Tuesday, September 8, 2015

MKAKATI KABAMBE KUIMARISHA MAZINGIRA YA BIASHARA, UTALII MBIONI-TNBC

 Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam
Hatua thabiti za utekelezaji wa maazimio ya mkutano wa Nane wa Baraza la Biashara la Taifa (TNBC) zinatarajiwa kujulikana wiki chache zijazo.

Maazimio hayo yanalenga hasa kuimarisha mazingira ya biashara nchini na sekta ya utalii.

Akiongea na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa TNBC, Bw. Raymond Mbilinyi (Pichani) alisema hatua za utekelezaji maazimio mbalimbali ya kuimarisha sekta hizo zitajulikana katika mkutano wa 9 wa baraza hilo unaotarajiwa kufanyika tarehe 2 mwezi ujao (Oktoba).

“Mapendekezo mengine ni ya kiutawala zaidi ambayo ni rahisi lakini kuna maswala mengine yatahitaji mabadiliko ya sheria mbalimbali na haya yatatakiwa kufuata taratibu zinazotakiwa,” alisema Bw. Mbilinyi na kumshukuru Rais Kikwete kwa kuendesha mkutano huo.

Akielezea baadhi ya maeneo yanayohitaji kuboreshwa alisema kuwa pamoja na kuwa na kitengo maalum cha kuhakikisha watanzania wanashiriki kikamilifu katika ujenzi wa uchumi.

“Hii ina maana kuwa watanzania wasibaki kuwa watazamaji tu bali wawe washiriki katika shughuli za uchumi,” alifafanua.

Alisema eneo lingine linaloshughulikiwa ni kuwa na eneo au kituo kimoja ambacho kitarahisisha wafanyabiashara kulipia leseni za biashara na kuwa tayari kuna kikosi kazi kinachoangalia swala hilo litatekelezwaje.

“Kikosi kazi hiki kitaangalia jinsi bora ya kutekeleza hili na ikiwezekana kutumia njia ya mtandao ili kufanya mambo kwa kisasa zaidi,” alifafanua.

Mapendekezo mengine yanayofanyiwa kazi ni pamoja na kuvutia utaalamu kutoka nje ambao hauko hapa nchini ili kuwezesha vyuo vikuu hapa nchini kutoa wahitimu wenye sifa zinazotakiwa na soko la ajira.

Kwa mujibu wa Bw. Mbilinyi, wadau wa mkutano huo pia walishauri kutumia vyema swala la soko la nyumba linalokua kwa kasi hapa nchini kwa kuangalia uwezekano wa kuruhusu wawekezaji toka nje kumiliki nyumba.

Mkutano huo pia wa tarehe 2 Oktoba utaangalia jinsi bora ya kutumia ardhi kwa maendeleo ya wengi.  

“Tanzania tuna ardhi kubwa lakini haijapimwa…hili litafanyiwa kazi,” alisema na kuongeza kuwa mpango wa MKURABITA ni muhimu ukapewa kipaumbele.

Kwa upande wa sekta ya utalii, alisema washiriki wa mkutano walipendekeza kutumiwa kwa utaratibu wa ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi katika kuendeleza sekta hiyo kwa mfano katika ujenzi miundombinu kama viwanja vya ndege.

“Wadau pia wanataka sekta hii iunganishwe kwenye mpango wa Matokeo Makubwa Sasa ili kuipa msukumo mkubwa zaidi kimaendeleo…hili pia litazingatiwa na kufikishwa katika mkutano ujao,” alisema.

Mapendekezo hayo yatafanyiwa kazi na wataalamu wa sekta ya umma na binafsi.

No comments: