Tuesday, March 1, 2016

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI AZINDUA MRADI WA MAJI MKOANI KILIMANJARO

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge amezindua mradi wa maji wa Longuo, katika Kijiji cha Longuo, Wilaya ya Moshi mwishoni mwa wiki katika ziara yake mkoani Kilimanjaro. Mradi huo unaohudumia vijiji vya Longuo na Kariwa, umekuwa faraja kubwa kwa wananchi, ambao kwa muda mrefu walikuwa na tatizo la kupata huduma ya majisafi na salama na kusababisha hatari ya magonjwa ya milipuko kwa wananchi.

Mhe. Lwenge, amefurahishwa na utekelezaji wa mradi huo ambao umechukua siku themanini tu kukamilika, na kuipongeza Mamlaka ya Majisafi na Mazingira Moshi (MUWSA) kwa usimamizi mzuri wa mradi huo. Pia, alitembelea chanzo cha maji, chemchemi ya Kisimeni iliyopo Kata ya Uru Kusini ambayo inachangia uzalishaji wa maji katika Wilaya ya Moshi.

Vilevile, Mhe. Lwenge alitembelea miradi ya maji inayotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Arusha (AUWSA). Katika ziara yake hiyo mkoani Arusha, Waziri wa Maji na Umwagiliaji, aliweza kufika kwenye chanzo cha maji cha Midawe, kilichopo kwenye Mto Nduruma, katika Kijiji cha Bangata, kilichopo Kata ya Bangata, Wilayani Arumeru ambao unachangia asilimia ishirini ya uzalishaji maji kwa Jiji la Arusha. 

Pia, alifika kwenye chanzo cha maji cha chemchemi ya Machare, iliyopo Kata ya Moshono, Wilayani Arumeru iliyovamiwa na wananchi wanaofanya shughuli za kibinadamu kinyume na sheria na kuhatarisha uzalishaji wa maji ya kutosha kwa ajili ya kuhudumia mji wa Arusha.
Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Novatus Makunga akizungumza mbele ya Waziri wa Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge, viongozi na wananchi wa Longuo, Wilayani Moshi.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge akimtwika maji mama katika Kijiji cha Longuo, Wilayani Moshi mara baada ya kuzindua mradi wa maji kijijini hapo.
Jiwe la msingi likiashiria uzinduzi wa mradi wa maji wa Kijiji cha Longuo, Wilayani Moshi.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge akiwa na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Novatus Makunga (kulia) na wajumbe wa Bodi ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Moshi (MUWSA).
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge akiwa na viongozi na wataalamu aliombatana nao kwenye ziara yake kwenye chanzo cha maji cha Midawe, kilichopo kwenye Mto Nduruma, katika Kijiji cha Bangata, kilichopo Kata ya Bangata, Wilayani Arumeru.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Arusha (AUWSA), Inj. Ruth Koya akimuonyesha Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mhe. Inj. Gerson Lwenge moja ya miradi ya maji inayotekelezwa na mamlaka hiyo, Kata ya Moshono, Wilayani Arumeru.

No comments: