Wednesday, December 12, 2012

MKATABA WA SHERIA YA BAHARI UMECHANGIA UWEPO WA AMANI DUNIANI



Na  Mwandishi Maalum
Imeelezwa kwamba  Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Sheria ya Bahari ( UNCLOS),  Umesaidia sana katika kuifanya dunia kuwa mahali pa amani, utilivu na salama.
 Hayo   yamejiri wakati Baraza Kuu la 67 la Umoja wa Mataifa, lilipoadhimisha miaka 30 ya uzinduzi wa utiaji saini wa mkataba huo, mkataba ambao katika duru za kimataifa unatambulika kama “  Katiba ya Bahari”.
Uzinduzi wa utiaji saini wa mkataba huo ulifanyika desemba 10 mwaka 1982  huko Montego Bay, Jamaica baada ya kukamilika kwa mchakato mgumu wa majadiliano  uliodumu kwa miaka 10.
Maadhimisho hayo yamefanyika hapa Umoja wa Mataifa, ambapo  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki  Moon,amesema anatiwa moyo na mwitikio mkubwa ambao umeonyeshwa na jumuiya ya kimataifa katika kuutambua mkataba huo.
Pamoja na kuridhika huko  Ban Ki Moon amezitaka nchi ambazo bado hazijautambua au kuuridhia  kufanya hivyo, ili hatimaye  Mkataba huo ambao  ameutaja kama muhimili muhimu katika mstakabali wa mataifa na watu wake uweze kutambuliwa na nchi zote.
Hadi kufikia kipindi cha  maadhimisho ya miaka 30 tangu kuzinduliwa kwa mkataba huo mataifa 163 pamoja na Jumuiya ya Ulaya zimekwisha kuuridhia.
Karibu wazugumzaji wote waliozungumza wakati wa  maadhimisho hayo walieleza bayana kwamba, kwa hakika mkataba huo  umekuwa nguzo kuu ya kuwapo kwa hali ya amani na usalama duniani na  kwamba hali  ingekuwaje kama pasingelikuwapo mkataba huo ambao unaanishwa kama moja ya sehemu muhimu katika sheria za Kimataifa.
Kwa ujumla pamoja na mambo mengine mkataba huo ambao Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  ikiwakilishwa  wakati huo ,na Waziri Mkuu Mstaafu Mhe, Jaji Joseph Sinde Warioba,  akiwa kiongozi   wa  ujumbe wa watu watatu ukiwahusisha   Balozi Mstaafu Asterius Hyera na Jaji James Kateka.
Unaratibu na kusimamia kisheria,  masuala yote yanayohusu matumizi ya bahari, ikiwa ni pamoja na usimamizi na matumizi endelevu ya raslimali zinazopatikana baharini, utunzaji wa mazingira na viumbe hai na utatuzi wa migogoro inayohusiana na mipaka ya bahari au matumizi ya raslimali hizo.
Akiungana na wazungumzaji zaidi ya 50 waliozungumza wakati wa maadhimisho hayo, Balozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa  Mataifa, Tuvako Manongi, amesema.
 “Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa miongoni mwa nchi 119 zilizotia saini Sheria ya Mwisho ya Mkataba wa Sheria ya  Bahari. Mkataba huu ulikuwa kilele cha Sheria muhimu kupitishwa kwa njia ya majadiliano katika historia ya Umoja wa Mataifa”
  Akaongeza kwa kusema “Tanzania inathamini mchango mkubwa unaotolewa   kupitia mkataba huu.  Mkataba ambao nchi yangu uliuridhia septemba 30 mwaka 1985 ikiwa ni nchi ya 24 mwanachama wa mkataba. Tunaamini katika umuhimu wa  uwapo wa mkataba  na tunafarijika kwa mafaniko ambayo yamekwisha kupatikana hadi sasa”.
Aidha  Balozi Manongi  amesema, Tanzania  inatambua vema kwamba katika kipindi  cha miaka 30 ya uhai wa Mkataba huo, hapana shaka kumekuwapo na changamoto nyingi, na kwa sababu hiyo akasisitiza haja na umuhimu kwa  wadau wote kushirikiana katika  kuzikabili changamoto hizo.
Akabainisha pia kuwa yalikuwa ni  matumaini ya Tanzania kwamba, kila nchi itawajibika katika  kuhakikisha kwamba bahari inakuwa mahali salama kwa  shughuli za usafiri na usafirishaji, biashara ya kimataifa, uchimbaji wa mafuta na shughuli nyinginezo za kiuchumi.
Balozi  Manongi pia amesisitiza umuhimu wa nchi zinazoendelea kusaidiwa na kuwezeshwa  ili ziweze kunufaika vema na malengo ya Mkataba huo, lakini pia katika  matumizi sahihi na endelevu ya raslimali zinazopatikana baharini zikiwamo zile zilizo nje ya mipaka ya nchi husika na ambazo zinatambuliwa kama urithi wa mwanadamu.
Kama sehemu ya maadhimisho ya  mkataba huo, wajumbe waligawia kitabu ambacho ndani yake  kulikuwa na   maandiko  ya kihistoria kutoka  kwa baadhi ya  wajumbe walioshiriki mchakato wa majadiliano  yaliyofanikisha kuwapo kwa mkataba huo.
 Miongoni mwa watu mashuhuri waliorejea historia ya ushiriki wao  katika mchakato huo, na  ambao wametoa maadiko yao kupitia kijitabu hicho ni    pamoja na  Mhe, Jaji Joseph Warioba na Jaji James  Kateka. Ambapo kupitia maandiko yao wameeleza hali halisi ya kile walichokabiliana nacho katika kipindi chote cha maandalizi ya  mkataba huo.


No comments: