Friday, June 10, 2016

USAJILI WANANCHI VITAMBULISHO VYA TAIFA KUKAMILIKA NCHI NZIMA DESEMBA 31 MWAKA HUU

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) Bi. Rose Mdami, akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo jijini Dar es Saalam. Katika kikao hicho NIDA iliwasilisha mpango usajili kufikia 31 Desemba 2016 ambapo usajili utakamilika nchini nzima na wananchi kuanza kutumia namba ya utambulisho kupata huduma. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Udhibiti Mifumo ya Komputa (TEHAMA) Ndugu Mohamed Khamis, kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji Vitambulisho Ndugu Alphonce Malibiche
Mkurugenzi wa Idara ya Udhibiti Mifumo ya Komputa (TEHAMA) Ndugu Mohamed Khamis, akifafanua namna mwananchi anaweza kutumia tovuti salama kujua taarifa zake wakati wa kikao na waandishi wa Habari katika Ukumbi wa idara ya Habari Maelezo Jijini Dar es salaam. Kushoto ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati wa NIDA Bi Rose Mdami.

Serikali imekusudia kukamilisha Usajili Vitambulisho vya Taifa kwa wananchi wote kufikia Desemba 31 mwaka huu.

Akuzungumza na vyombo vya habari leo, msemaji wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa Bi. Rose Mdami, amesema NIDA imepanga kutumia taarifa za NEC kukamilisha usajili wa awali na kutoa namba ya Utambulisho kwa wananchi wote ambao hawakusajiliwa katika mfumo wa NIDA.

Akifafanua, Bi Rose amesema baada ya kuhakikisha kila mwananchi ana Nambari ya Utambulisho, kila mwananchi atalazimika kukamilisha usajili wake ikiwa ni hatua ya kujaza vipengele vya maswali vilivyobakia katika fomu ya maombi ya vitambulisho kabla ya kupata utambulisho kamili.

“kama mnavyofahamu, katika usajili wa NEC fomu ilikuwa na vipengele 32 vya kujaza kulinganisha na fomu ya NIDA ambayo ina vipengele 74, hivyo ni lazima kila mwananchi kutambua, ili kuwa na utambulisho kamili lazima kujaza vipengele vilivyobaki pamoja na kuambatanisha nakala ya viambata vyake muhimu kuthibitisha taarifa za umri, uraia na makazi” alisisitiza.

Amesema lengo la kuanza kutoa namba ya utambulisho ni kuwawezesha wananchi kuanza kufaidi huduma zinazotolewa, wakati uzalishaji Vitambulisho ukiendelea. Uwezo wa mashine za NIDA ni kuzalisha vitambulisho 24,000 kwa siku hivyo itachukua muda kukamilisha uchapishaji wa vitambulisho kulingana na idadi ya Watanzania, Wageni na Wakimbizi watakao andikishwa.

Akifafanua namna NIDA ilivyojipanga kuhakikisha zoezi la usajili linakamilika kwa wakati iliyojiwekea, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji Vitambulisho Ndugu Alphonce Malibiche, amesema NIDA imeshapokea BVR Kit 5000 na kwakuwa NIDA tayari ilishakuwa na MEU (Mobile Enrolment Unit) 1500, vifaa hivi vitasambazwa nchi nzima mpaka ngazi ya Kata ambapo wananchi watasajiliwa kwa hatua zote; lengo ni kuwafikia wananchi ambao hawakujisajili kupiga kura na vijana wanaotimiza umri wa miaka 18.

“NIDA imejipanga kuchakata taarifa za NEC na kuingiza taarifa hizo katika mfumo wa NIDA utakaoondoa durufu ili kuruhusu majina kupelekwa kwenye Kamati za Ulinzi na Usalama kwa uhakiki pamoja na kuruhusu wananchi kuweka mapingamizi kwa wale wote watakaotiliwa shaka ya uraia”.

Amesema NIDA itatumia mbinu zote katika kusambaza namba za Utambulisho mpaka vijijini, pamoja na kutumia ofisi za NIDA zitakazofunguliwa katika Wilaya zote nchini, kuwezesha kuanza kwa matumizi ya utambulisho yatakayojikita katika huduma mbalimbali zitolewazo nchini.

Akipambanua namna mfumo wa Utambulisho wa Taifa utakavyotumika katika kutoa huduma mbalimbali, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Uchambuzi Mifumo ya Kompyuta ndugu Mohamed Khamis amesema tayari NIDA imeshabuni mifumo mbalimbali itakayotumika kusoma taarifa katika mfumo Mama (Kanzidata) ya NIDA ikiwemo tovuti salama ambayo itamwezesha mtoa huduma kusoma taarifa za mteja wake mahali alipo kwa idhini itakayotolewa na mteja mwenyewe.

Amesema mfumo huu wa kitaalamu umebuniwa katika kumrahisishia mwananchi kupata huduma pamoja na kufuatilia hatua ya usajili wake ilipofikia. Mbali na tovuti salama pia njia ya SMS itatumika kusoma taarifa za mwombaji.

Katika hatua zote hizi suala la usalama wa taarifa limezingatiwa na hakutakuwa na taarifa za mwananchi zitakazosomwa bila idhini ya mhusika ambaye ni mmiliki wa Utambulisho/kitambulisho.

“kupitia mfumo huu wa NIDA Serikali itaweza kubaini na kuondokana kabisa na tatizo la wafanyakazi hewa kwani namba ya utambulisho niya kipekee na hivyo hakutakuwepo durufu ya taarifa” alisema.

Tayari NIDA imeshaanza mazungumzo na Utumishi kufanya usajili wa watumishi Nchi nzima ili mfumo wa mishahara kuunganishwa na mfumo mama wa taarifa (Kanzidata) NIDA.

Mpaka sasa NIDA imekamilisha ujenzi wa miundombinu na kusajili wananchi katika mikoa ya Dar-es- salaam, Pwani, Lindi, Mtwara, Tanga, Morogoro na Zanzibar.

Zaidi ya vitambulisho mil 2.7 vimeshagawanywa kwa wananchi na kuanza matumizi katika baadhi ya huduma zikiwemo za kibenki katika baadhi ya mabenki nchini.

No comments: