Tuesday, December 1, 2015

WATENDAJI WA MASHIRIKA YA NDEGE WATAKA BARABARA YA KUELEKEA UWANJA WA NDEGE IPANULIWE

Watendaji wa mashirika ya ndege nchini wameiomba Serikali kupanua Barabara ya Nyerere ili kuwawezesha abiria wanaosafiri kwa ndege kuwahi usafiri kufuatia ongezeko lao kubwa na la ndege pia linalotarajiwa  kufuatia kuwepo kwa jengo jipya la abiria (TB III) linalotarajiwa kukamilika mwaka 2016.

Rai hiyo imetolewa jana na watendaji wa mashirika 19 ya ndege yanayoendesha shughuli zake katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) walipozuru ujenzi TB III ikiwa  ni moja ya ziara za wadau zinazoandaliwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA).
Baadhi ya CEOs wa mashirika ya ndege wakitoka kutembelea TB III (nyuma yao) jana JNIA.

Akijibu rai hiyo, Mkurugenzi wa Mradi wa TB III, Mhandisi Mohammed Millanga amesema, wameipokea kama changamoto lakini tayari walishawasiliana na mamlaka husika kuomba kuboreshwa kwa usafiri kwenda JNIA lakini jibu walilopata halioneshi suluhisho la haraka.

“Tuliwasiliana na Wakala wa Barabara (TANROADS) na Shirika la ReliTanzania (RAHCO). RAHCO walisema hawana mpango wowote kuhusu eneo hili. Wakala wa Mabasi ya Mwendo Kasi (DARTS) wao wameiweka Barabara ya Nyerere katika awamu ya tatu ya mradi wao. “amesema.
Mmoja wa CEOs akimwonesha Mhandisi Carloline Ntambo wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) inayojenga TB III, eneo ambalo wangependa kufanyia shughuli zao za huduma kwa abiria wa ndege.

Mhandisi Millanga amesema, katika kuhakikisha hakuna tatizo hilo, TAA iliwasiliana na wawekezaji wa treni ya juu kutoka Afrika Kusini lakini mpango huo haujazaa matunda. Hata hivyo, amesema, anaamini Serikali ya awamu ya tano itapata suluhisho la tatizo hilo mapema.

Watendaji hao walitaka kujua TAA imejiandaaje kukabiliana na foleni kubwa ya magari Jijini kuanzia eneo la TAZARA ili abiria wasichelewe ndege kufutia kuongezeka kwa abiria wakati TB III itakayokuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni sita kwa mwaka, itakapoanza kazi 2016.

Pamoja na changamoto hiyo, watendaji hao waliipongeza TAA kwa kujenga TB III kwa wakati muafaka na kueleza matumaini yao kuwa maeneo mengi ya miundombinu ya usafiri wa anga inayotakiwa kuwekwa TB III kwa ajili yao kama maofisi, maeneo ya biashara yatawekwa pia.

Watendaji hao walitaka kujua idadi ya ofisi za mashirika ya ndege na wakala wa huduma za usafiri wa anga,idadi ya kaunta za kuhudumia abiria, maeneo ya maofisa Uhamiaji, Usalama, Forodha, mizigo, ukatishaji tiketi, uunganishaji safari na mwingiliano wa TB III na TB II,

Pia walitaka kujua uwezo wa maegesho ya magari, ndege, biashara za maduka ya bidhaa zisizolipiwa ushuru, mahoteli, biashara ya magari ya kukodi na teksi, kituo cha ujazaji mafuta katika ndege na anayekiendesha, uhakika wa umeme, mfumo wa usalama wa abiria na mizigo.

Mhandisi Millanga amewaambia TAA imezingatia mahitaji mengi muhimu TB III ikiwemo kutenga maeneo ya abiria kusali, watoto kucheza na kuoga, sehemu za abiria na wafanyakazi kula, huduma za benki, jenereta la dharura la KV 33, umeme na mifumo mtambuka ya usalama.

Amesema wameweka mfumo mzuri  kuzuia majanga ya moto na kutakuwa na mwingiliano wa mfumo wa usalama kati ya TB III na TB II na ndege za mashirika yote zitaruhusiwa kunywa mafuta katika kisima kinachojengwa na kuendeshwa na Puma Energy iliyopewa zabuni hiyo.

Pia amesema, awamu ya kwanza ya TB III inayochukua abiria milioni 3.5 itakamilika Juni 2016 na ya pili Desemba 2017   ambapo TB II itafanyiwa ukarabati mkubwa kwa fedha zitakazotolewa na Ufaransa iliyolijenga mwaka 1984 likiwa na uwezo kuchukua abiria milioni 1.5 ( sasa 2.5m).

Hivi sasa TB III imekamilika kwa asilimia 65. Tayari wadau mbalimbali wametembelea ujenzi huo. Watendaji waliotembelea leo walitoka katika mashirika ya ndege ya Swissair, Oman Air, Air Seychelles, Mauritius Air, Fly Dubai, ATCL, South African Airways, Qatar Airways, Emirates n.k.
Mkuu wa Idara ya Masoko TAA, Ndugu Scolastica Mukajanga akiwaelekeza baadhi ya CEOs , maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli za mashirika yao TB III walipotembelea jengo hilo jana.
CEOs wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kutembelea TB III
Mkurugenzi wa Mradi wa ujenzi wa jengo la tatu (TB III) la abiria katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Mhandisi Mohammed Millanga akitoa taarifa kwa Watendaji Wakuu (CEOs) wa Mashirika ya Ndege kuhusu ujenzi wa TB III unavyoendelea walipotembelea jengo hilo jana.
Baadhi ya CEOs wakiangalia dari la TB III walipotembelea jengo hilo jana JNIA.

No comments: