Tuesday, September 2, 2014

Umoja wa Azaki za Vijana wakutana na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba.

Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta akiongea na Umoja Azaki za Vijana wakati alipofanya mkutano nao wakati wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Kiongozi wa msafara wa Umoja wa Umoja wa Azaki za Vijana Alfred Kiwuyo akisoma taarifa ya mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Paul Makonda akisisitiza juu ya Katiba kuweka kipengele cha kuwezesha kuundwa kwa Baraza Huru la Vijana la Taifa wakati Umoja wa Azaki za Vijana wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Vijana wanaounda Umoja wa Azaki za Vijana wakisikiliza kwa makini maneno mazuri toka kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba (hayupo pichani) wakati walipokuwa wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakiwa kazini kufuatilia mambo yakiyoendelea katika mkutano huo wa Umoja wa Azaki za Vijana uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma.
Kiongozi wa msafara wa Umoja wa Umoja wa Azaki za Vijana Alfred Kiwuyo (kulia) akikabidhi taarifa kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakati wakiwasilisha mapendekezo ya maboresho ikiwa ni msisitizo katika masuala yao ya vijana, mkutano uliofanyika 02 Septemba, 2014 katika Ukumbi wa Spika Mjini Dodoma. (Picha zote na Benedict Liwenga, Malezo-Dodoma)

UMOJA wa Azaki za Vijana wakutana na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakiwa na lengo la kuja kuwasilisha mapendekezo yao kwa ajili ya maboresho ya Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya.

Akizungumza kwa niaba ya vijana wenzake, Kiongozi wa msafara huo Alfred Kiwuyo amesema kuwa Azaki hizo za vijana zilishiriki mchakato mzima wa Katiba katika hatua zote muhimu ikiwemo kukusanya maoni na kuyawasilisha mbele ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Pamoja na ushiriki huo, Bw. Kiwuyo ameeleza kuwa sehemu kubwa ya maoni ya vijana yamejumuishwa katika kifungu cha 44 cha Rasimu ya Pili ya Katiba, na mjumuisho huo wa haki na wajibu wa vijana umefinya sana maoni ya vijana katika Rasimu hiyo.

“Lengo kuu la mtazamo huu sio kuleta hoja mpya, bali ni kuboresha Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya na katika maboresho hayo tunapendekeza mambo matatu ya msingi, kwanza ni kuwekwa kwa tafsiri ya neno kijana katika Rasimu, kutenganisha haki na wajibu wa vijana na mwisho ni kuweka kifungu kitakacho wezesha kuundwa kwa Baraza huru la Vijana la Taifa”, alisema Kiwuyo.

Aidha, Kiwuyo ameongeza kuwa Azaki za vijana zinatambua kuwa haki ya uandishi wa Katiba ni ya kila Mtanzania na kwa utaratibu waliojiwekea wao wenyewe Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba ndiyo wawakilishi wao katika hilo, hivyo wanamatumaini makubwa kuwa Katiba itaandikwa na Watanzania wa makundi yote wakiwemo na vijana.

Naye Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta amesema kuwa Ibara ya 44 katika Rasimu ya Tume inayuzungumzia mambo ya vijana imekuwa fupi na imeacha baadhi ya mambo muhimu zikiwemo haki ambazo hazikuelezewa vizuri, mambo ya haki na wajibu wa vijana na pia haijataja juu ya chombo cha uwakilishi cha vijana.

“Hii Ibara ya 44 katika Rasimu ya Tume imekuwa fupi na imeacha baadhi ya mambo muhimu, hivyo niwahakikishieni kuwa mawazo haya ya vijana tutawafikishia wahusika ambao ni Kamati ya Uandishi na Uongozi wa Bunge Maalum la Katiba ili yaweze kufanyiwa kazi, lakini pia suala la wajibu ambalo mmeliomba ni jambo zuri kwa ninyi vijana kwani ni muongozo”, alisema Mhe. Naye Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Paul Makonda amemshukuru Mwenyekiti wa Bunge hilo, kwa kupokelewa kwa vijana hao kama kundi kubwa katika jamii na amesisitiza juu ya Katiba kuwezesha kuundwa kwa Baraza Huru la Vijana la Taifa kwani litawezesha kuwaunganisha vijana nchini.

“Baraza kwetu ni jambo la msingi kwani litakuwa ni chombo kitakachotusaidia katika mambo ya uwakilishi kwa vijana nchini, kwani hivi sasa hatuna vijana wenye kuwakilisha vijana wenzao katika mambo mbalimbali kupitia chombo kama hiko, hivyo Katiba iweke kipengele kitakachowezesha kuundwa kwa chombo hiko”, alisema Makonda.

Makonda alisisitiza kuwepo na haki, wajibu na uwajibikaji kutasaidia kuwa na vijana waadilifu na wenye kuzingatia maadili.

Azaki za Vijana katika mchakato wa Katiba zinajumuisha Tanzania Youth Vision Association (TYVA), FEMINA, Restless Development, Tanzania Youth Coalition (TYC), Youth of United Nations Association of Tanzania (YUNA) pamoja na TAMASHA.

No comments: