Wednesday, September 9, 2015

WANANCHI WA KATA YA BARAY KARATU WAKAABIDHIWA MIRADI MINNE

Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Mkoani Arusha Omary Kwaang’ (katikati mwenye kaunda suti) akiwa na baadhi ya watumishi wa wilaya hiyo, akikagua lambo la maji eneo la Endesh, linalotumiwa na mifugo na binadamu, lililogharimu sh169 milioni kwa ufadhili wa shirika la World Vision. 
 Mkuu wa Wilaya ya Karatu, Mkoani Arusha Omary Kwaang’ (kushoto) akiwa na baadhi ya watumishi wa wilaya hiyo, akikagua lambo la maji eneo la Endesh, linalotumiwa na mifugo na binadamu, lililogharimu sh169 milioni kwa ufadhili wa shirika la World Vision.
 
WANANCHI 12,082 wa Kata ya Baray Wilayani Karatu Mkoani Arusha wamekabidhiwa miradi nane ya elimu na afya ambayo imegharimu sh447.8 milioni kwa ufadhili wa shirika lisilo la kiserikali la World Vision Korea.
 
Mratibu wa mradi wa World vision Karatu John Massenza akikabidhi jana miradi hiyo kwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo John Mabula alisema  itawanufaika wakazi wa vijiji vitatu vya Dumbachang, Mbuga Nyekundu na Jobaj.
 
Massenza alitaja miradi hiyo kuwa ni madarasa matatu, ofisi ya walimu na choo cha wanafunzi ya shule ya msingi Mbuyuni iliyogharimu sh83 milioni na madawati 200 kwa ajili ya wanafunzi wa shule hiyo iliyogharimu sh13 milioni.
 
Alitaja mingine ni samani na vifaa zahanati ya Endesh sh11 milioni, madawati 100 ya shule ya msingi Mohedagew Gidamilanda sh13 milioni na vifaa vya vikundi 11 vya hisa vijiji vya Dumbecha, Jobaj na Mbuga Nyekundu sh5 milioni.
 
“Mingine ni lambo kwa matumizi ya binadamu na wanyama sh169 milioni, zahanati na choo Endesh sh83 milioni, vitabu na vifaa vya ufundishaji 1,570 vya sh11 milioni na madarasa mawili sh53.9 Endesh,” alisema Massenza.  
 
Alisema katika wilaya hiyo, World vision ilianza kufanya shughuli zake mwaka 2009 kwenye tarafa za Endabash na Lake Eyasi ambapo imekuwa ikitekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye sekta tofauti.
 
“Miradi hiyo iliyotekelezwa ni ya upande wa sekta ya elimu, afya, kilimo, maji na ufadhili wa watoto kwa kushirikiana na halmashauri ya wilaya ya Karatu na wana jamii wa eneo hili,” alisema Massenza.
 
Kwa upande wake, mkuu wa wilaya ya Karatu Omary Kwaang’ alipongeza shirika la World vision kwa kufanikisha ujenzi wa miradi hiyo ya thamani ya sh447.8 milioni ambayo itanufaisha jamii ya wafugaji na wakulima.
 
Kwaang’ aliwataka wananchi wa kata hiyo kuhakikisha kuwa wanaitunza miradi hiyo ili iwe endelevu na kudumu kwa faida ya kizazi kilichopo na kijacho, kwani shirika la World vision limetumia gharama kubwa kufanikisha miradi hiyo.
 
Alisema kwenye suala la zahanati wilaya ya Karatu imepiga hatua kwenye kutekeleza sera ya wizara ya afya inayotaka kila kijiji kiwe na zahanati kwani wamejenga zahanati kwenye vijiji 45kati vijiji 58 hivyo vimebaki vijiji 13.
 
“Nawapongeza viongozi na wananchi wa wilaya ya Karatu kwa kupiga hatua kwenye ujenzi wa zahanati, ila tujitahidi kwenye elimu kwani vyumba vya madarasa vinahitajika 1,109 na vilivyopo ni 875,” alisema Kwaang’.
 
Alisema kwenye ujenzi wa nyumba za walimu kuna hitajika 694 na zilizopo ni 578 na matundu ya choo yanahitajika 1,221 na pungufu ni matundu 975 hivyo wajitahidi kumalizia mapungufu yote wakishirikiana na serikali ya wilaya hiyo.

No comments: