Wednesday, February 17, 2016

MO DEWJI FOUNDATION YAKABIDHI MILIONI 100 KWA WAFUGAJI WA KUKU, KIJIJI CHA MSOGA, CHALINZE


Afisa Mahusiano wa Mo Dewji Foundation, Zainul Mzige (wa pili kulia) akikabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 100 kwa Mwenyekiti wa mradi ufugaji kuku wa kienyeji katika kijiji cha Msoga, Michael Mkindo (wa tatu kushoto). Wanaoshuhudia tukio hilo ni Mbunge wa Jimbo la Chalinze, Mh. Ridhiwani Kikwete (wa pili kushoto), Mkuu wa Wilaya ya ya Bagamoyo, Mh. Majid Mwanga (kushoto) na Diwani wa kata ya Msoga, Hassan Mwinyikondo (kulia).
Afisa Mahusiano wa MO Dewji Foundation, Zainul Mzige akisoma hotuba wakati wa makabidhiano ya mfano wa hundi kwa wafugaji wa kuku wa kienyeji chotara kutoka kijiji cha Msoga, Chalince mkoa wa Pwani. Wa kwanza kushoto ni mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete akifuatiwa na Mkuu wa Wilaya ya Chalinze, Majid Mwanga, wa kwanza kulia ni Diwani wa Kata ya Msoga, Hassan Mwinyikondo.

Mfuko wa MO Dewji umeupatia mradi wa ufugaji wa kuku wa kienyeji chotara wa kijiji cha Msoga mkoani Pwani shilingi milioni 100 kufanikisha uendeshaji wa mradi huo awamu ya kwanza.

Mradi huo unaokisiwa kuwa na makisio ya uzalishaji ya sh 2,777,901,500 ulibuniwa mwaka 2013 kwa lengo la kukabiliana na umaskini kijijini hapo.

Kwa mujibu wa taarifa za mradi makisio ya mapato kutokana na mauzo ya mayai, vifaranga na kuku baada ya kukoma kutaga zinakadiriwa kuwa sh 4,913,708,000

Aidha mradi huu unasimamiwa na kufadhiliwa na rais Mstaafu Dk Jakaya Mrisho Kikwete.

Akikabidhi hundi hiyo ya sh milioni 100, Afisa Mahusiano wa Mo Dewji Foundation, Zainul Mzige alisema kwamba fedha hizo zitaumika kujenga mabanda 200, ununuzi wa vifaranga, ununuzi wa chakula cha kuku, chanjo na dawa na malipo kwa wataalamu.
Afisa Mahusiano wa MO Dewji Foundation, Zainul Mzige akisoma hotuba wakati wa makabidhiano ya mfano wa hundi kwa wafugaji wa kuku wa kienyeji chotara kutoka kijiji cha Msoga.

Mambo mengine ni utawala, mawasiliano, ununuzi wa chachu za mpunga na vifaa vya chakula na maji.

Mzige alisema pamoja na kutoa fedha hizo kuunga mkono juhudi za Msoga Poultry Farming Project (MPFP) kuendesha na kuuendeleza mradi kibiashara, aliwataka wahisaniwa kutambua kwamba maendeleo ya mradi wao yatategemea sana namna wanavyokuwa makini kutumia fursa mbalimbali kujiimarisha.

Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Mo Dewji Foundation imetumia zaidi ya dola za Marekani milioni 3 kwa ajili ya kusaidia miradi mbalimbali ya kijamii nchini.

Aidha hivi karibuni Mfuko wa MO Dewji kwa kushirikiana na kampuni ya Darecha Limited walizindua shindano la Mo Mjasiriamali lenye lengo la kusaidia kukuza ujasirimali miongoni mwa vijana.

Shindano ya Mo Mjasiriamali litatoa fursa ya ukuzaji wa mitaji, ulezi wa wajasiriamali na mitandao ya biashara kuongeza mwanga, ujasiri na kuzalisha wajasiriamali Tanzania.

Ili kufanikisha nia ya kuwa na wajasiriamali wengi, shindano hilo linatarajiwa kuwa daraja kwenda kwa Ofisa Mtendaji, Mohammed Dewji (MeTL Group na mwenyekiti wa Mo DewjiFoundation) ambapo vijana ambao wanaonekana wana kitu cha kufanya, lakini hawana msaada watashiriki kwa lengo la kupata msaada katika mfumo wa mtaji, mtandao na usimamizi wa ukuaji wa shughuli wanayofanya au kutaka kuifanya ili kuianzisha na kuikuza.

Kwa niaba ya wananchi wa Msoga, mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete alimshukuru Mwenyekiti wa Taasisi ya Mo Dewji, Mohammed Dewji kw ufadhili ambao ameufanya kwa wananchi wa kijiji cha Msogo na kumtaka kuwa na moyo wa kutoa zaidi ili azidi kusaidia wananchi walio na mahitaji.
Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete akitoa neno la shukrani kwa MO Dewji Foundation mara baada ya kukabidhiwa mfano wa hundi ya shilingi 100 kwa ajili ya ufugaji wa kuku wa kienyeji Chotara.

Alisema kuwa kupitia mradi huo wa ufugaji wa kuku wa kienyeji chotara, wananchi wa kijiji cha Msoga wataweza kujikwamua na janga la umasikini na wataendelea kuwa wakiandika maombi ya miradi mbalimbali ambayo wanataka kuifanya ili kuzidi kutengeza ajira zaidi kwa wananchi wa Mzoga.

“Tunamshukuru Mohammed Dewji kwa msaada huu tunaimani utasaidia wananchi wa Mzoga na namuomba asisite kutupokea muda mwingine tunapokuwa na miradi mingine,” alisema Kikwete.

Nae Mratibu wa Mradi wa ufugaji wa kuku wa kienyeji chotara (Msoga Poultry Farming Project), Novatus Kailembo alisema wazo la kuanzisha mradi huo lilitolewa na Rais wa awamu ya nne, Dkt. Jakaya Kikwete mwaka 2013 ili kusaidia kuboresha maisha ya wananchi wa Msoga kama kiuchumi, kielimu na kiafya.

Alisema wanataraji kuanza na wanakijiji 300 ukiwa ni mradi wa mfano, awamu ya kwanza ambao wanataraji kuanza kufanyika katika vitongoji tisa ambavyo ni Hospital, Takalagame, Kota, Mnazi Mmoja, Tumbi Juu, Tumbi Chini, Kingugi, Mkundi na Mokela.
Mkuu wa Wilaya ya Chalinze, Majid Mwanga akimshukuru Mwenyekiti wa MO Dewji Foundation, Mohammed Dewji kwa ufadhili ambao ameutoa kwa wilaya yake kwa ajili ya ufugaji wa kuku wa kienyeji chotara ambapo ufugaji huo unataraji kufanyika katika kijiji cha Msoga.

No comments: