Friday, June 8, 2018

DK. KIKWETE AISHAURI CMSA KUTOA ELIMU KUHUSIANA NA FAIDA ZA HISA

CMSA yairudisha NICOL soko la hisa

Na Chalila Kibuda, Globu ya Jamii

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne , Dk.Jakaya Mrisho Kikwete ameishauriwa Mamlaka ya Masoko na Mitaji ya Dhamana (CMSA) kutoa elimu kwa watanzania kuhusiana na ununuaji wa hisa katika soko la hisa.

Kikwete ameyasema wakati hafla ya Kampuni ya NICOL kurudishwa katika Soko la Hisa Dar es Salaam(DSE) baada ya kukidhi vigezo vya kisheria kuongia katika soko hilo, amesema CMSA ikitoa elimu kwa wananchi kutafanya kuongeza hamasa ya ununuaji hisa kuliko ilivyo sasa.

Dk.Kikwete amesema kuwa CMSA ikitoa elimu kutafanya kampuni nyingi kuorodheshwa katika soko la hisa na kufanya uwekezaji wa miradi mingine.Aidha amesema kutokana na ukuaji wa teknolojia katika masoko CMSA imeshauriwa kuboresha zaidi manada wa soko la Hisa wakati wa kufungua na kufunga.Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete alisema kwamba lengo la kuisajili Nocol ilikuwa ni kuwasaidia .

"Nakumbuka wakati serikali inauza hisa zake NMB kulikuwa na mjadala mkali wa kuhoji kwanini nicol wapewe asilimia tano, lakini kwa imani kwamba hii ni kampuni ya wazalendo, basi tukachukua uamuzi kuwapa wazalendo," alisema.Kikwete kwamba hakuwahi kuusikia mgogoro wa NICOL wakati wa utawala wake.

"Lengo lilikuwa kusaidia wazawa kujijenga kuichumi na kukuza maendeleo, nimesikia leo (jana) hadithi ya Nicol katika uongozi wangu sikusikia kabisa mgogoro wao," alisema Kikwete.Aidha aliipongeza CMSA kwa utendaji kazi wake, ikiwemo kusimamia kwa madhubuti masoko ya mitaji.

Nae Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko na Mitaji ya Dhamana (CMSA), Nicodemus Mkama,amesema kuwa imefanikiwa kuorodhesha hisa 69,165,170 za Kampuni ya Uwekezaji wa Pamoja ya National Investment Company Limited (NICOL) katika soko la hisa la Dar es Salaam (DSE) ni kutokana na kukidhi vigezo vya kisheria .

Amesema NICOL iliondolewa katika orodha ya kampuni ya kampuni zilizoorodheshwa DSE Juni 2011 kutokana na matatizo ya kiutendaji katika uwekezaji katika uwekezaji.mamlaka iliidhinisha mauzo ya awali ya hisa za Kampuni ya NICOL kwa umma yaani (Initial Public Offers – IPO). 

Amesema kwamba mauzo hayo yalifanyika katika awamu mbili, moja ikiwa ni Novemba 2004 ambapo Kampuni NICOL ilifanikiwa kukusanya sh. bilioni 3.9 na awamu nyingine ilifanyika Oktoba mwaka 2007, ambapo jumla ya sh. bilioni 5.6 zilikusanywa. 

"Kutokana na mwenendo mzuri wa mauzo ya hisa, Kampuni hii ilifanikiwa kuorodheshwa katika soko la hisa la Dar Es Salaam Julai 15, 2008. Hata hivyo, kutokana na matatizo ya uongozi na kiutendaji katika uwekezaji,kampuni hii tuliiondoa sokoni Juni mwaka 2011 na CMSA iliamuru kuwasimamishwa kwa Wakurugenzi wa Bodi na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya NICOL ili kuwezesha uongozi mpya kuteuliwa na wanahisa wote,"alisema.

Mkama alisema kwamba Aprili 14, 2012, Kampuni ya NICOL ilifanikiwa kupata uongozi mpya chini ya Mwenyekiti wake Dk. Gideon Kaunda na ofisa Mtendaji Adam Kinoni ambao ulithibitishwa kupitia Mkutano mkuu wa wanahisa wote.

"Uongozi huu umeweza kushughulikia matatizo ya uendeshaji wa kampuni na uwekezaji ambayo yalisababisha Kampuni hii kuondolewa katika soko la hisa,NICOL pia imeweza kutekeleza maelekezo yote yaliyokuwa yametolewa na CMSA Mamlaka ili kukidhi hadhi ya kuendelea kuwa kwenye Soko la Hisa.

Mkama aliyataja masharti ambayo CMSA ilitoa kwa NICOL nikutoa notisi kwa wanahisa kuwaelezea kile kinachoendelea ndani ya kampuni na kutayarisha mkutano mkuu wa wanahisa,kuhakikisha mahesabu ya NICOL tokea mwaka 2009 yanakamilishwa kama ilivyopangwa, Kuteua wakaguzi wa nje (External Auditos) kwa ajili ya hesabu za kampuni kwa miaka ya fedha 2010-2015 ili kuhakikisha kuwa mkutano mkuu unafanyika Octoba.

Amesema masharti mengine waliyowapa ni Kutayarisha taarifa ya shughuli za kampuni ikiwemo kuiwezesha kuanza kutekeleza kazi zake na kuangalia uwezekano wa kuirudisha kampuni sokoni. 

Mkama alisema NICOL imefanya mabadiliko ikiwa ni pamoja na kuandaa mkakati mpya wa uwekezaji unaohusisha kuugawa uwekezaji wake kwenye dhamana za serikali kwa lengo la kupata anuwai, kuleta ulinzi wa mtaji na uongozi madhubuti. 

"Mageuzi makubwa ya kiutendaji na matokeo mazuri ya mwenendo wa Kampuni ya NICOL ni matokeo ya usimamizi madhubuti wa CMSA uliodhihirika katika kusimamia sheria, miongozo na kanuni za masoko ya mitaji. Misingi hiyo ndiyo iliyotumika kuiwakilisha serikali kulinda masilahi ya wawekezaji katika kampuni ya NICOL, na hivyo kukuza thamani ya uwekezaji kutoka sh. 4.6 bilioni Mwaka 2004 mpaka Sh. Bilioni 96.2 mwaka 2017, sawa na ongezeko la asilimia 1,991,"alisema.

Mwenyekiti wa DSE, Jonathan Njau, alisemakwamba DSE wana furaha kuiona Nikol ikirejea tena katika soko la hisa kwaajili ya kuuza, kununua, na kukuza uchumi wa kampuni pamoja na taifa.

Aliwaasa viongozi wa Nicol kufuata taratibu ikiwa wanataka kuendelea kukaa katika soko lazima wafuate sheria na utaratibu ikiwemo kutengeneza mahesabu na kukaguliwa kwa uwazi.Mwenyekiti bodi ya NICOL, Dk. Gideon Kaunda, alisema kwamba wamerudi sokoni kwa kasi hivyo itauza, kununua na kuzalisha zaidi.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete akigonga kengele kwa ajili ya kufungua soko la hisa la Dar es Salaam (DSE) kuingia kampuni ya NICOL.
Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko na Mitaji ya Dhamana (CMSA), Nicodemus Mkama akitoa maelezo kwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kuhusiana na kuingia NICOL katika Soko la Hisa la Dar es Salaam , jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti bodi ya NICOL, Dk. Gideon Kaunda akitoa maelezo kwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kuhusiana na kuingia NICOL katika soko hisa na changamoto walizoweza kukabiliana nazo .
Picha za pamoja za makundi mbalimbali katika hafla ya CMSA kuisajili NICOL kwa mara nyingine
Picha za pamoja za makundi mbalimbali katika hafla ya CMSA kuisajili NICOL kwa mara nyingine

Picha za pamoja za makundi mbalimbali katika hafla ya CMSA kuisajili NICOL kwa mara nyingine

Picha za pamoja za makundi mbalimbali katika hafla ya CMSA kuisajili NICOL kwa mara nyingine

No comments: