Friday, May 16, 2014

MAKALA ATOA MAJIBU YA MATATIZO YA MAJI MAJIMBO YA MSALALA NA MBOGWE

Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akipokea maelezo ya kisima Wilayani Mbogwe. Tayari Wizara ya Maji imeshatoa shilingi milioni 200 kwa ajili ya upanuzi wa miundombinu ya maji wilayani hapo kutimiza ahadi ya Waziri wa Maji Prof. Maghembe.
Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akimuandikia jambo Mbunge wa Mbogwe Mh. Augustino Masele. Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Geita Magalula Said Magalula.
Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akiwaonesha jambo, Mbunge wa Mbogwe, Mkuu wa Mkoa wa Geita, RAS wa Geita kabla ya hutuba yake.
Mbunge wa Mbogwe, Mh. Augostino Masele akiwahutubia wananchi wa Mbogwe namna ambavyo yeye kwakushirikiana na Mbunge wa Msalala Mh. Maige walivyoweza kumleta Naibu Waziri wa Maji ili kutatatua na kuzitafutia suluhisho la kudumu kero za maji katika majimbo yao.
Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akiwahutubia wananchi wa wilaya ya Mbogwe baada ya kukagua miradi ya maji katika Wilaya ya Mbogwe Mkoani Geita.
Mbunge wa Msalala Mh. Ezekiel Maige akimuonesha jambo Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla kabla ya kuanza kwa mkutano wa hadhara katika mji mdogo wa Isaka.
Mbunge wa Msalala Mh. Ezekiel Maige akiwahutubia wananchi wa Isaka Wilayani Kahama juu ya utatuzi wa kero ya maji katika eneo hilo. Kulia ni Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akichukua dondoo za hotuba hiyo ili aipatie majibu.
Naibu Waziri wa Maji Mh. Amos Makalla akiwahutubia wananchi wa Isaka, aliyekaa chini ni mbunge wa Msalala, Mh. Ezekiel Maige.

Na Athumani Shariff
Naibu Waziri wa Maji, Mh. Amosi Makalla aliongozana na Wabunge wa Msalala na Mbogwe walilazimika kuacha vikao vya bunge la bajeti vinavyoendelea Bungeni mjini Dodoma ilikwenda kukabiliana na matatizo ya maji katika majimbo ya Msalala na Mbogwe.

Makala alichukua uamuzi huo baada ya kupewa mualiko na Ezekiel Maige Mbunge wa Msalala pamoja na Augostino Masele Mbunge wa Mbogwe pindi walipokuwa katika bunge maalumu la katiba.

Akiwa Wilayani Mbogwe, Mh. Naibu Waziri alipokea taarifa za hali ya wilaya pamoja na kero za maji katika wilaya hiyo na kisha kutembelea miradi ya maji kujionea hali halisi ya maji ilivyo pamoja na kero za maji katika maeneo hayo.

Akitaka kujua kuhusu ahadi ya Mh. Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe aliyoitoa juu ya kuchangia shilingi milioni 200 ikiwa ni ahadi aliyoitoa mbele ya Rais. Masele alimtaka Makala awaeleze wananchi wa Mbogwe hatma ya ahadi ya Waziri wa Maji mbele ya Rais Kikwete kwa wananchi wa Mbogwe.

“Mh. Naibu Waziri wa maji, katika ziara ya Rais aliyoambatana na Waziri wa Maji Prof. Maghembe, Waziri wa Maji aliahidi kutuchangia shilingi milioni 200 ili kutanua mtandao wa maji katika wilaya ya Mbogwe, je wananchi wa Mbogwe wanauliza juu ya utekelezaji wa ahadi hii ya Mh. Waziri.” Aliuliza Masele alipokuwa anahutubia wananchi.

Akijibu swali hilo katika mkutano wa hadhara, Mh. Makala alisema, tayari pesa hizo Waziri ameshazitoa tangu tarehe 6 Mei, na ni mategemeo yangu kuwa zitatumika kwa ufasaha na kwa malengo yaliyokusudiwa. “Mh. Waziri ameshazitoa pesa hizo na zipo kwenye akaunti ya mhandisi wa maji, ni nimatarajio yangu kuwa zitatumika kwa malengo yaliyokusudiwa” alijibu Makala.

Katika hatua nyingine Masele alimuomba Naibu Waziri, Wilaya ya Mbogwe ipatiwe maji kupitia mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Viktoria kwani chanzo chake ni chakudumu.

Akiwa Wilayani Kahama katika jimbo la Msalala kata ya Isaka, Naibu Waziri alikumbana na kero kubwa ya maji baada ya kujionea upungufu wa maji kwa zaidi ya asilimia 79. 

Mbunge wa Msalala Ezekiel Maige alimueleza Naibu Waziri kuwa shida ya maji Isaka ni kubwa na vyanzo vya maji vilivyopo havitoshelezi hata robo ya mahitaji ya wananchi.

Akijibu hoja hizo katika mkutano wa hadhara, Mh. Makalla alisema Isaka ipo katika kipaumbele cha hali ya juu kwani ahadi ya kuleta maji katika eneo hili ni ya Rais. Pia aliongeza kuwa Mradi wa kuleta maji Isaka kupitia maji ya Ziwa Viktoria utaanza mwakani. 


 “Mradi mkubwa wa maji Isaka kutoka ziwa Viktoria utaanza mwaka ujao wa fedha, ahadi ya kuleta maji hapa ni Rais, hivyo hatuwezi kuacha kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais” alisema Makalla. 

No comments: