Monday, February 3, 2014

Rais wa Zanzibar Dk.Shein afanya mazungumzo na Makamo wa Rais India

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein akiwa kwenye picha ya pamoja na Makamu wa Rais wa India Mohamed Hamid Ansari wakati walipokuwatana nchini India.

Tanzania na India zimeeleza kuridhishwa na uhusiano na ushirikiano uliopo baina yao na kusisitiza dhamira ya kweli ya kuona kuwa ushirikiano huo unazidi kuimarika kwa manufaa ya Serikali na wananchi wa nchi hizo.

Hayo yamejitokeza leo wakati wa mazungumzo kati ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na Makamu wa Rais wa India Mohamed Hamid Ansari.

Katika mazungumzo hayo viongozi hao wamesema kuwa uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo ulioanzishwa mwanzoni mwa miaka ya sitini umekuwa ukiimarika mwaka hadi mwaka kwa kuongeza maeneo ya ushirikiano katika nyanja mbalimbali za uchumi na kijamii.

Wameeleza kuwa ziara za viongozi wa nchi hizo pamoja na ziara za mara kwa mara katika ngazi ya mawaziri ni uthibitisho wa uhusiano huo mzuri kati ya nchi hizo.

Katika mazungumzo hayo Dk. Shein ameupongeza ushirikiano uliopo kati ya Zanzibar na India na ameishukuru Serikali na wananchi wa India kwa misaada mbalimbali ambayo imekuwa ikiitoa kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wake.

Dk. Shein alimueleza Makamu wa Rais wa India kuwa ziara yake nchini humu imelenga kuimarisha uhusiano huo wa kidiplomasia uliasisiwa miaka ya sitini chini ya misingi imara ya urafiki iliyowekwa na waasisi wake viongozi wa kwanza wa nchi mbili hizo.

Halikadhalika alimueleza kuwa ziara hiyo amedhamiria kukukuza ushirikiano kati ya Zanzibar na India katika maeneo ya elimu, mafunzo, biashara, kilimo pamoja na kuhimiza uwekezaji katika sekta mbalimbali za uchumi.

Alifaanua kuwa uhusiano na ushirikiano kati ya watu wa Zanzibar na watu wa India ni wa kihistoria uliodumu kwa karne nyingi hivyo kuufanya kuwa wa kidugu.

Amemueleza Bwana Ansari kuwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imefurahishwa na msaada wa ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Amali kitakachojengwa huko Pemba pamoja na makubaliano yaliyofikiwa jana ya kuanzisha Chuo kama hicho huko Unguja kupitia Chuo cha Barefoot cha Tilonia, Jaipur.

Amebainisha kuwa katika miaka ya hivi karibuni kumekuwepo na wananchi wengi wa Zanzibar wanakwenda India kwa sababu za kimatibabu hivyo ametaka kuwepo na ushirikiano zaidi wa namna bora ya kuleta wagonjwa hao nchini humu.

Kwa upande mwingine Dk. Shein ameiomba Serikali ya India kuangalia namna inavyoweza kushirikiana na Serikali ya Zanzibar kuisaidia upatikanaji wa madawa kwa Zanzibar.  

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ametumia fursa kumueleza Makamu wa Rais wa India haja ya kuongeza fursa zaidi za masomo ya muda mfupi na muda wa kati kwa wananchi wa Zanzibar ili kujenga uwezo katika taaluma mbalimbali ili kuharakisha maendeleo.  

Kwa upande wake Makamu wa Rais wa India Bwana Mohamed Hamid Ansari amemhakikishia Dk. Shein kuwa Serikali ya nchi yake itaendelea kusaidia jitihada zinazofanywa na Serikali na wananchi wa Zanzibar za kujiletea maendeleo.

Bwana Ansar amesema uhusiano wa kihistoria wa wananchi wa India na Zanzibar ulioanza karne nyingi tangu enzi za kutegemea pepo za Kusi na Kaskazi umekuwa imara na kila siku wananchi wake wameonyesha ari ya kuzidi kuuimarisha. 

Mapema asubuhi alitembelea makumbusho ya Mahatma Ghandi iliyopo mjini New Delhi ambapo aliweka shada la maua pamoja na kusaini kitabu cha kumbukumbu.

Baadae mchana anatarajiwa kukutana na watanzania anaoishi mjini hapa katika ukumbi wa Urafiki kwenye hoteli ya Ashok na atakutana pia na Waziri wa Afya na Ustawi wa Familia wa India. Jioni atahudhuria chakula cha jioni kilichoandaliwa kwa heshma yake na mwenyeji wake Makamu wa Rais wa India.

Hapo jana kabla ya kuondoka Jaipur, Jimbo la Rajastan, kuja New Delhi Dk. Shein alitembelea makumbusho ya Hawa Mahal na Albert yaliyopo mjini humo.

Miongoni mwa waliofuatana na Rais katika ziara hiyo ni pamoja na Mke wake Mama Mwanamwema, Waziri wa Fedha Omar Yusuf Mzee, Waziri wa Uwezeshaji, Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto Bibi Zainab Omar Mohamed, Waziri wa Biashara na Viwanda na Masoko Nassor Ahmed Marzui, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Dk. Mahadhi Juma Maalim na Balozi wa Tanzania nchini India Injinia John Kijazi.

Wengine ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya Mohamed Saleh Jidawi, Katibu Mkuu Kilimo na Maliasili Affan Othman Maalim, Mshauri wa Rais Ushirikiano wa Kimataifa, Uwekezaji na Uchumi Balozi Mohamed Ramia na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Zanzibar –ZIPA Salum Khamis Nassor.

No comments: