Tuesday, July 19, 2016

CHANZO CHA MOTO KIWANDA CHA NGUO MOROGORO CHAFAHAMIKA

Na John Nditi, Morogoro

MOTO mkubwa umeteketeza Jengo la Idara ya Uzalishaji la  Kiwanda cha  21st Century Textiles  Ltd ambapo zamani kabla ya kubinafsishwa na Serikali kilijulikana  kwa jina la Morogoro Polyester Textile Ltd  ambapo bado haikujulikana  hasara iliyopatikana. 

Moto huo  ulianza  majira ya saa 12: 45 asubuhi ya Julai 19, mwaka huu kwenye  Kiwanda hicho kilichopo eneo  Viwanda Kihonda, Manispaa ya Morogoro.

 Kufuatia kutokea kwa moto huo, Kikosi cha Jeshi la  Uokoaji na Zimamoto kwa kushirikiana na Polisi walifika eneo la tukio mara moja na kuanza kazi ya  kuzima  moto uliokuwa ukiwaka kwa nguvu juu ya paa la Jengo hilo .
Kamanda wa mkoa wa Morogoro , Jeshi la Uokoaji na Zimamoto, Ramadhan Pilipili, alisema licha ya kuwahi eneo la tukio, bado walikabiliana na ugumu wa kuingia ndani  hivyo kulazimika kutoboa ukuta kwa kutumia katapira ili  kupata nafasi ya uwazi ya kurusha maji  ndaniya jengo ili  kuuzima.

Hivyo alisema , ndani ya jengo hilo kulikuwa na  marotoba ya pamba  ambayo yalishika  moto  na kuwawia vigumu kuingia ndani  na kulazimika kwanza kutoboa sehemu za ukuta wa jengo ili kupenyeza maji  yatakayowezesha  kuuzima moto  huo.  

Kamanda wa mkoa wa Jeshi la Uokoaji na Zimamoto alisema  jitihada  za kuuzima moto huo  zilikuwa zinaendelea hadi majira ya saa tisa alasiri ambapo pia waliungana na timu ya askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuezesha zoezi la kuuzima moto huo.
Katika tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Ulrich  Matei aliungana na viongozi wengine  na vikosi hivyo ili  kuona moto huo unadhibitiwa ili usiweze kuleta madhara makubwa zaidi.

Kwa upande wake  Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Dk Kebwe Stephen Kebwe aliyefika kujioenea tukio hilo  alitumia fursa hiyo kuuagiza  uongozi wa Jeshi la Uokoaji na Zimamoto mkoa kufanya ukaguzi wa mara kwa mara katika viwanda.

Dk Kebwe alisema , lengo ni kuona  maeneo ya viwanda vinakuwepo  vifaa vya dharura vinavyofanya kazi ya kuzima moto  unapojitokeza ikiwemo na maeneo mengine  ya majengo ya matumizi ya mkusanyiko wa kazi.
“ Maeneo kama haya ya viwanda ni lazima kuwepo na vitu vya tahadhari , kama sehemu za kuchota maji , vifaa vya kuzimia moto viwemo  ndani ya viwanda na maeneo mengine  ili  moto unapozuka iwe ni rahisi kuwahi kuuzima”  alisema Dk Kebwe.

Mbali na hayo, pia mkuu wa mkoa alimwagiza Kamanda wa Polisi wa mkoa kulimaisha ulinzi eneo hilo ili kuzuia vibaka na wezi kuweza kuiba mali zilizopo.

Naye  Meneja  Uzalishaji  Kiwanda cha 21st Century Textiles Ltd, Clemence Munis , alisema kuwa moto huo ulitokea kwenye Idara ya usokotaji wa nyuzi za nguo baada ya moja ya mashine zake kutoa cheche na kurukia katika  marotoba ya pamba na kisha kuwaka moto uliokwenda kunasa kwenye  nyanya za umeme.

Munis alisema  wakati wakianza kuchukua hatua za  kuzima kwa kutumia vifaa vya kuzima  ndani ya kiwanda , walikiarifu  Kikosi cha Jeshi la Uokoaji na Zimamoto pamoja na  Polisi wa mko ambao  walifika katika kipindi cha muda mfupi kiwandani hapo.

“ Moto umetokea majira ya saa moja kasorobo asubuhi ya leo ( Julai 19) sehemu ya uzalishaji baada ya kutokea hitirafu ya umeme kwenye mashine ya kusokota pamba “ alisema Munis.

Kiwanda hicho kina majengo  na  idara mbalimbali ikiwemo ya usokotaji, useketaji na umaliziaji wa nguo na mashine zinazotukika kwa kazi hizo.

 “ Nawapongeza Jeshi la Ukoaji  na Zimamoto Morogoro, wamefika kwa wakati ndani ya dakika 10 na kuanza kuzima moto  wakishirikiana Polisi , wananchi na wafanyakazi wakiume  na ninatumai  zoezi litafanyikiwa kwa haraka na mali nyingi kuokolewa” alisema Munis.

 Munis alisema  hakuna madhara ya kibinadamu , isipo kuwa moto huo umetekeleza marotoba ya pamba ,nguo  na mashine zilizokuwepo katika  idara hiyo  ambapo  bado  kiwango cha gharama halisi ya hasara iliyotokana na moto huo  kujulikana .

“ Bado hatuajua hasara kamili , isipokuwa moto huu umetekeleza mali nyingi hasa marotoba ya pamba, nguo na mashine eneo la idara ya ufumaji wa nguo ...na hii itajulikana baaada ya kufanyika kwa tathimini “ alisema Munis. 

Kiwanda cha  21st Century Textiles , kimuundo ni kampuni tanzu ya Mohamed Enterprises ( TANZANIA) LTD – (MeTL) na ilianza uzalishaji mwaka 2005, baada ya kununua  katika zoezi la ubinafsishaji mali za kampuni ya umma iliyojulikana kwa jina  la MOROGORO POLYESTER TEXTILES LTD.

No comments: