Friday, July 31, 2015

ASKARI WA TANAPA ASHINDA TUZO YA ULINZI WA FARU BARANI AFRIKA

Askari wa Shirika la Hifadhi za Taifa(Tanapa)Daraja la Pili,Malale Patrick Mwita akiwa ameshika Tuzo na Cheti alivyokabidhiwa na Mwana wa Mfalme Albert wa Pili wa Monaco nchini Afrika Kusini wiki iliyopita katika mkutano na waandishi wa habari Makao Makuu ya Tanapa jijini Arusha.
Meneja Mawasiliano wa Tanapa,Pascal Shelutete akitangaza ushindi wa Tuzo hiyo akiwa na maafisa wa Shirika hilo  ambao wana jukumu la kuhifadhi maliasili kwaajili ya kizazi cha sasa na kijacho.
Waandishi wa habari wakimsikiliza Meneja Mawasiliano wa Tanapa,Pascal Shelutete akitangaza ushindi wa Tuzo hiyo ambayo imeipa heshima Tanzania katika mapambano yake dhidi Ujangili nchini.

Mwandishi wetu,Arusha
Askari Daraja la Pili ,Malale Patrick Mwita kutoka Hifadhi ya Taifa Serengeti ameshinda Tuzo ya kila mwaka ya Askari Bora katikaulinzi wa Faru kwa mwaka 2015 barani Afrika inayojulikana "2015 Rhino Conservation Awards"

Meneja Mawasiliano wa Tanapa,Pascal Shelutete ametangaza ushindi  huo leo katika ofisi za Makao Makuu ya Tanapa jijini Arusha.

Amesema Tuzo hiyo amekabidhiwa na Mwana wa Mfalme Albert wa Pili wa Monaco ambaye ni mlezi wa Tuzo hizo ambazo washindi walikabidhiwa Julai 27 mwaka huu nchini afrika Kusini.

Askari huyo ameibuka mshindi miongoni mwa washindani wengine kutoka nchi zote za Afrika zenye miradi ya kuendeleza Faru katika  ambapo Tuzo hizo hutolewa kila mwaka baada ya taasisi hiyo kutambua matendo ya kijasiri yaliyofanywa na askari huyo.

Baadhi ya matukio ya kijasiri yaliyofanywa na askari huyo ni askari pekee mwenye uwezo wa kuwatambua Faru zaidi ya asilimia 90  ndani ya Hifadhi ya Serengeti kwa kutumia alama za asili wakati mwaka 2007 alizuia tukio la kuuwawa kwa Faru na mwaka 2008 alishiriki kukamata silaha  5 za kivita. 

Amesema mradi wa Faru wa Moru,serengeti ndio mradi mkubwa kabisa wa faru wenye mafanikio barani Afrika unaoongoza kwa kasi ya kuzaliana ambayo ni zaidi ya asilimia 5 kwa mwaka.

Tuzo hizo huandaliwa pamoja Wizara ya Mazingira ya Afrika Kusini ambayo inahusika na Utalii.

Malale amesema Tuzo hiyo imempa hamasa ya kutambua mchango wa askari katika kukabiliana na majangiri hatari wanaotumia silaha za kivita kwaajili ya kuwinda Faru na Tembo .

"Tuzo hii ni heshima kubwa kwa Tanapa na nchi yetu kwa ujumla katika kuhakikisha tunawalinda wanyama hawa ambao wako katika hatari ya kutoweka kila mmoja wetu ni mdau muhimu kuhakikisha Faru anaishi."amesema Mwita.

No comments: