Thursday, March 10, 2016

WANDISHI WA HABARI WA ZANZIBAR WATAKIWA KUELIMISHA JAMII JUU YA MARADHI YA KIPINDUPINDU

Mkurugenzi Mtendaji Kamisheni ya Maafa Zanzibar ndugu Ali Juma Hamad akifungua mafunzo ya waandishi wa habari juu ya kujikinga na ugonjwa wa kipindupindu katika Ukumbi wa gereji ya Wizara ya Afya Mombasa Mjini Zanzibar, (kulia) daktari dhamana Kanda ya Unguja Dkt Fadhili Mohd na (kushoto) Mwakilishi wa WHO Zanzibar Dkt. Ghirmay. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.
Washiriki wa mafunzo hayo wakimsikiliza kwa makini Daktari dhamana Kanda ya Unguja Dkt. Fadhili Mohamed alipokuwa akielezea njia za kukabiliana na kipindupindu katika mafunzo ya siku moja yaliyofanyika Ukumbi wa Gereji ya Wizara ya Afya Mombasa Mjini Zanzibar. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo Zanzibar Rafii Haji Mkame akiwasilisha mada ya wajibu wa waandishi wa habari katika kukabiliana na maradhi ya miripuko katika mafunzo yaliyofanyika Ukumbi wa Gereji ya Wizara ya Afya Mombasa Mjini Zanzibar.
Katibu wa Jumuiya ya Maafisa wa Afya Zanzibar Ahmed Suleiman Said akitoa elimu ya kupambana na maradhi ya kipindupindu kwa wananchi wa shehia ya Shaurimoyo Mjini Zanzibar. Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.

Baadhi ya wananchi wa shehia ya Shaurimoyo Mjini Zanzibar wakifuatilia juu ya elimu ya ugonjwa wa Kipindupindu iliyotolewa na Jumuiya ya Maafisa wa Afya Zanzibar.Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.……
…………………………

Mwashungi Tahir – Maelezo Zanzibar.

Daktari dhamana kanda ya Unguja Dkt. Fadhil Mohammed Abdallah amewataka wananchi kuchukua tahadhari kuhusu maradhi ya kipindupindu ambayo kwa sasa ni tishio kubwa Zanzibar.

Hayo ameyasema katika Ukumbi wa Gereji ya Wizara ya Afya Mombasa kwenye mafunzo ya waandishi wa habari juu ya kujikinga na ugonjwa huo ambao bado unaendelea katika sehemu mbali mbali Zanzibar.

Amesisitiza kuchukuliwa tahadhari zaidi kupambana na maradhi ya kipindu pindu ikiwemo kuweka mazingira safi, kufuata masharti ya afya, kuchemsha maji ya kunywa ama kutumia maji yaliyotiwa dawa ya kuulia bektiria wanaosababisha maradhi hayo..

Dkt. Fadhil amewataka wananchi kuacha tabia ya kula ovyo njiani, kukosha matunda na mboga mboga kabla ya kula na kuchukua tahadhari kubwa wakati wa kumshughulikia maiti ya maradhi ya kipindu pindu kwani ni miongoni mwa njia za maambukizi ya maradhi hayo.

Amewataka waandishi wa habari kutekeleza majuku yao ya kutoa elimu kwa wananchi ili wapate uelewa mkubwa zaidi kukabiliana na maradhi hayo.

Amesema maradhi ya kipindu pindu ingawa ni tishio kwa maisha ya wananchi lakini ni rahisi zaidi kuyadhibiti kuliko maradhi mengine iwapo wananchi watafuata masharti ya afya.

“Waandishi wa habari mnao mchango mkubwa wa kutoa elimu kwa jamii katika kukabiliana na maradhi ya kipindupindu hivyo tunategemea mashirikiano makubwa kutoka kwenu,” alisisitiza Dkt. Fadhili

Akifungua mafunzo hayo Mkurugenzi Mtendaji Kamisheni ya Maafa Zanzibar ndugu Ali Juma Hamad amesema juhudi za pamoja zinahitajika katika kukabiliana na kipindupindu na mchango wa kila mtu na taasisi unahitajika.

Amesema kumekuwa na changamoto kubwa katika kukabiliana na maradhi hayo tokea yalipogundulika mwezi Septemba mwaka jana ikiwa ni kipindi cha jua kali, kuchukua muda mrefu na kusambaa sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba kinyume na watu walivyozoea vipindi vya nyuma.

Akiwasilisha mada ya majukumu ya vyombo vya Habari katika kudhibiti miripuko ya maradhi ya kuambukiza, Mkurugenzi wa Idara y Habari Maelezo Zanzibar Rafii Haji Makame amesema vyombo hiyo vinajukumu la lazima katika kusaidia umma kudhibiti vifo na athari nyengine za kiuchumi na kijamii zinazosababishwa na miripuko ya maradhi .

Katika kufanikisha majukumu hayo Mkurugenzi Rafii ametaka kuongezwa ushirikiano kati ya vyombo vya habari na sekta ya afya ili kupata taarifa sahihi kwa wakati katika kufikisha ujumbe kwa umma.

Aidha amesema utoaji wa elimu ya kudhibiti magonjwa ya kuambukiza kupitia vyombo vya habari liwe suala endelevu ili jamii iweze kupata uwelewa na kubadilika kitabia.

Jumla ya kambi 18 zilifunguliwa na kuhudumia wagonjwa 1066 Unguja na Pemba na kati yao wagonjwa 22 walifariki. Hivi sasa kuna kambi nne tu zinazoendelea kupokea wagonjwa katika kisiwa cha Unguja.

Wakati huo huo Katibu wa Jumuiya ya maafisa wa afya Zanzibar Ahmed Suleiman Saidi amewashauri wananchi wa shehia ya Shaurimoyo kubadili tabia na kuweka mazingira wanayoishi katika hali ya usafi ili kujikinga na kipindupindu.

Alitoa ushauri huo alipokuwa akizungumza na wananchi wa shehia hiyo katika skuli ya Shaurimoyo walipowatembelea kutoa taaluma juu yamaradhi hayo kwa vile shehia hiyo ni miongozi kati ya shehia zilizoathirika na kipindupindu.

No comments: