Wednesday, March 5, 2014

USAHIHISHAJI WA MITIHANI SHULE ZA MSINGI KWA KUTUMIA KOMPYUTA WAPATA MAFANIKIO JIJINI DAR

Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es salaam Bi. Theresia Mmbado akifunga mafunzo ya siku 3 ya matumizi ya Fomu za OMR kwa walimu wakuu 254 wa shule za Msingi za mkoa wa Dar es salaam yaliyofanyika katika shule ya Sekondari Shaaban Robert.
Afisa Elimu wa mkoa wa Dar es salaam Bw. Raymond Mapunda akitoa ufafanuzi kwa walimu wakuu wa shule za Msingi za mkoa wa Dar es Salaam kuhusu namna mkoa ulivyojipanga kutatua changamoto za elimu. 
Baadhi ya Walimu wakuu wa shule za Msingi jijini Dar es salaam wakifuatilia michango mbalimbali iliyokuwa ikiwasilishwa kuhusu maboresho ya matumizi ya mfumo wa OMR.

Na. Aron Msigwa – MAELEZO.

Matumizi   ya mfumo mpya wa  kufanya  mitihani kwa kutumia karatasi maalum  za OMR (Optical Mark Reader) na usahihishaji wa mitihani hiyo kwa njia ya kompyuta umeonyesha mafanikio  jjini Dar es salaam mara baada ya vitendo vya udanganyifu na wizi wa mitihani ya shule ya msingi kudhibitiwa.

 Katibu Tawala wa Mkoa wa Dar es salaam Bi. Theresia Mmbado ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es salaam wakati akifunga mafunzo ya siku 3 ya matumizi ya Fomu za OMR  kwa walimu wakuu 254 wa shule za Msingi za mkoa wa Dar es salaam.

Amesema matumizi ya karatasi maalum za OMR yamefanikiwa kudhibiti vitendo vya udanganifu  na kurahisisha utoaji wa matokeo na kuipunguzia serikali gharama ya  kusahihisha mitihani hiyo ambayo hapo awali ilikua ikichukua muda mrefu na kuchelewesha matokeo ya wanafunzi.

“ Nikiwa mwenyekiti wa usimamizi wa mitihani wa mkoa wa Dar es salaam kwa mwaka 2013 nakiri kuwa mkoa wetu umepata fomu mafanikio makubwa katika usimamizi wa mitihani na kupunguza udanganyifu kwa sababu ya hizi” amesema.
Amesema kuwa zipo changamoto ambazo mkoa unaendelea kuzifanyia kazi ili kurahisisha matumizi ya mfumo huo kwa walimu na wanafunzi kuwa ni pamoja na uchakavu wa meza za kufanyia mitihani ambazo huchangia karatasi za OMR kujikunja na wakati mwingine kuchakaa na kupoteza sifa ya kusahihishwa na kompyuta.
Pia ameeleza kuwa ipo changamoto ya baadhi ya shule binafsi ambazo walimu wakuu wake wamekwishapatiwa mafunzo hayo lakini  wamekuwa wakihama kutoka eneo moja hadi jingine hivyo kuathiri mafunzo kwa wanafunzi na waalimu  kuhusu namna ya kuweka vivuli kwenye karatasi hizo.

“ Natoa rai kwa baadhi ya wamiliki na walimu wakuu hasa wa shule binafsi wasiotoa ushirikiano na kushindwa kuleta walimu wao katika mafunzo kama haya tutaanza kuwafuatilia, ikibidi watumie gharama zao wenyewe kuhakikisha walimu wao wanapata mafunzo haya muhimu kwa mustakabali wa taifa letu na maisha wanafunzi wetu” amesisitiza.

Amewataka wakuu hao waliopata mafunzo hayo kuwa mabalozi kwa wengine ambao hawakupata mafunzo hayo kwa kuonyesha utofauti ili gharama iliyotumika wakati wa mafunzo hayo iweze kuzaa matunda na kuleta faida kwa wananchi.

Amesema  Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA) limekwishatoa kiasi cha shilingi milioni 138 kwa ajili ya mafunzo ya walimu wa kuendelea kusimamia zoezi la matumizi ya fomu za OMR katika uendeshaji wa mitihani ya kumaliza elimu ya msingi na kuongeza kuwa takribani walimu 7,105 wameshapatiwa mafunzo kwa ngazi ya kata.

Kwa upande wake Afisa Elimu wa mkoa wa Dar es salaam Bw. Raymond Mapunda ameeleza kuwa mkoa wa Dar es salaam licha ya kukabiliwa na changamoto mbalimbali umekuwa ukifanya vizuri katika matokeo ya shule za msingi kitaifa.

“Mkoa wa Dar es salaam ni miongoni mwa mikoa inayopokea wanafunzi wengi kila mwaka mathalani mwaka 2013 tumesajili wanafunzi 63,000 na mwaka huu 2014 tunatarajia kupokea wanafunzi 68,000 kiwango ambacho kinazidi kupanda kilinganishwa na miundombinu iliyopo”

Kuhusu matumizi ya fomu za OMR, Bw. Mapunda ameeleza kuwa ameeleza kuwa zimepunguza makosa ya kibinadamu na gharama za usahihishaji na kuongeza kuwa baadhi ya changamoto za baadhi ya karatasi kujikunja, kuchafuka na kutoboka na pia baadhi ya wanafunzi kushindwa kuweka vivuli kwenye vyumba husika vya majibu waliyochagua zinaendelea kufanyiwa kazi katika maeneo husika.

Kuhusu umuhimu wa mafunzo hayo amesema kuwa yamewajengea uelewa walimu hao juu ya namna ya kukabiliana na changamoto zinazojitokeza na pia kubadilishana uzoefu ikiwa ni sehemu ya kutekeleza Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).

Aidha katika hatua nyingine Bw. Mapunda amesema mkoa wa Dar es salaam unaandaa maonyesho maalum ya wiki ya Taaluma ambayo itazihusisha shule za Binafsi na zile za sekondari ambapo washindi katika wiki hiyo watapewa zawadi mbalimbali.

Naye mwenyekiti wa waliu wa shule za Msingi mkoa wa Dar es salaam Mwalimu Rehema Ramole akizungumza kwa niaba ya washiriki wenzake amesema kuwa tayari wamejipanga kuhakikisha kuwa wanaondoa makosa yote  yatokanayo na mfumo wa matumizi ya karatasi za OMR katika mkoa wa Dar es salaam.

No comments: