Monday, January 25, 2016

KATIBU MKUU MAMBO YA NDANI YA NCHI NA NAIBU WAKE WALIPONGEZA JESHI LA POLISI KWA KAZI NZURI NA KULITAKA KUWACHUKULIA HATUA KALI BAADHI YA ASKARI WENYE TABIA YA KUWABAMBIKIZIA KESI WANANCHI.

 Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira (kushoto) akimsalimia Naibu Inspekta Generali wa Polisi, D/IGP Abdulrahman Kaniki wakati Katibu Mkuu huyo akiambatana na Naibu wake, Balozi Simba Yahya (wakwanza kushoto) walipokuwa wanawasili Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya ziara ya kikazi. Katikati ya Katibu Mkuu na D/IGP ni Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu ambaye alikuwa anawatambulisha viongozi wakuu wa jeshi hilo.
 Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu (meza kuu kushoto) akiwaongoza viongozi wakuu wa Jeshi hilo kuimba wimbo wa maadili kabla ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira (meza kuu katikati) pamoja na Naibu wake, Balozi Simba Yahya (kulia meza kuu) kuzungumza na viongozi hao wakati walipofanya ziara ya kikazi ofisi ya Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam.
 Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu (wapili kushoto) akitoa taarifa ya utendaji kazi wa Jeshi lake kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira (katikati meza kuu) wakati Katibu Mkuu huyo ambaye aliambatana na Naibu wake, Balozi Simba Yahya (wapili kulia meza kuu) katika ziara ya kikazi Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam. Hata hivyo, Meja Jenerali Rwegasira aliwataka viongozi hao kuhakikisha wanaliondoa tatizo la kuwabambikizia kesi wananchi linalofanywa na baadhi ya askari wasiokuwa na maadili ndani ya jeshi hilo, kwa kuwa wanalitia doa jeshi hilo ambalo linasifa nzuri nchini na nje ya nchi. Kulia meza kuu ni Naibu Inspekta Generali wa Polisi, D/IGP Abdulrahman Kaniki na kushoto ni Kamishina wa fedha na Lojistiki wa jeshi hilo, Clodwig Mtweve.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira (katikati) akizungumza na Makamanda wa Jeshi la Polisi wakiongozwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu (wapili kushoto) wakati Katibu Mkuu na Naibu wake, Balozi Simba Yahya (wapili kulia) walipofanya ziara ya kikazi Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam leo. Katika hotuba yake, Meja Jenerali Rwegasira aliwataka viongozi hao kuhakikisha wanaliondoa tatizo la kuwabambikizia kesi wananchi linalofanywa na baadhi ya askari wasiokuwa na maadili ndani ya jeshi hilo, kwa kuwa wanalitia doa jeshi hilo ambalo linasifa nzuri nchini na nje ya nchi.
 Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Balozi Simba Yahya (kulia) akizungumza na Makamanda wa Jeshi la Polisi (hawapo pichani) wakiongozwa na Mkuu wa Jeshi hilo, IGP Ernest Mangu (kushoto) wakati Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Rwegasira (katikati) pamoja na Naibu huyo walipofanya ziara ya kikazi katika ofisi ya Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam. Katika hotuba yake, Balozi Simba aliwataka viongozi hao wa jeshi kupambana na wezi wa mitandao ili kuusambaratisha mtandao huo nchini.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira (kulia) akimuaga Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Ernest Mangu pamoja na viongozi wengine wa jeshi hilo mara baada ya Katibu Mkuu huyo ambaye aliambatana na na Naibu wake, Balozi Simba Yahya (katikati) kumaliza ziara ya kikazi iliyofanyika katika ofisi za Makao Makuu ya Jeshi hilo, jijini Dar es Salaam.
Msafara wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira ukiwasili katika lango Kuu la Makao Makuu ya Jeshi la Polisi, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kufanya mazungumzo na Viongozi Wakuu wa Jeshi hilo. 
Picha zote na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Na Felix Mwagara (MOHA).
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Meja Jenerali Projest Rwegasira amewataka viongozi wakuu wa Jeshi la Polisi nchini kuhakikisha wanawachukulia hatua kali askari polisi wenye tabia ya kuwabambikizia kesi wananchi.

Meja Jenerali Rwegasira alisema Jeshi hilo lina sifa nzuri nje ya nchi pamoja na hapa nchini lakini kuna baadhi ya askari wasiowaadilifu wanawaonea wananchi mitaani wasiokuwa na hatia kwa kuwabambikizia kesi ambapo wanalitia doa jeshi hilo.

“Jeshi letu lina sifa nzuri, niliwahi kwenda nchini Kenya nikaambiwa Jeshi la Polisi Tanzania lina maadili kwani hata likimkamata mhalifu linafuata sheria na utaratibu na sio kutumia nguvu kubwa kama yalivyo majeshi mengine,” alisema Rwegazira.

Rwegasira aliongeza kuwa, amefurahishwa sana na utendaji kazi wa jeshi hilo na kutaka kuongeza umakini zaidi ili kuliletea sifa zaidi jsehi hilo na yeye yupo karibu nao katika kuliendeleza jeshi hilo ili liweze kufanya kazi kwa weledi.

Alisema kuwa ni askari wachache mno wenye tabia hiyo ya kuwabambikizia kesi wananchi na kutofuata sheria za jeshi, hivyo kazi ya kupambana na askari hao inawezekana endapo viongozi wa jeshi wakiamua kulifanyia kazi.

“Utendaji kazi wenu ni mzuri, nawapongeza sana hasa mlivyosimamia uchaguzi mkuu vizuri kwani wananchi wengi walikuwa na wasiwasi kuhusu usalama wao katika kipindi cha uchaguzi, lakini mlisimama imara kuhakikisha uchaguzi unamalizika salama,” alisema Rwegasira.

Hata hivyo, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Balozi Simba Yahya naye alitoa pongezi kwa jeshi hilo na kuwataka kuyapeleka mahitaji yao katika ofisi ya Katibu Mkuu pamoja na yeye ili waweze kuyafanyia kazi na hatimaye kuliboresha jeshi hilo.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi hilo nchini, IGP Ernest Mangu aliwapongeza Viongozi hao wa Wizara kwa kuwatembelea katika ofisi za Makao Makuu ya Jeshi kwani wamefariji na kuwahakikishia viongozi hao kuwa wamejipanga vizuri katika kulinda usalama wa raia na mali zao na watayafanyia kazi maagizo waliyopewa.

Katibu Mkuu pamoja na Naibu wake wanamekamilisha ziara yao ya kuzitembelea Idara za Wizara hiyo ambazo ni Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Idara ya Uhamiaji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), ambapo lengo la ziara hizo ni kujitambulisha kwa viongozi hao pamoja na kujifunza kazi mbalimbali zinazofanywa na idara hizo.

No comments: