Sunday, October 9, 2016

MKURUGENZI MKUU WA PPF, WILLIAM ERIO AKAGUA ENEO LITAKALOTUMIKA KUJENGA KIWANDA KIPYA CHA KUCHAKATA NGOZI NA KUTENGENEZA VIATU, GEREZA LA KARANGA MJINI MOSHI


Mkuu wa gereza la Karanga, mjini Moshi, mkoa wa Kilimanjaro, ambako ndiko kilipo kiwanda cha kutengeneza viatu, Kamishna Msaidizi wa Magereza, (ACP), Hassan Bakari Mkwiche, (kushoto), akionyesha kitu, wakati Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PPF, William Erio, (wakwanza kulia), alipotembelea kiwanda hicho ili kuona eneo lililotengwa kwa ujenzi wa kiwanda kipya cha kisasa cha viatu, Oktoba 9, 2016. Wengine pichani ni Mkurugenzi wa Uwekezaji wa PPF, Steven Alfred, (wapili kushoto), Mkuu wa magereza mkoani Kilimanjaro, Kamishna Msaidizi wa Polisi, (ACP), Anderson Kamtera.
Bw. Erio, na maafisa wake, wakipatiwa maelezo na maafisa wa Jeshi la Magereza alipokagua moja ya maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda hicho

NA K-VIS MEDIA, MOSHI

MKURUGENZI Mkuu wa Mfuko wa Pensheni wa PPF, Bw.William Erio, ametembelele kiwanda cha kutengeneza viatu cha Karanga mjini Moshi mkoani Kilimanjaro Oktoba 9, 2016, ili kuona eneo ambalo kitajengwa kiwanda kipya na cha kisasa.

Bw. Erio ambaye alifuatana na Mkurugenzi wa Uwekezaji wa Mfuko huo, Bw. Steven Alfred, na Meneja Uhusiano, Bi.Lulu Mengele, pia alipata fursa ya kupokea taarifa ya uendeshaji wa kiwanda cha sasa na changamoto zinazokikabili. Bw. Erio alisema, ziara yake inalenga kujua mambo mawili ambayo ni kuona eneo patakapojengwa kiwanda kipya cha kutengeneza bidhaa za ngozi, lakini pia kupata uelewa wa nini kifanyike ili kuboresha kiwanda cha sasa ambacho kilijengwa mwaka 1977.

Maafisa wa kiwanda hicho, walimuonyesha maeneo mawili ambayo yanafaa kujengwa kiwanda hicho. “Kama mtakumbuka, wiki iliyopita mimi na Kamishna Jenerali wa Magereza, (CGP), John Minja tulisaini makubaliano ya ushirikiano kati ya PPF na Jeshi la Magereza katika kukiboresha kiwanda cha kutengeneza viatu cha Karanga, lakini pia kujenga kiwanda cha kisasa cha kuchakata ngozi na kutengeneza bidhaa zitokanazo na ngozi.” Alianza kwa kusema.

Alisema, nia ya Mfuko ni kuona kazi ya ujenzi wa kiwanda kipya inakamilika ifikapo Desemba 2018 ili kutekeleza azma ya serikali ya awamu ya tano ya kujenga uchumi wa viwanda. “Wakati tukisubiri ujenzi wa kiwanda kipya ukamilike, lazima pia tuboreshe hiki cha sasa kwa kuimarisha miundombinu iliyopo, na hivyo kuongeza uzalishaji na kupanua masoko ” alisema Bw. Erio.

Aliagiza wataalamu wa PPF kwa kushirikiana na wenzao wa Magereza (kiwanda cha Karanga), wakutane haraka ili kuainisha chamngamoto zinazokikabili kiwanda cha sasa, ili uboreshaji wa mitambo uweze kufanyika kwa haraka.” Alifafanua.

Awali Kaimu Mkuu wa kiwanda cha viatu Karanga, Naibu Mrakibu wa Magereza,( ASP), Michael Minja, alisema kiwanda cha sasa kinakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwa ni pamoja na uchakavu wa mitambo, ambapo alisema baadhi ya mashine zimepitwa na wakati na zingine zimeharibika na hivyo zinahitaji kufanyiwa ukarabati mkubwa.

“Mambo yanayotakiwa kufanyiwa kazi ili kuwezesha uendeshaji bora wa kiwanda, ni pamoja na kununua vipuri kwa ajili ya ukarabati wa baadhi ya mashine, lakini pia kuna upungufu wa baadhi ya mashine hivyo tunahitaji kuongeza idadi yake.” Alisema ASP Minja.

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna Jenerali wa Magereza, Kamishna wa Magereza, (CP), Editha Malya, alisema, Jeshi la Magereza limefurahishwa na hatua iliyochukuliwa na PPF katika kushirikiana katika uendeshaji wa kiwanda cha viatu Karanga ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwanda kipya na cha kisasa.

“Tutashirikiana kwa karibu ili kuhakikisha azma yetu inatimia kwa haraka,” alisema CP Malisa. Kiwanda cha viatu Karanga, kilichoko kwenye eneo la Gereza la Karanga mjini Moshi, kilizinduliwa na Rais wa awamu ya kwanza, Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Juni 3, 1977 na wateja wakubwa wa bidhaa za kiwanda hicho ni taasisi cha kijeshi, ikiwa ni pamoja na JWTZ, JKT, Magereza na Jeshi la Polisi.
Kamishna wa Magereza, (CP), Editha Malya, aliyemuwakilisha Mkuu wa Jeshi la Magereza Nchini, (CGP), akizungumza wakati wa kikao cha kupeana taarifa na ujumbe wa PPF ulioongozwa na Mkurugenzi Mkuu Erio Oktoba 9, 2016
Bw. Erio, akizungumza wakati wa mkutano huo mfupi kabla ya kukagua maeneo hayo ya ujenzi
Mkurugenzi wa Uwekezaji wa PPF, Steven Alfred, (katikati), akizungumza jambo wakati wa mkutano huo. Kulia ni Meneja Uhusiano wa Mfuko huo, Bi. Lulu Mengele, na kushoto ni Kamishna wa Magereza, Editha Malya
Afisa magereza ambaye ni fundi viatu wa kiwanda cha viatu cha gereza la Karanga, akishona viatu
Bw. Erio, akiongozwa na mama Malya, na maafisa wengine akitembelea kiwanda
Kaimu Mkuu wa Kiwanda cha kutengeneza viatu cha Karanga, Mrakibu Msaidizi wa Magereza, (ASP), Michael Minja, akitoa taarifa ya utendaji wa kiwanda
Mkurugenzi Mkuu wa PPF, Bw. Erio, na Mkurugenzi wa Uwekezaji Bw. Alfred, wakiangalia viatu vilivyotengenezwa kiwandani hapo
Bw. Erio(kushoto), akiangalia moja ya viatu vilivyotengenezwa kiwandani hapo
Mkurugenzi wa Uwekezaji wa PPF, Bw. Steven Alfred, akionyeshwa namna kiatu kinavyotengenezwa, (katikati) ni mwakilishi mkuu wa ofisi ya PPF mkoani Kilimanjaro, Bw. Jacob Cornel Sule
Mkurugenzi Mkuu wa PPF, Bw. Erio, na Mkurugenzi wa Uwekezaji Bw. Alfred, wakiangalia viatu vilivyotengenezwa kiwandani hapo. Kushoto ni Mkuu wa Gereza la Karanga, Kamishna Msaidizi wa Magereza, (ACP), Hassan Bakari Mkwiche
Mkuu wa kitengo cha umeme wa Kiwanda cha viatu Karanga, Staff Surgent, Aulelia Mushi, akziungumzia mahitaji ya umeme kiwandani hapo
Maafisa wa wa Jeshi la Magereza, wakisikiliza mazungumzo hayo
Picha ya Pamoja baada ya kutembelea kiwanda
Ukaguzi wa moja ya maeneo ya ujenzi wa kiwanda
Jiwe la msingi aliloweka Mwalimu Nyerere wakati wa ufunguzi wa kiwanda Juni 3, 1977
Meneja Uhusiano wa PPF, Bi. Lulu Mengele, (watatu kushoto), akiangalia moja ya viatu vinavyotengenezwa kiwandani hapo, Kushoto ni Kamishna wa Magereza, Editha Malya, Mwakilishi Mkuu wa PPF, Mkoani Kilimanjaro, Jacob Cornel Sule, Mkuu wa Magereza mkoani Kilimanjaro, (RPO), Kamishna Msaidizi wa Magereza, Anderson Kamtera, na maafisa wengine
Bw. Erio akisalimiana na Kamishna wa Magereza, Editha Malya

No comments: