wazo lililobuniwa.

“Kuweni wabunifu katika hii fursa ili mje na wazo zuri ambalo litawawezesha kushinda hii fursa hasa hii ya nAnA (new Arts new Audiences) kwani inamhusu msanii mmoja mmoja au kikundi”, alisema, Bi. Kihimbi.

Aliongeza kuwa, Serikali itajitahidi kutatua baadhi ya changamoto ambazo zinaonekana kuwa kero kwa wasanii nchini ikiwemo suala la wizi wa kazi za sanaa (Piracy) ambalo kwa sasa tayari Waziri mwenye dhamana katika Wizara hiyo, Mhe. Nape Nnauye ameonyesha mfano kwa kukamata DVDs feki pamoja na mitambo ikiyotumika kudurufu kazi hizo za sanaa nchini.

Kwa upande wake, Katibu wa Bodi ya Filamu Tanzania, Bi. Joyce Fissoo alisema kwamba Bodi yake inashirikiana vema na wasanii nchini kwa kuzingatia Sheria za nchi pasipo kumuonea msanii yeyote na kuwataka wasanii kote kuendeleza uhusiano huo mzuri uliopo kwa manufaa yao na Taifa kwa ujumla.

Aidha, aliwataka viongozi wa Shirikisho hilo la Sanaa kuendelea na utaratibu wa kupeana taarifa kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu sanaa na kuwahimiza wasanii kupenda kujiendeleza kielimu ili waweze kumudu soko huku akiwasisitiza kuhakikisha kuwa kazi zao wanazotengeneza zinapata kibali cha Bodi kwa kuwekewa madaraja na zinakuwa na stika halali ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ili kuepusha uharamia wa kazi zao.

Naye Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Bw. Simon Mwakifwamba ameiomba Serikali kuendelea kushirikiana na Wasanii kwa karibu kwa kuzifanyia kazi baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo na ikiwemo suala la uharakishaji wa Sera ya Filamu kwani ndiyo kipaumbele chao cha kwanza, elimu ya namna ya kutengeneza filamu bora, usambazaji wa kazi zao pamoja na adui yao mkubwa ambaye ni uharamia wa kazi za sanaa.


Ameishukuru Serikali kwa kuunda Sekta mpya ya Sanaa na kusema kuwa, Sekta hiyo itakuwa Mkombozi kwao kwani wanajisikia fahari kutambuliwa na kuwa na kitengo chao cha masuala ya kazi zao huku akiaahidi ushirikiano mzuri kwa sekta hiyo.

No comments: