Friday, December 11, 2015

JIJI LA MBEYA LAPATA MEYA MPYA DAVID MWASILINDI (CHADEMA) DIWANI KATA YA NZOVWE

Meya Mteule wa jiji la Mbeya Diwani wa Kata ya Nzovwe(CHADEMA) Ndugu David Mwasilindi ambaye aliibuka kidedea kwa kupata kura 34 dhidi ya Mpinzani wake wa CCM aliyepata kura 14 katika uchaguzi uliofanyika Desemba 10 katika ukumbi wa Mkapa jijini humo.
Katibu Tawala Wilaya ya Mbeya Ndugu Quip Mbeyela ambaye ndiye aliyekuwa Mwenyekiti katika Kikao cha Baraza la Madiwani ambacho kiliketi kufanya uchaguzi wa kumpata Meya wa jiji hilo pamoja na Naibu Meya katika Halmashauri ya jiji la Mbeya .
Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya jiji la Mbeya Dkt Samuel Lazaro akizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani ambalo liliketi kwa ajili ya kumchagua Meya pamoja na Naibu Meya katika Ukumbi wa Mkapa jijini humo.
Kaimu Mkurugenzi Halmashauri ya Jiji la Mbeya Dkt Samuel Lazaro akiteta jambo na Meya Mteule wa jiji la Mbeya Mh.David Mwasilindi katika kikao cha Baraza la Madiwani Halmashauri ya jiji hilo. 
Wajumbe wa baraza la Madiwani Halmashauri ya jiji la Mbeya wakifuatilia kwa umakini majadiliano katika mkutano huo.

Baadhi ya watumishi wa jiji la Mbeya wakiteta jambo katika mkutano huo wa baraza la Madiwani la Halmashauri ya jiji la Mbeya ambalo liliketi na kumchagua Meya na Naibu wa jiji hilo ambaye ni David Mwasilindi (CDM) baada ya kupata kura 34 dhidi ya mpinzani wake wa CCM aliyepata kura 14.
Diwani akizungumza katika baraza hilo.
Madiwani wakiimba wimbo wa taifa baada ya kukamiliza zoezi la uchaguzi katika baraza hilo la Madiwani halmashauri ya jiji la Mbeya .


Baadhi ya wananchi na wafuasi wa vyama mbalimbali jijini mbeya wakifuatilia kwa umakini uchaguzi wa kumpata Meya wa jiji la Mbeya na Naibu Meya wakiwa nje ya ukumbi wa Mkapa jijini humo.
Tukifuatilia Mkutano.
Na EmanuelMadafa, Mbeya
HATIMAYE Halmashauri ya jiji la Mbeya limepata Meya wake mara baada ya kufanyika kwa uchaguzi wa kugombea nafasi ya Meya na Naibu Meya watakaoongoza halmashauri ya jiji la Mbeya katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Meya huyo mpya wa jiji la mbeya ametokana na Chama cha Chadema Mch David Ponela Mwashilindi kutoka kata ya Nzovwe pamoja na Naibu wake Mch David Nelson Ngogo kutoka kata ya Nsalaga ambao wote wametokana na chama hicho.

Katika uchaguzi huo uliofanyika Desemba 10 kwenye ukumbi wa Mkapa na kusimamiwa na Katibu tawala wa wilaya ya Mbeya Quip Mbeyela,alimtangaza mshindi wa Umeya kuwa ni Mwashilindi aliyepata kura 34 akimshinda mgombea wa nafasi hiyo kutoka CCM,Kefas Mwasote Changani aliyeambulia kura 14.

Kwa upande wa nafasi ya Naibu Mbeya mshindi wa kura nyingi aliyetangazwa ni Mch Ngogo(Chadema) aliyeipata kura 34 dhidi ya mgombea wa CCM katika kinyang’anyiro hicho,Modest Pantaleo Shiyo aliyeambulia kura 14 na hivyo kukifanya chama cha Chadema kuongoza halmashauri ya jiji hilo.

Mara baada ya kutangaza matokeo hayo yaliyowashirikisha madiwani wa Chadema 34 dhidi ya wale wa CCM 14,msimamizi wa uchaguzi huo,Mbeyela alisema kuwa vyama vyote vilivyoshiriki kwenye mchakato huo sasa umekwisha na wanachotakiwa kukifanya madiwani wote ni kuchapa kazi kwa nguvu ili kusukuma kwa kasi maendeleo ya jiji hilo.

Akizugumza mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa nafasi ya Naibu Meya,Ngogo alisema kuwa atahakikisha kuwa anaheshimu haki na uhuru wa kila diwani katika kushauri na kutoa maoni bila kujali itikadi ya vyama vyao kwa kuwa kazi kubwa iliyo mbele yao ni kuwatumikia wananchi wote.

Mstahiki Meya wa jiji hilo kutoka Chadema,Mwashilindi akiwashukuru madiwani wote kwa kura nyingi alizopigiwa,alisema kuwa atahakikisha kuwa anashirikiana na madiwani wote na kuhakikisha kuwa kata zote za jiji hilo zinapiga hatua kubwa na huo ndio mtazamo wake.


Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya jiji hilo,Dk Samwel Lazaro alisema kuwa atahakikisha watendaji wa halmashauri hiyo wanatoa ushirikiano wa kutosha kwa madiwani wote pale wanapohitaji ufafanuzi wa kitaalamu ili kila jambo wanalotaka kulifahamu wapate kwa wakati.

1 comment:

Anonymous said...

Hongera Meya ... Piga kazi sasa