Friday, January 29, 2016

MAHAKAMA KUU KANDA YA MWANZA YAFUTA KESI YA KUPINGA MATOKEO JIMBO LA TARIME VIJIJINI.

Kulia ni Mwl.Chacha Heche ambae ni Katibu wa Chadema Mkoani Mara akiongea na wanahabari nje ya Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza.

Na:George Binagi.
MAHAKA kuu Kanda ya Mwanza jana imeitupilia mbali kesi ya kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Novemba 25 mwaka jana, katika Jimbo la Tarime Vijijini Mkoani Mara, iliyofunguliwa na aliekuwa mgombea ubunge katika jimbo hilo kupitia Chama cha Mapinduzi CCM Christopher Ryoba Kangoye.

Katika kesi hiyo, wajibu maombi walikuwa ni Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini Mhe.John Heche (Chadema), Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambapo mtoa maombi alikuwa akiiomba Mahakama kutengua matokeo ya Uchaguzi Mkuu katika Jimbo hilo kwa kuwa haukuwa huru na haki.

Baada ya Mahakama hiyo kupitia kwa Jaji Lameck Mlacha kusikiliza utetezi wa pande zote, iliamua kuifuta kesi hiyo ambayo ilikuwa ni nambari nne ya mwaka 2015 kutokana na hoja za mleta maombi kuwa na kasoro mbalimbali ikiwemo kutoainisha majina ya waliokuwa wakilalamikiwa kuvuruga uchaguzi Jimboni humo.

Wakili wa mleta maombi Costantine Mutalemwa pamoja na Wakili wa mjibu maombi Paul Kipeja aliekuwa akisaidiana na Wakili Tundu Lisu katika kesi hiyo, wameelezea kuridhika na maamuzi ya Mahakama hiyo.

Nae Mwl.Chacha Heche ambae ni Katibu wa Chadema Mkoani Mara, ameelezea kuwa na imani na Mahakama kutokana na maamuzi iliyoyatoa katika kesi hiyo pamoja na kesi nyingine zilizowahi kuamuliwa Mahakamani hapo na kuongeza kuwa sasa kazi imebaki moja kwa Mhe.Heche ambayo ni kuwatumikia wakazi wa Jimbo la Tarime Vijijini.

Kwa upande wake Mrimi Zabloni ambae ni Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, ameelezea furaha kwa wananchi wa jimbo hilo huku akiwasihi kuweka imani na Mahakama hapa nchini katika kutoa maamuzi ya kesi mbalimbali.

Wananchi wengi Mahakamani hapo kutoka Jimboni Tarime Vijijini walikuwa ni wafuasi wa Chadema na wameonyesha kuyapokea maamuzi ya mahakama hiyo kwa furaha kubwa na kwamba wao waliamua ushindi wa Heche tangu Novemba 25 mwaka jana kwenye daftari la kupigia kura.

Kesi hiyo ilisikilizwa January 19,2016 mwaka huu na kuahirishwa hadi juzi January 27,2015 kwa ajili ya kutolewa maamuzi, lakini pia iliahirishwa hadi jana January 28,2016 ambapo maamuzi yameweza kutolewa.
Mrimi Zabloni (Katikati) ambae ni Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini akiongea na wanahabari
Wakili wa mjibu maombi Paul Kipeja akihojiwa na wanahabari
Wakili wa mleta maombi Costantine Mutalemwa  akihojiwa na wanahabari
Mwl.Chacha Heche ambae ni Katibu wa Chadema Mkoani Mara na wafuasi wengine wa Chadema wakifurahia baada ya maamuzi ya Mahakama
Mahakamani kabla ya mashauri kutolewa
Mahakamani kabla ya mashauri kutolewa
Mahakamani kabla ya mashauri kutolewa.

No comments: