Wednesday, October 30, 2013

MAREKANI YATETEA MSIMAMO WAKE WA KUIWEKEA CUBA VIKWAZO VYA KIUCHUMI

Muwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi akizungumza wakati wa upigaji kura wa Azimio nambari A/68/L4 linaloitaka Marekani kuiondolea Cuba Vikwazo vya Kiuchumi, Kibiashara na Kifedha. Pembeni ni Naibu Muwakilishi wa Kudumu, Balozi Ramadhan Mwinyi. Nchi 188 kati ya nchi 194 ambazo ni Mwanachama wa Umoja wa Mataifa zilipiga kura ya ndiyo kuunga mkono azimio hilo katika mkutano uliofanyika siku ya Jumanne hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa zikiwamo nchi zote za Jumuiya ya Ulaya ilihali Marekani na Israel zilipiga kura ya hapana huku nchi tatu ambazo ni Marshall Island, Micronesia na Palau zilipiga kura ya kutofungamana na upande wowote.

Na Mwandishi Maalum

Licha ya  Jumuiya ya Kimataifa  kwa  mara nyigine tena kupiga kura ya ndiyo  kuunga mkono Azimio namba A/68/L4  linalosisitiza  umuhimu wa Marekani  kuiondolea Cuba vikwazo vya kiuchumi, kibiashara na kifedha. Marekani kwa upande wake imetetea  msimamo wake  huo kwa kusema   inafanya hivyo kutetea maslahi ya wananchi wa  Cuba.

Akizungumza  kabla ya azimio hilo kupigiwa kura  muwakilishi wa Marekani, Bw Ronald Godard alisema kwamba wakulaumiwa ni  serikali ya Cuba   na si Marekani kwa kile alichoeleza kwamba   watu wa nchi yake  wanaurafiki  mkubwa na  watu wa Cuba  na ndiyo maana  Marekani  imekuwa ikitetea  maslahi   ya wananchi wa  Cuba  ya kujiamlia mambo yao na hatima yao.

Akaongeza kwamba   ukiukwaji wa haki za binadamu,  mbinyo wa uhuru wa  habari na uhuru wa kujieleza pamoja na mifumo na sera mbaya za kiuchumi na uwezekaji ndiyo vinavyorudisha nyuma maendeleo ya Cuba na watu wake na kwamba bila masuala hayo na mengine kurekebishwa  itakuwa ndoto kwa wananchi wa  Cuba kijiletea maendeleo yao. Na akawataka wajumbe wa  Baraza Kuu  la Umoja wa  Mataifa kutounga  mkono  azimio hilo.

Pamoja na rai hiyo ya Marekani ya kutaka  jumuiya ya kimataifa isiunge mkono azimio hilo,  nchi wanachama 188 walipiga kura ya ndiyo, huku Marekani yenyewe na Israeli  zikipiga kura ya hapana wakati Marshall Island,  Federated States of  Micronesia na Palau zikipiga kura ya kutofungamana na upande wowote.

Katika  upigaji kura hiyo,  nchi zote wanachama wa Jumuiya ya Ulaya  ( EU) nazo zilipiga kura ya ndiyo kuunga mkono Azimio hilo licha ya kwamba zilikuwa hazikubaliana na baadhi ya mambo  yakiwamo ukiukwaji wa haki za binadamu katika taifa hilo la Cuba.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  ni kati ya  mataifa yaliyopiga kura ya ndiyo  kuunga  mkono azimio hilo ambalo kama ilivyokuwa kwa miaka iliyopita liliwasilishwa  mbele ya  Baraza na  Waziri wa Mambo ya Nje wa Cuba  Bw. Bruno Rodriquez Parrila.

Akiwasilisha  Azimio hilo,  Waziri Parrila alianisha athari za kiuchumi, kifedha,  kimawasiliano na kudumazwa kwa ustawi na maendeleo ya nchi ya Cuba na watu wake, adhari ambazo zimetoka na  miaka mingi ya vikwazo vilivyowekwa na  Marekani.

Akiungana na wazungumzaji wengi waliotoa wito wa kutaka kuondolewa kwa vikwazo hivyo,  Muwakilishi wa Kudumu wa  Tanzania katika Umoja wa  Mataifa Balozi  Tuvako Manongi alitoa rai kwa mataifa hayo mawili kukaa mezani na kumaliza  tofauti zao.

 Akasema  licha ya  vikwanzo hivyo kudumu wa miaka 50 ukweli wa  mambo ni kwamba athari zake zimekuwa zaidi kwa  wananchi wa sio kuwa na hatia. Akasema Tanzania kama  rafiki wa mataifa hayo mawili ilikuwa ikitoa rai kwa pande hizo mbili kukaa meza moja na  kumaliza tofauti zao kwa manufaa ya wananchi wa pande hizo mbili.

Wazungumzaji wengi, walieleza kwamba kuendelea  kwa vikwazo vya kiuchumi nchini Cuba ni  ukiukwaji wa sheria za kimataifa  pamoja na kanuni za msingi ambazo zimeainishwa katika katiba ya Umoja  wa Mataifa.

 Baadhi ya wasemaji walieleza kwamba vikwazo ambavyo  Marekani  imeiwekea Cuba havikuwa na maana yoyote zaidi ya kuendeleza tofauti zilizojiri wakati wa  vita baridi na kwamba Cuba kama taifa huru lilikuwa na haki ya kujiamulia mambo yake yenyewe.

Aidha wasemaji kadhaa waliitaka  Marekani  ifikie mahali sasa isikilize wito wa mataifa mengi, wito wa kuitaka  kuondoa vikwazo hivyo  kwa  manufaa na ustawi wa wananchi wengi wa cuba.

 Wazungumzaji wengine walibainisha kwamba  haikuwa haki kwa  Marekani kuwachukulia hatua nchi au makampuni ya kimataifa ambayo  yanataka  au yamethubutu kushirikiana kiuchumi na  Cuba na  kusisitiza kwamba Marekani inatakiwa kuachana na utaratibu huo.

No comments: