Sunday, August 4, 2013

UZINDUZI WA CHAMA CHA WAZAZI WA WATOTO WENYE ULEMAVU WA MTINDIO WA UBONGO, AKILI NA VIUNGO TANZANIA.

CHAMA CHA WAZAZI WA WATOTO WENYE ULEMAVU WA MTINDIO WA UBONGO, AKILI NA VIUNGO TANZANIA. (CHAWAUMAVITA)
                                   
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

UZINDUZI WA CHAMA CHA WAZAZI WA WATOTO WENYE ULEMAVU WA MTINDIO WA UBONGO, AKILI NA VIUNGO TANZANIA. (CHAWAUMAVITA) UTAKAOFANYIKA SIKU YA JUMAMOSI AGOSTI 24’ 2013 KATIKA UKUMBI WA SABASABA AMBAPO MGENI RASMI ANATARAJIWA KUWA RAIS WA JAMUHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE.

1.0 UTANGULIZI
Kwa kuwa vitendo vya ukiukwaji wa haki za Binadamu kwa watoto wenye ulemavu wa Mtindio wa ubongo, akili na viungo vimekuwa vikishamiri nchini;
Na kwa kuwa baadhi ya wazazi wamekuwa wakifarakana, kukimbiana, na hata kumtelekeza mtoto na pia wakati mwingine kumdhuru mtoto mwenye ulemavu baada ya mtoto huyo kuzaliwa au kupatwa na ulemavu baadaye;
Na kwa kuwa kumekuwa na dhana potofu iliyotawala katika jamii juu ya upatikanaji wa watoto wenye ulemavu wa mtindio wa ubongo, akili na viungo na maisha yao kwa ujumla;
Na kwa kuwa hakuna huduma za awali kabla na baada ya tatizo zilizo endelevu zitolewazo kwa watoto wenye mtindio wa ubongo, akili na Viungo kwa watoto/watu wanoishi na ulemavu huo;
Na kwa kuwa mipango na mikakati  iliyopo nchini haikidhi changamoto zinazoendelea kujitokeza   kwa watoto/watu wenye ulemavu wa mtindio wa ubongo, akili na  viungo nchini;
Na kwa kuwa  mtoto mwenye ulemavu ni sawa na mtoto mwingine yeyote anastahili kupata huduma na vifaa tiba maalum vya matibabu, na nafasi sawa ya elimu na mazoezi ili kumsaidia kufikia malengo yake ya kimaisha;
Na kwa kuwa sisi wazazi na wananchi kwa ujumla tuna jukumu la awali la kuhakikisha  kuwa watoto/watu  wenye ulemavu wa mtindio wa Ubongo na Viungo wanakuwa salama na duniani panakuwa ni mahala bora pa kuishi kwao;

HIVYO BASI Sisi  Wazazi wa Watoto wenye Ulemavu wa Mtindio wa Ubongo na Viungo tunaopata huduma katika Hospitali na vituo vya  CCBRT tuliamua, kuunda chama kiitwacho  CHAMA CHA WAZAZI WA WATOTO WENYE ULEMAVU WA MTINDIO WA UBONGO, AKILI NA VIUNGO TANZANIA. (CHAWAUMAVITA)
Dira ya CHAWAUMAVITA ni kuwa CHAMA cha mfano kinachochangia upatikanaji wa  huduma bora na endelevu kwa watoto wenye Ulemavu wa Mtindio wa Ubongo, Akili na Viungo Tanzania ili kuhakikisha watoto wenye Ulemavu huo wanasaidiwa kukabiliana na changamoto zilizopo na kuandaa mazingira bora ya makuzi na maisha yao kwa ujumla.
Chama kimesajiliwa na Wizara ya Mambo ya ndani tangu April 2013 kwa usajili wenye namba S.A 18732.

MALENGO YA CHAWAUMAVITA NI:-
Kuwaleta pamoja watu/familia zinazolea  watoto wenye ulemavu wa mtindio wa Ubongo, akili na viungo ili kubadilishana uzoefu, kupata elimu ya namna ya kuwatunza watoto wenye ulemavu huo.
Kutoa elimu ya ulemavu wa Mtindio wa Ubongo na Viungo  kwa jamii ili Kupunguza athari na maumivu yatokanayo na Mtindio wa Ubongo, akili na viungo.
Kukusanya, kuchapisha na kusambaza taarifa zinazohusu matatizo yatokanayo na ulemavu wa Mtindio wa Ubongo,akili na viungo.
Kuwasaidia wanachama/wazazi katika kuwatunza na  kutetea na kupata haki zao kwa mujibu wa sheria.
Kujenga na kuendeleza vituo vya mazoezi tiba, kuratibu na kusambaza vifaa tiba kwenya vituo na;
Kujenga na kuimarisha vituo kwa ajili ya masuala ya kijamii na michezo kwa  watoto wenye ulemavu



UZINDUZI
Baada ya Usajili, CHAWAUMAVITA iliandaa Mpango Mkakati wa Miaka mitano 2013-2018 ambao una  lengo la kuwasaidia watoto wenye Ulemavu wa Mtindio wa Ubongo akili na Viungo pamoja na kutoa elimu kwa jamii ili kwanza jamii ishiriki katika kuzuia upatikanaji wa watoto hawa na pia iwalee na kuwasaidia kupata mahitaji yao muhimu ya kila siku pamoja na kufikia malengo yao ya kimaisha
Ni kwa muktadha huu Ndio maana tumeamua kufanya Uzinduzi wa Chama cha CHAWAUMAVITA na kumualika Rais Jakaya Mrisho Kikwete ili:-
Ø Kuishirikisha jamii na wadau wengine kushiriki katika harakati kupigania ustawi wa watoto wenye ulemavu kwa maslahi ya watoto wote wa Tanzania wenye Ulemavu wa Mtindio wa Ubongo, Akili na Viungo. 
Ø Kuzindua Mpango Mkakati wa chama wa miaka mitano 2013-2018.
Ø Kuonyesha Makala Filamu (Documentary) inayoonyesha hali halisi ya maisha ya jamii inayowalea watoto wenye ulemavu wa Mtindio wa Ubongo Akili na Viungo pamoja na walezi wao.
Ø Kuzindua tovuti ya Chama na kualika juhudi za wadau katika kuchangia harakati za kufikia malengo ya Chama na jamii kwa ujumla.
Uzinduzi utafanyika siku ya jumamosi ya tarehe 24.08.2013, saa 4:00 Asubuhi hadi saa 8:00 Mchana. Na Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa  Dr Jakaya Mrisho Kikwete.

Chawaumavita inachukua fursa hii kuwaalika wadau wote muhimu wakiwemo waandishi wa habari, Serikali, Mabalozi, Asasi na taasisi mbalimbali kushiriki katika tukio hili muhimu kwa maslahi ya watoto wenye ulemavu wa Mtindio wa Ubongo, Akili na viungo Tanzania.

Imtolewa na
Jonathan Kawamala
MWENYEKITI CHAWAUMAVITA

MAFANIKIO
Kwa takribani kipindi cha mwaka mmoja tangu kuanzishwa na kusajiliwa kwa chama, tumeweza kufanya yafuatayo;
·       Kujenga mawasiliano mazuri na taasisi za serikali ,binafsi na za kiraia.
·       Mwaka jana kupitia wizara ya afya,tuliweza kupata mfadhili katika kampuni ya Montero kwa kushirikiana na mama ANNA MKAPA ambapo watoto walemavu 50 waliweza kupatiwa baiskeli za watoto wenye ulemavu kutoka katika vituo mbali mbali jiji Dar es salaam.
·       Kupata usajili wa kamili,kuandikisha wanachama wapya na kuongeza hamasa kwa wazazi wenye watoto walemavu.
Changamoto:
·       ELIMU kuhusu upatikanaji wa watoto wenye ulemavu haijafikishwa kwa jamii vya kutosha,
·       Elimu juu ya utunzaji, mazoezi tiba, huduma za kijamii kwa wazazi imekuwa hairidhishi
·       Asilimia kubwa ya wazazi wenye watoto walemavu ni akina mama wa nyumban ambao hawana fursa ya kupata bima za afya hivyo utunzaji wa watoto  ni gharama kubwa.
Tunaamini-
Umoja daima ndio suluhisho kwa changamoto”
Kwa pamoja tukishikamana tutashinda. AHSANTE!


No comments: