Wednesday, September 2, 2015

LAPF WATOA TAHADHARI KWA WASTAAFU






  RPC wa Mkoa wa Dodoma SACP. David A. Misime akiongea na waandishi wa Habari leo akitoa tahadhari juu ya matapeli wanaowadanganya na kuwatapeli wastaafu. LAPF kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma imefanikiwa kumkamata mtu mmoja na kumfikisha Mahakamani baada ya kujifanya ni mtumishi wa TAMISEMI, LAPF na OFISI YA KATIBU MKUU WIZARA YA AFYA na kufanikiwa kuwaibiwa fedha kwa njia ya mtandao wastaafu kutoka katika mikoa mbalimbali.
   Mkurugenzi wa Huduma kwa Wanachama wa LAPF Bw. Valerian Mablangeti akitoa ufafanuzi katika mkutano huo na waandishi wa habari.
Baadhi ya washiriki.
MFUKO WA PENSHENI WA LAPF
  
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI TAREHE 02.09.2015
          MFUKO wa Pensheni wa LAPF unapenda kutoa kutoa tahadhari hasa kwa Wastaafu au wanaotarajia kustaafu, Idara, Wizara zote zinazoshughulika na wastaafu, Wakurugenzi wa Manispaa na Halmashauri kujihadhari na watu wanaowapigia simu na kujitambulisha kuwa wao ni watumishi wa Mashirika ya Hifadhi za Jamii na Idara zingine za Serikali na kwamba wanashughulika na mafao ya wastaafu.

          LAPF inatoa tahadhari hiyo kwa sababu kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma tumefanikiwa kumkamata mtu mmoja kwa jina la DAVID MAGESA MAKALI @ PETER MABULA na kumfikisha Mahakamani baada ya kujifanya ni mtumishi wa TAMISEMI, LAPF na OFISI YA KATIBU MKUU WIZARA YA AFYA na kufanikiwa kuwaibiwa fedha kwa njia ya mtandao wastaafu kutoka katika mikoa mbalimbali.

          Wanachofanya watu hao wanapiga simu Idara mbalimbali na kujifanya wapo TAMISEMI au Wizara nyingine na kuwataka wawatumie orodha ya wastaafu wa mwaka fulani pamoja na namba zao za simu. Inaonyeha kwa njia hiyo wameweza kupata orodha ya wastaafu takriban kutoka katika Mikoa 15 hususan kutoka Idara ya afya. 

Wakishapata orodha ya majina ya wastaafu na namba zao za simu humpigia mstaafu na kujitambulisha anatokea Wizarani na anashughulikia wastaafu ambao inaonekana walipunjwa kwenye mafao yao na inaonyesha naye amepunjwa kiasi cha milioni fulani. 

Ili aweze kumsaidia kurekebisha kumbukumbu na kumwezesha kupata fedha hizo amtumie kiasi fulani cha fedha. Mstaafu huyo akishamtumia hapatikani tena kwenye hiyo namba aliyotumia na mstaafu huyo anakuwa ameishaibiwa fedha zake.

          LAPF inatoa tahadhari kwa wastaafu wasikubaliane na watu wa aina hiyo na idara mbalimbali zichukue tahadhari kubwa na kila mara wahakikishe kinachohitajika kinatoka katika idara husika na kwa mtu sahihi.

Mfuko wa Pensheni wa LAPF unaendelea kutoa huduma bora kwa wanachama na wastaafu wake na katika kuhakikisha kuwa tunamlipa jana mstaafu wa kesho. LAPF inawakumbusha wanachama wake wanaokaribia kustaafu kuwasilisha mapema maombi ya mafao ya kusataafu (miezi sita kabla ya kustaafu) ili tuweze kuandaa mafao mapema.
         
LAPF ni Mfuko wa Pensheni ambao  pamoja na majukumu mengine, jukumu lake kuu ni kutoa mafao ya Pensheni kwa wanachama wake. Mafao yanayotolewa na LAPF ni pamoja na;
·        Pensheni ya Uzeeni.
·        Pensheni ya Ulemavu.
·        Pensheni ya Urithi.
·        Fao la Uzazi.
·        Mikopo ya kujikimu.
·        Mikopo ya elimu .
·        Mikopo ya nyumba.
·        Mikopo kwa wanachama wa kupitia Saccos.
·        Mikopo kwa Wastaafu.na
·        Msaada wa mazishi.
Kwa sasa Mfuko wa pensheni wa LAPF unaandikisha wanachama kutoka sekta zote kama vile Waalimu, Watumishi wa Afya, Wajasiliamali nk.

Imetolea na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa LAPF 

No comments: