Monday, October 19, 2015

AGRICS YAKABIDHI MBEGU ZA MAHINDI NA ALIZETI KWA WAKULIMA MKOANI SHINYANGA NA SIMIYU

 Wakulima wakifurahia mbegu bora za mahindi, alizeti pamoja na mbolea mara baada ya kukabidhiwa na meneja miradi wa kampuni ya Agrics. Wakulima walionufaika na mbegu hizo ni pamoja na Maswa, Meatu na Shinyanga vijijini.
Afisa Miradi wa kampuni ya Agrics Ltd, Bwana Semeni Kime (wa pili kulia) akifurahi na wakulima wa kijiji cha Mwakabeya baada ya kuwakabidhi wakulima hao mbegu za mahindi, alizeti pamoja na mbolea kwa ajili ya msimu mpya kilimo.
Kampuni ya Agrics imetimiza ahadi ya kuwakabidhi mbegu bora za mahindi, alizeti na mbolea wakulima wa Maswa, Meatu na Shinyanga vijijini. Zoezi hili limefanyika kwa wakati kufuatia msimu mpya wa kilimo kutazamiwa kuanza hivi karibuni. Kampuni ya Agrics iliwapa fursa wakulima kuchagua aina ya mbegu wazitakazo ili kuhakikisha wanapata kile wakipendacho. Wakulima wanaendelea kuandaa mashamba yao huku wakiwa huru kabisa kwani tayari Agrics imewapatia mbegu zao kwa mkopo nafuu kabisa na wametanguliza asilimia 25%.  Zoezi la kukabidhi mbegu lilisindikizwa na viongozi mbalimbali wa vijiji ili kuhakikisha wakulima wanajipatia mbegu zao kwa manufaa ya kijiji na mkoa kwa ujumla.
Akiongea kwa niaba ya Agrics Meneja miradi Bwana Charles Laswai alisema, “Tunajivunia kuwatimizia wateja wetu mahitaji yao kwa wakati. Kwa sasa wakulima wanasubiri mvua wakiwa na amani kabisa kwani tayari wana mbegu zao na wapo tayari kuanza kilmo. Kupitia mkopo wetu wakulima wamejipatia mbegu zao kwa kulipia 25% tu ya mkopo na watalipa asilimia inayobakia baada ya kuwa wamevuna mazao yao. Hii ni fursa kubwa kwa mkulima kwani kwa sasa amepata nafasi nzuri ya kuzingatia kilimo bila kuwaza jinsi ya kupata pesa ya kulipa. Lengo la Agrics ni kuhakikisha kauli mbiu ya ‘Kilimo Kwanza’ inazingatiwa na inakuwa ni yenye tija kwa mkulima wa Shinyanga vijijini, Maswa pamoja na Meatu.  ”
“Kwa upande wetu kukabidhi mbegu kwa mkulima ni mwanzo wa mengi makubwa tutakayomsaidia mkulima katika msimu huu wa kilimo. Mara zote tumekuwa tukiwajali wateja wetu kwa kushirikiana na viongozi wa serikali pamoja na wataalamu wa kilimo kuhakikisha tunawapa mafunzo juu ya kilimo bora na cha kisasa. Elimu hii haiishii tu wakati wa kulima bali hata wakati wa kuvuna na kuhifadhi ili uvunaji na uhifadhi pia uzingatie teknolojia mpya inayompa fursa mkulima kuvuna mazao yake na kuyahifadhi vizuri kwa matumizi ya baadae.  Tunahakikisha mazao yanahifadhiwa kitaalamu ili yasiathiriwe na wadudu kwa kuhakikisha mafunzo yanatolewa kwa wakulima wetu”. Aliongeza Bw. Jonathan Kifunda, Mkurugenzi wa Agrics Tanzania.
Kampuni ya Agrics huwapatia wakulima wake mbegu za mahindi aina ya Seedco Tumbili, Seedco Pundamilia, Pannar na Faru pia huwapatia mbegu za alizeti aina ya Kenyafedha pamoja na mbolea ya kukuzia aina ya CAN (YARA). Mkulima hujipatia mbegu hizi kwa mkopo nafuu na hulipa kwa awamu tano ndani ya miezi 9. Mbegu hizi zimedhibitisha na zinastahimili ukame na wadudu hivyo zinaendana na hali ya hewa ya mikoa ya Simiyu na Shinyanga na kuwawezesha wakulima kupata mazao mengi zaidi.
 “Kampuni ya Agrics imekuwa mkombozi wetu kwa miaka mingi sasa! Tumekua tukikopeshwa mbegu kwa gharama nafuu kabisa na sasa wametukabidhi mbegu kwa ajili ya msimu huu kwa wakati, hivyo tuna amani na tunachosubiri ni mvua zianze kunyesha ili tupande mbegu zetu. Kupitia Agrics kijiji chetu kina mabadiliko makubwa sana kwani wakulima wengi wameweza kujenga nyumba za kisasa (kwa vigezo vya nyumba za vijijini) na tuna akiba ya chakula tofauti na zamani kwani mavuno yalikuwa ni kidogo sana. Binafsi nimeweza kuwasomesha watoto watatu sekondari na mmoja amejiunga na chuo kikuu. Na nimefanikiwa yote haya kupitia kilimo, suala ambalo lilikuwa ni ndoto kwetu maana tulitegemea mifugo tu ili tuweze kuwasomesha watoto wetu.” Alieleza bwana Emmanuel Titus mkazi wa kijiji cha Ipililo wilayani Maswa.
Agrics Ltd ni kampuni ya kibiashara inayofanya kazi zake kwa kushirikiana na shirika la ICS. Agrics inawapa wakulima wadogo wa kanda ya ziwa nchini Tanzania na Kenya fursa ya kujipatia mbegu bora na za kisasa kwa mkopo nafuu unaolipwa kwa awamu zinazompa mkulima nafasi nzuri ya kujiendeleza. Pia Agrics inahakikisha akiba ya chakula kwa mkulima ni lazima kwa ajili ya kupunguza njaa kwa wakulima.
Kwa mhariri,
Kwa maelezo Zaidi wasiliana na Salima Salum, Afisa mawasiliano na masoko, Agrics Tanzania                                                                                                                                    kupitia  0716120482 or salima.salum@agrics.org    

No comments: