Sunday, February 25, 2018

DC TEMEKE AHIMIZA WAENDESHA BODABODA KUZINGATIA SHERIA ZA USALAMA BARABARANI

Na Emmanuel ,Globu ya Jamii

MKUU wa Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam, Felix Lyaniva amewataka madereva wa pikipiki na Bajaj kuwa makini na kuzingatia sheria za usalama barabarani ikiwemo kuvaa kofia ngumu na viatu wakati wanapoendesha vyombo vya moto.

Amesema lengo ni kuepuka ajali zinazosababishwa na madereva wazembe na kuwataka kufanya kazi kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Lyaniva ameyasema hayo leo, wakati wa utambulishaji rasmi wa mfumo wa namba utakaowatambulisha madereva pikipiki na bajaji katika vituo vyao mbalimbali katika katika Kata ya Kibondemaji, Mbagala Jijini Dar es salaamu uliofadhiliwa na Diwani wa Kata hiyo Abdallah. 

Diwani huyo ameshirikiana na Kampuni ya Tanzania Motorcycle and Bajaji Association (TAMOBA) kwa ajili ya kuzisajili Pikipiki na Bajaji katika mfumo wa GPS utakaowawezesha kujua Pikipiki iliyoibiwa ipo eneo gani na kuweza kupatikana kwa haraka zaidi.

Akizungumza zaidi Lyaniva amewapiga marufuku mgambo wa wilaya hiyo kutokamata pikipiki na Bajaj kwani wengi wao wamekuwa wakikamata pikipiki hizo bila ya kuzingatia sheria.

Amesena kazi ya kukamata bodaboda itafanywa na askari wenye weledi na wenye kujua sheria za usalama barabarani.Lyaniva pia amewapongeza TAMOBA kwa kuwafikia madereva bodaboda na bajaj kwani walikuwa na wasiwasi wa kuibiwa vyombo vyao na kuporwa na majambazi.

Ameongeza Diwani huyo ameleta maendeleo makubwa na mazuri katika Kata hiyo na pia TAMOBA imeleta usalama mzuri kabisa wa kisasa kwa kuwa madereva hao watafanya kazi zao wakiwa hawana wasiwasi wa kuibiwa Pikipiki zao na mali zao wawapo katika majukumu yao hayo pamoja na abiria wao.

Naye Diwani wa Kata ya Kibondemaji, Abdallah Mtinika amewashukuru TAMOBA kwani wameweza kumpatia refrector 300 kwa ajili ya madereva pikipiki katika kata yake hiyo na kuahidi kushirikiana na Bodaboda hao wa Kata yake.

Kwa upande wake, Ofisa Utumishi wa TAMOBA Erasto Lahi amesema Kampuni hiyo ilianzishwa rasmi mwaka 2006 na lengo ni kuwalinda madereva wa pikipiki na Bajaj na vyombo vyao.

Hivyo ameahidi kila bodaboda atapata sare ili kutambulika pia kuingizwa katika mfumo wa utambulishi utakaowatambua na kueleza mfumo huo utasaidia kuokoa gharama za kulipia Bima kubwa kwa kuwa kipengele cha hofu ya usalama wa chombo chake kitafanyiwa kazi masaa 24 labda iwe kwa sababu zingine, mfumo huu unawahakikishia wamiliki kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi watakuwa salama.

“Kila atakayesajiliwa na Kampuni hii atasajiliwa na mfumo maalum wa GPS utakaowezesha kujua Pikipiki iliyoibiwa ipo wapi, inatumiwa na nani na kuwezesha kui-lock hapohapo ilipo."Mtu aliye katika mfumo huu atapata msaada wa kulindwa kwenye mfumo muda wote saa 24, hivyo mmiliki wa chombo muda wowote akihitaji taarifa za chombo kilipo, kilipopita na kinapoelekea atazipata," amesema.

Amesisitiza pia mfumo huu utaunganishwa na Jeshi la Polisi moja kwa moja ili kuharakisha zaidi huduma za kiusalama.

Awali akisoma risala mbele ya mgeni rasmi Katibu wa Bodaboda Kata hiyo ya Kibondemaji Hassan Habibu amemshukuru Diwani huyo ambae ni mlezi wao na kueleza changamoto wanazokutana nazo ni pamoja na baadhi ya askari shirikishi maarufu kama mgambo kuwakamata nyakati za usiku bila utaratibu wa kisheria na kuwapiga kwa kutumia magongo bila ya kujua makosa yao.

Pia kutopata mikataba ya uhakika kutoka kwa wamiliki wa pikipiki hizo wanazoziendesha.


Mkuu wa Wilaya ya Temeke Mhe Felix Lyaniva akizungumza na madereva wa pikipiki na Bajaj juu ya kuzingatia sheria za usalama Barabarani ikiwemo kuvaa kofia ngumu na viatu wakati wanapoendesha vyombo vya moto,leo jijini Dar es Salaam.(picha na Emmanuel Massaka,Globu ya jamii)
Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es Salaam Kate Sylivia Magdalena Kamba akizungumza na akizungumza na madereva wa pikipiki na Bajaj juu ya kufanya kazi kwa kuzingatia sheria zilizopo, leo jijini Dar es Salaam.

Afisa Utumishi wa TAMOBA Bw. Erasto Lahi akizungumza na madereva wa pikipiki na Bajaj juu ya kuzisajili Pikipiki na Bajaj katika mfumo wa GPS utakaowawezesha kujua Pikipiki iliyoibiwa ipo eneo gani na kuweza kupatikana kwa haraka zaidi, le,jijini Dar es Salaam.
Semu ya madereva wa pikipiki na Bajaj piki na Bajaj wakiwa kwenye mkutano utambulishaji rasmi wa mfumo wa namba utakaowatambulisha madereva pikipiki na bajaji katika vituo vyao mbalimbali vya Kata ya Kibondemaji, Mbagala Jijini Dar es salaamu.

No comments: