Friday, February 23, 2018

UWEPO WA VIWANDA UTACHANGIA UZALISHAJI WA BIDHAA ZA KILIMO-MHANDISI STELLA MANYANYA


Na Humphrey Shao, Globu ya Jamii

NAIBU Waziri wa Viwanda, Uwekezaji na Biashara Mhandisi Stella Manyanya amesema uwepo wa viwanda nchini utachangia kwa kiasi kikubwa uzalishaji wa bidhaa za kilimo kwa kuwahakikishia wakulima wanakuwa na soko la uhakika.

Mhandisi Manyanya ameyasema hayo leo jijijini Dar es Salaam wakati wa kongamano la wajibu wa taasisi za fedha katika kuendeleza viwanda nchini lililoandaliwa na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA).

Amesema ili kufikia malengo hayo kunahitajika ushirikiano mkubwa kati ya sekta binafsi na Serikali kwa kuweka mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara."Tasisi za fedha mnatakiwa kuhakikisha mnatatua changamoto za wajasiriamali za ukosaji wa mitaji jambo ambalo limekuwa likiwasumbua wengi wao, ili kuhakikisha tunafikia Tanzania ya viwanda" amesema.

Mhandisi Manyama, amesisitiza ikiwa taasisi za fedha zitasaidia kukuza uchumi kupitia viwanda maana yake itakuwa chachu ya kukuza kipato cha wawekezaji na kuongeza mnyororo wa thamani.

“Kuna changamoto kadhaa katika taasisi za fedha ambazo ni lazima zifanyiwe kazi kwa sababu wafanyabiashara wengi wanapokopa fedha kwa mfano kununua mashine wanatumia muda mrefu kutafuta ushauri. Niwaombe kuwasaidia kuwapa ushauri pale mnapowakopesha,"amesema Mhandisi Manyanya

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Geofrey Simbeye, ameishauri Serikali kuanzisha benki maalumu zitakazosadia kutoa mikopo ya kuanzisha na kuendeleza viwanda kama imekusudia kufikia uchumi wa kati unaotegemea sekta hiyo.

Pia Simbeye amesema licha ya ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania(BoT) kuonesha Sh. trilioni 16.3 zilitolewa kwa sekta binafsi ni alisimia 9.8 tu ya fedha hizo iliyoelekezwa sekta ya uzalishaji huku kiasi kikubwa kikielekezwa kwenye biashara.

“Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB, Charles Kimei, amezungumza mambo mengi, lakini ninachosisitiza ni lazima tuwe na mfumo mpya, kwa sababu kama fedha zilizokopeshwa kwa private sekta ni Sh.trilioni 16.3, kwa mujubu wa taarifa ya BoT.

“Na ripoti ya Benki Kuu hiyo hiyo, inaonesha katika hizo ni asilimia 9.8 tu ndizo zimekwenda kwenye viwanda. Sasa tunajiuliza kwa ‘rate’ hiyo tutafika kwenye viwanda? Amehojia Simbeye.Amesema benki za kibiashara zimekuwa zikiangalia zaidi wapi zinapata faida ambapo mikopo inaweza kurudi haraka, ambapo mikopo mingi imekuwa ikielekezwa kwenye biashara ambako watu wengi hukopa ili kuagiza bidhaa za biashara na kujenga nyumba tofauti na uwekezaji wa viwanda ambao ni wa muda mrefu.

“Sasa tunajiuliza swali je, tutaendelea kutegemea benki hizi za kibiashara katika kuendeleza viwanda hapa Tanzania? Tunatakiwa kufikiria nje ya boksi nini tufanye.

“Kujenga uchumi wa viwanda nchini Tanzania ni sawa sawa na projecti ya kitaifa yaani ni project ya kujenga Taifa ndiyo itakayotulepeka kwenye uchumi wa viwanda na kama tunaichukua kama project ya kitaifa lazima tuje na mfumo tofauti wa kuiwezesha,” amesema Simbeye.

Amesema mchakato wa ujenzi wa viwanda unapaswa kuchukuliwa kama unavyochukuliwa mradi wa ujenzi wa reli ya kiwango cha kimataifa (standard gauge) ambapo Rais amesema anazo zaidi ya Dola za Marekani bilioni 3.5 za kujenga mradi huo kuanzia Dar es Salaam hadi makao makuu ya nchi Dodoma.

Amesema hivyo ni vema kuwa na chombo maalumu kitakachokuwa kikitoa mikopo ya maendeleo hasa sekta ya viwanda ili kuwezesha kufikia lengo la uchumi wa kati unaotegemea viwanda.“Hakuna kiwanda kinaanzishwa kikae miaka mitano, kiwanda ni project za milele na milele, wewe mwanzishaji utakufa lakini kile kiwanda kipo, kwa hivyo vinahitaji uwekezaji wa muda mrefu.

“Tatizo hapa wanaangalia faida zaidi lakini tukiwa na ‘industrial development bank’ kama TIB ni kama una-empower watu kuanzisha viwanda,” amefafanua Simbeye.Ameongeza sensa ya maendeleo ya viwanda ya mwaka 2013 iliyozinduliwa mwaka 2016 inaonesha Tanzania ina jumla ya viwanda 49,242 lakini viwanda vikubwa ni 1,322 tu. "Hivyo ni vema kujiuliza kwanini viwanda vidogo ndiyo vingi na kwanini visianzishwe viwanda vikubwa".

Amesema tatizo kubwa ni ukosefu wa mitaji, hivyo ni vema kusaidia kuanzishwa viwanda vingi vikubwa vitakavyosaidia pia kuanzishwa kwa viwanda vidogo vitakavyokuwa vinazalisha malighafi kwa za viwanda vikubwa na kutoa ajira nyingi kwa wananchi.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Mabenki ya Tanzania, Dk. Charles Kimei, amesema licha ya taasisi za fedha kuwa na jukumu la kusaidia upatikanaji wa fedha kwa watu bado kuna changamoto nyingi nchini ikiwamo wafanyabiashara wengi wazawa kutoaminika katika taasisi za fedha hususani za kigeni.

Dk. kimei amesema kutokana na changamoto nyingi zinazowakabili wajasiriamali wadogo na wa kati taasisi za fedha nchini zinapaswa kuongeza ushirikiano na wajasiriamali hao badala ya kufikiria viwanda vikubwa tu.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara , Mhandisi Stela Manyanya akizungumza wakati wa ufunguzi wa Kongamano lililofanyika katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere(MNMA) kuhusu wajibu wa taasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania.
Mkurugenzi wa Benki ya CRDB Nchini na Mwenyekiti wa jumuiya ya Mabenki , Charles Kimei akichokoza mada wakati wa Kongamano kuhusu wajibu wa Tasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania.
Mkurugenzi Mtendaji wa Tasisi ya Sekta Binafsi Nchini(TPSF),Geoffrey Simbeye, akichokoza mada wakati wa kongamano la kujadili umuhimu wa mabenki na sekta binafsi katika maenedeleo ya Viwanda.
Naibu Mkuu wa Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Dr.Thomas Ndaluka akitoa neno kwenye Kongamano kuhusu wajibu wa Tasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania. 
Mhadhiri wa Chuo Cha MNMA, Binto akitoa mada ya Ujasiliamali ktika Uwekezaji wa Viwanda kwa mfumo wa ushirikiano kati ya sekta ya Umma na Sekta Binafsi.
Mkurugenzi wa Uchumi ,Utafiti na Sera , Benki kuu ya Tanzania Johson Nyela akichangia jambo wakati wa Kongamano kuhusu wajibu wa Tasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania.
Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Kisare Makori akiwa ameketi pamoja na Washiriki wengine wa Kongamano kuhusu wajibu wa Tasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania.
Mkuu wa Chuo Cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere , Prof Shadrack Mwakalila wa kwanza kulia akiwa ameongozana na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara , Mhandisi Stela Manyanya (Katikati) pamoja na Mkurugenzi wa Benki ya CRDB Nchini na Mwenyekiti wa jumuiya ya Mabenki , Charles Kimei 
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara , Mhandisi Stela Manyanya wakati wa Kongamano kuhusu wajibu wa Tasisi za fedha katika kuendeleza Viwanda Tanzania.

No comments: