Wednesday, February 24, 2016

MH. LUKUVI ATOA MSAADA KWA WAATHIRIKA WA MAFURIKO IDODI, MKOANI IRINGA

Na MatukiodaimaBlog

MBUNGE wa jimbo la Isimani Bw Wiliam Lukuvi amewapa pole waathirika wa mafuriko wa kata ya Mapogolo tarafa ya Idodi wilaya ya Iringa mkoani Iringa kwa kuwakabidhi msaada wa pesa zaidi ya Tsh milioni 9 kwa ajili ya kusaidia mahitaji mbali mbali ikiwa ni pamoja na kurejesha miundo mbinu ya maji safi iliyoharibiwa na mafuriko.

Bw Lukuvi ambae pia ni waziri wa Ardhi ,nyumba na maendeleo ya makazi alikabidhi msaada huo jana baada ya kutembelea waathirika hao waliopo kambi ya Kitanewa pamoja na kutembelea eneo la barabara ya kutoka Iringa kuelekea hifadhi ya Taifa ya Ruaha ambayo kwa sasa imekarabatiwa baada ya awali barabara hiyo kukatika kutokana na mafuriko hayo , alisema kuwa lengo lake kama mbunge wa jimbo hilo la Isimani na serikali ni kuona wananchi waliokumbwa na mafuriko wanaendelea kusaidiwa .
 
Mbunge wa jimbo la Isimani Bw Wiliam Lukuvi ambae ni waziri wa Ardhi ,nyumba na maendeleo ya makazi (kulia) akimpa maelekezo mwenyekiti wa kijiji cha Mapogolo baada ya kumkabidhi fedha kiasi cha Tsh milioni 2 za kulipa fidia ya ardhi kwa wananchi watakaohamishiwa makazi mapya kutoka kitongoji cha Kitanewa Idodi ambao nyumba zao zilisombwa na mafuriko.

Alisema kuwa awali aliomba msaada wa mahindi tani 100 kutoka serikali kwa ajili ya waathirika hao wa mafuriko Idodi na Pawaga ikiwa ni pamoja na kuwasaidia msaada wa fedha kiasi cha zaidi ya Tsh milioni 3 kwa ajili ya kuwawezesha waathirika hao wa mafuriko kupata mahitaji mengine kama mboga na pesa ya kusagia mahindi hayo .

Bw Lukuvi alisema kuwa kwa ajili ya kurejesha huduma ya maji kijijini hapo amewasaidia kiasi cha Tsh miliobni 4 ambazo wameomba kwa ajili ya kuboresha miundo mbinu hiyo ,pia kiasi cha Tsh milioni 2 kwa ajili ya kukiwezesha kijiji kulipa fidia ya ardhi kwa wananchi waliotoa ardhi yao kwa ajili ya wakazi wa kitongoji cha Kitanewa ambao wanapaswa kuhamishwa eneo hilo la mafuriko la kupewa makazi mapya . 
Wananchi wanaotakiwa kuhamishwa kwenda makazi mapya baada ya nyumba zao kusombwa na mafuriko wakimsikiliza kwa makini mbunge wao Lukuvi.

" Waambieni watu wenye mashamba ambayo yatachukuliwa kwa ajili ya viwanja mwaka huu wavune mazao yao na baada ya hapo kila mmoja muweze kumlipa fidia ya Tsh 200,000 na baada ya hapo waitini wataalamu wa ardhi ili waweze kupima viwanja na mpanfgilio mzuri zaidi kwa ajili ya makazi mapya .......pia nataka hata mashamba ya kawaida ya wananchi kupimwa ili kupata hati za ardhi zitakazowawezesha kutumia kupata mikopo ....ila nitawaletea mashine za kufyatulia tofari ambazo unaweza kuzijengea bila kuchoma "

Alisema kuwa kwa ajili ya kuhamasisha ujenzi wa nyumba bora mwananchi atakayekuwa wa kwanza kupandisha jengo atamchangia bati japo kwa sasa amekwisha toa bati zaidi ya 300 kwa mkuu wa wilaya ya Iringa kwa ajili ya waathirika hao.
 
Lukuvi kushoto akiwa na mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela katikati jana.

Bw Lukuvi pia amewapongeza wadau mbali mbali zikiwemo taasisi za dini ,watu binafsi ,taasisi ya kifedha pamoja na mifuko ya hifadhi za jamii kwa kujitolea misaada mbali mbali kwa ajili ya waathirika wa mafuriko na wagonjwa wa Kipindupindu Pawaga .

Pamoja na kuwashukuru wadau hao Lukuvi alimpongeza waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa kuwatembelea waathirika hao wa Mafuriko na wale wa Kipindupindu Pawaga .

Hata hivyo Lukuvi alimpongeza mkuu wa wilaya ya Iringa Bw Richard Kasesela na viongozi wote akiwemo mkuu wa mkoa Amina Masenza kwa kusimamia shughuli mbali mbali ikiwemo ya urejeshaji wa miundo mbinu ya barabara iliyokuwa imekatika katika barabara ya Iringa - Ruaha .

Katika hatua nyingine Bw Lukuvi aliagiza serikali ya kijiji cha Mapogolo kutowabagua wananchi katika kugawa chakula hicho cha msaada na kutaka hata ambao si waathirika wa mafuriko ambao wana njaa wapewe chakula hicho cha msaada kwa waathirika wa mafuriko .

Wakati huo huo Waziri Lukuvi alisema kuwa serikali inakusudia kuijenga barabara ya Iringa- kuelekea hifadhi ya Ruaha kwa kiwango cha lami kama mbavyo Rais Dr John Magufuli alivyoahidi wakati wa kampeni kupitia ilani ya uchaguzi ya CCM

Pia kwa ajili ya kuwafanya wananchi kunufaika watalii wanaotembelea hifadhi hiyo ya Ruaha Iringa alisema tayari jitihada za kujenga viwanja vidogo vya ndege nje ya hifadhi ya Ruaha zimeanza na kuwa lengo la serikali ni kuwahamisha wafanyakazi wanaoishi ndani ya hifadhi hiyo na kujumuika na wananchi nje ya hifadhi ili waweze kupata mahitaji kama wananchi wengine.
 Lukuvi akizungunza na waathirika wa mafuriko ambao kwa sasa wanaishi katika mahema 
 
Mkazi wa Kitanewa akifurahia baada ya Lukuvi kuwapatia misaada mbali mbali.
 
Mmoja kati ya wakazi wa KItanewa ambao walikubwa na mafuriko aliyepata kusoma na waziri Lukuvi darasa moja shule ya msingi akimsikiliza mbunge wake 



 
Lukuvi akitoa maelekezo kwa wananchi wa Kitanewa Idodi.
 
Mkazi wa Kitanewa akilalamika kunyimwa msaada wa mahindi ya msaada wakati yeye ni mlemavu japo si mlengwa wa msaada huo wa waathirika wa mafuriko 
 
Lukuvi akielezwa jambo na mmoja kati ya waathirika wa mafuriko Idodi.
 
Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela akimweleza jambo mbunge Lukuvi 

 
MKazi wa kitanewa Idodi akimpongeza mbunge wake Lukuvi kwa kuwajali wananchi.
 
Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela Katikati na kamati yake ya Ulinzi na usalama wakitazama daraja la Iringa -kuelekea hifadhi ya Ruaha ambalo awali lilikuwa halipitiki baada ya kusombwa na mafuriko na sasa linapitika.






 
Gari la watalii wa ndani likipita kuelekea hifadhi ya Ruaha baada ya daraja kurejeshwa ndani ya siku tano sasa.





No comments: