Friday, May 17, 2013

MAELFU WAFURAHIA MCHEZO WA RUGBY UWANJA WA TWICKENHAM...

 Na Urban Pulse 
 Kila mahali zilijazana foleni. Za kuingia; kutokea, kununua vinywaji, kupata chips, nyama au vinywaji na za kuchangamkia majukwaa ya muziki na ngoma za Kiafrika. Ngoma hizo zilipigwa na bendi ya ACD Arts iliyoajiriwa na Hotel Marriott na wanamuziki mseto wa kijadi toka Uganda, Mali, Burkina Faso, Italia na Tanzania. 
Maelfu ya watu walijazana kushuhudia michuano ya mchezo wa Rugby baina mataifa mbalimbali ikiwemo Kenya na Afrika Kusini toka bara letu mama. Ilikua Jumamosi tarehe 11 Mei, 2013 ambapo uwanja maarufu wa Twickenham nje kidogo ya London, uligeuka ulingo wa mpira huu wa mikono, mieleka, kusukumana na mbio. Mashindano haya ya Sevens Series England yalishuhudia watani wetu wa jadi –Kenya wakiifunga Canada mabao 38 - 12, halafu Kenya ikachapwa 31-17 na New Zealand, baadaye wakawashinda Wales 31-19.
 Afrika Kusini nayo ilkuwa na matokeo yenye wastani huo huo kwa kuishinda Australia 5-0, Ufaransa 17-14 ila wakazabwa 19-12 na Marekani. Watazamaji waliokuja kwa mabasi na magari moshi walivalia na kuonyesha pia mavazi ya kila aina na ki ajabu ajabu kama sehemu ya starehe hii iliyochukua siku nzima. Wazee kwa watoto, akina dada na baba wa makamo- vijana na mama wa kila umbo na rika walijumuika katika hala hala ya kufurahia Rugby ambao kinyume na mpira wa soka, hauna fujo, na unahusudiwa zaidi na watu wa tabaka la kati kuelekea juu. 
Rugby wahitaji maguvu, wepesi, ustahilimivu na mabavu. Mfungaji bao huchukua mpira akatimka nao, huku wenzake wakimfukuza utadhani mwizi, akiwahi kuwasili mwisho wa kiwanja atajirusha chini , atauweka mpira ule wenye umbo la papai. Bao limeingia. 
Akizuiwa ataangushwa na juhudi zake zatakiwa amudu kuwarushia wenzake mpira kabla ya kusalimu amri. Kiyume na soka, Rugby kama mpira wa kikapu au nyavu huwa na mabao mengi sana. 
Wachezaji wanatakiwa wasemeshane na refa kwa heshima na nidhamu na kumwita “Bwana” au “Sir” kwa Kiingereza. 
Kijumla kati ya mataifa 21yaliyoshiriki michuano hii ya Sevens – majirani zetu wa Kenya wamechukua nafasi ya 5 wakiwa na pointi 99. Walioongoza ni New Zealand (pointi 173) wakifuatiwa na Afrika Kusini(132). Mashindano ya Seven Series huzunguka dunia nzima : Australia (Okt 2012) Dubai (Novemba 2012), New Zealand (Feb 2013), Marekani (Feb 2013), Hong Kong (Machi 2013), Japan (Machi 2013), Scotland na Uingereza (Mei 2013). 
 Ingawa Rugby imekuwa ikichezwa Ulaya kwa miaka mingi sana, uliwekewa sheria na kanuni rasmi hapa Uingereza karne ya 19. Rugby ya akina mama ilianzishwa rasmi miaka ya 1970 na inaendelea kuimarika Uingereza. -London, 12 Mei, 2013
ACD Arts band at Twickenham May 2013-pic by Urban Pulse
Bendi la Disco -Love Train- likifanya vitu vyake
Kenya wakichuana na New Zealand
Kiongozi wa ACD Arts -Stephen Kasamba-kushoto- akitingisha vitu

Maelfu ya Watazamaji

Mchezaji wa Kenya akipasha misuli joto kabla ya mechi
Uwanja wa Twickenham London
Vituko kila sehemu
Kenya wakichuana na New Zealand

No comments: