Thursday, February 11, 2016

SIRI YA KUPAMBA NYUMBA KWA GHARAMA NAFUU

 
Ukitaka kufanikiwa katika jambo lolote ni muhimu kuwa na mipango iliyoandaliwa. Vilevile katika mapambo ya nyumba mipango ni jambo muhimu. Kama toka awali uliweka mipango ya namna utakavyopamba nyumba yako hii ninayoongelea hapa itakusaidia. Laa haukuweka mpango bado hujachelewa unaweza kuanza leo. 
Mpango ninaozungumzia hapa ni wa rangi ya kuta na sakafu za nyumba toka awali. Ni kwamba kama ukiwa na kuta na sakafu zenye rangi ambazo haziegemei upande wowote, unaweza kubadili muonekano wa chumba chochote kirahisi sana kwa kubadili tu vitupio vya mapambo. Rangi zisizoegemea upande wowote sio lazima tu ziwe jamii ya nyeupe au krimu bali ni rangi zote nyepesi na zilizotulia ambazo ni pamoja na kijivu na bluu bahari. 
 Kama unataka chumba kiwe sehemu ya kupumzikia unatakiwa utumie rangi zilizopoa. Rangi zilizopoa ambazo ni bluu, kijani na zambarau maana yake ni kwamba zikiwa mahali zinaleta hisia ya utulivu. 
Kama una kuta na sakafu zenye hizo rangi tulizosema kuwa haziegemei upande wowote, ukiwa na vitupio vya rangi zilizopoa unabadilisha muonekano kirahisi mno na kwa gharama nafuu sana. Rangi za kuwaka ambazo ni nyekundu, njano na rangi ya chungwa zinaaminiwa kuwa zinaonekana sana na zina nguvu. Unaweza kutumia rangi hizi zenye nguvu kwenye vyumba vya watoto, na kwenye vitupio vya sebuleni kama vile mito, vesi za maua na taa za mezani. 
Kiti kimoja au viwili vyenye rangi za kuwaka vinabadili kabisa muonekano wa sebule. Pia mito mikubwa ya sakafuni ya rangi hizi inaweza kutumika badala ya viti na hivyo kupunguza wingi wa viti sebuleni. 
 Vile vile rangi hizi zenye nguvu unaweza kuzitumia kwenye vyombo vya jikoni kama vile kwenye mabakuli ya kufanya chakula kibaki cha moto, vikombe, glasi na masufuria ya rangi. Kwa upande wa bafuni rangi za kuwaka unaweza kuzitumia kwenue mataulo na vizulia. 
 Kwa hivyo kuendana na tamanio lako unaweza kuwa na vitupio vya rangi zilizopoa au za kuwaka kwa kadri unavyotaka chumba kiwe, au vileviile unaweza kuchanganya vya rangi za jamii zote mbili ili kuweka fenicha zako maridadi na hai.
Unachopaswa tu ni kuangalia hitaji la chumba husika. Ukiwa na kuta na sakafu za rangi zisizoengemea upande wowote ni rahisi mno kutumia vitupio kubadilisha muonekano wa chumba 
kabisa. Pamoja na hayo niliyosema bado kuna baadhi ya vitu unatakiwa kukum buka. Cha kwanza ni kwamba kwenye chumba kidogo, “vingi ni vidogo”. 
Maana ya msemo vingi ni vidogo ni nini? 
Ni kwamba utakavyoweka vitupio vingi kwenye chumba kidogo matokeo yake ni chumba kuonekana kidogo zaidi.Kiweke kitulie usikijaze vitu ili kuepuka kuzidi kuonekana kidogo. 
Halafu, kama una nyumba ndogo weka vitupio vya rangi za kuendana nyumba nzima. Utakachopochanganyachanganya sana nyumba itaonekana kuwa na mhemko na itazidi kuonekana ndogo.
Mwisho, katika kila chumba kwenye nyumba yako muonekano wako unatakiwa ukutambulishe. 
Unaweza kuwa na chumba au nyumba nzuri sana hapa Tanzania lakini kama haitaendana na muonekano au staili yako hautaifurahia. Kama huna uhakika juu ya namna vitupio vyako vya rangi vitakavyoonekana ndani ya chumba, anza kidogokidogo na ongeza vitu taratibu. 
Ukishazijua rangi hizi kama nilivyoainisha wala haitakupa shida na hakika nyumba yako itavutia. Kanuni kuu ni kutengeneza mapambo ya nyumba ambayo wewe na familia yako mtafurahia kuishi humo. 
 Makala hii imeandikwa na Vivi Machange ambaye ni mshauri wa mapambo ya nyumba. Maoni au mawasiliano simu ni 0755 200023 pia tembelea www.vivimachange.blogspot.com

No comments: