Wednesday, February 10, 2016

Serikali yasisitiza kuendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi nchini

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango akiongea na wafanyabiashara nchini jijini Dar es salaam kuhusu Serikali inavyoshirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi wa nchi ili kuweza kuwahudumia wananchi katika kupata huduma za jamii.
Naibu Waziri Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji (kulia) akiwa katika mkutano wa wafanyabiashara nchini jijini Dar es salaam kuhusu Serikali inavyoshirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi wa nchi ili kuweza kuwahudumia wananchi katika kupata huduma za jamii. Kushoto ni Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Alfayo Kidata.
Makamu Mwenyekiti wa TPSF Salum Shamte (kushoto) akisisitiza jambo wakati wa mkutano wa Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango na wafanyabiashara nchini kuhusu Serikali inavyoshirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi wa nchi ili kuweza kuwahudumia wananchi katika kupata huduma za jamii. Katikati ni Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango na kushoto ni Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Servacius Likwelile.
Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Dkt Reginald Mengi (kushoto) akiteta jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF Godfrey Simbeye (kulia) wakiwa katika mkutano wa wafanyabiashara nchini jijini Dar es salaam kuhusu Serikali inavyoshirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi wa nchi ili kuweza kuwahudumia wananchi katika kupata huduma za jamii.
Baadhi ya wafanyabiashara wakiwa katika mkutano wa wafanyabiashara nchini jijini Dar es salaam kuhusu Serikali inavyoshirikiana na sekta binafsi katika kuinua uchumi wa nchi ili kuweza kuwahudumia wananchi katika kupata huduma za jamii. (Picha na Eleuteri Mangi-MAELEZO)

Na Eleuteri Mangi-MAELEZO

Serikali imesema dhamira yake ya kujenga uchumi wa viwanda nchini imejengwa kupitia maeneo ya vipaumbele ambayo yataanza kutekelezwa katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa kutumia malighafi zipatikana nchini ikiwemo mzao ya misitu, kilimo, uvuvi na madini ili kuwahudumia wananchi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango alipokuwa akiongea na wafanyabiashara nchini jijini Dar es salaam.

Dkt. Mpango aliyaeleza maeneo hayo ya vipaumbele ambayo yataanza kutekelezwa katika bajeti hiyo ni pamoja na kuvirudisha viwanda vilivyobinafsishwa na kutafuta wabia ambao wanaweza kufanyakazi iliyodhamiriwa.

Maeneo mengine ni miradi mikubwa ya kielelezo ambalo wataalam wanalifanyiakazi ili kuweza kupata matokeo makubwa, akitolea mfano Dkt. Mpango alisemas kuwa yapo maeneo maalum ya kibiashara yakiwemo Bagamoyo, Kigoma na Mtwara kutokana na maliasili iliyopo hapo.

Zaidi ya hayo, Dkt. Mpango aliongeza kuwa ujenzi wa kiwanda cha chuma kwa kutumia malighafi inayozalishwa kwa kutumia chuma kutoka Liganga na Mchuchuma itakuwa ni msingi wa viwanda mama ikizingatiwa “Hakuna ujenzi usiohitaji chuma”.

Katika suala la ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha Kimataifa, Dkt. Mpango alisema kuwa mradi huo ni muhimu kwa lengo la kusukuma mbele sekta ya usafirishaji ndani na nje ya nchi ikwemo nchi za Rwanda, Burundi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na mataifa mengine.

Mafanikio ya ujenzi wa viwanda nchini yanawezekana kwa kwa kuwa Serikali imedhamiria kushirikiana na serkta binafsi kwa kuwa maendeleo ya viwanda yanapaswa kuendana na maendeleo ya watu kwa kuwapatia ajira, elimu inayoendana na mahitaji ya viwanda ili maisha ya wananchi yawe bora zaidi.

Aidha, ili kujenga uwezo wa kuwa na viwanda nchini, Serikali imejipanga kukusanya kodi ambayo ndiyo msingi wa kuwa na uchumi imara utakaosaidia nchi kujiendesha ambapo wafanyabiashara wote nchini wanapaswa kujisajili na kupewa namba ya usajili (TIN) huduma ambayo inapatikana nchi nzima kupitia ofisi za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Katika mkutana huo, Dkt. Mpango amewaasa wafanyabiashara kutunza kumbukumbu za biashara yao ili kuwa na kumbukumbu ambazo zinatoa taarifa sahihi na kuhimiza wafanyabiashara wenye mashine za kielekroniki (EFD) waendelee kuzitumia wanapouza bidhaa zao na kuwaptia risiti wateja wao, kwa wale wasio na mashine hizo, Serikali inaendelea kutekeleza agizo la Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli la kuwapatia mashine hizo.

Vile vile, Dkt. Mpango ametoa namba za simu za ofisi za TRA kitengo cha Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi ambapo wananchi wanaweza kuwasiliana moja kwa moja na Idara ya Mambo ya Ndani TRA juu ya maadili ya watumishi wa mamlaka hiyo nchi nzima kwa namba 0689122515 na kutuma ujumbe mfupi kwa namba 0689122516.

Aidha, Dkt. Mpango amewaonya wafanyabiashara ambao sio waaminifu waache kufanyabiashara za magendo ambapo ameainisha baadhi ya maeneo yanayotumiwa ni pamoja na mwambao wa bahari ya Hindi maeneo ya Mbweni, ziwa Victoria na ziwa Tanganyika.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati na Sera TPSF Felix Mosha  amesema kuwa Sekta binafsi itaendelea kushirikiana na Serikali katika mpango wa kukuza uchumi wa nchi na kumhakikishia  Waziri wa Fedha na Mipango kuwa watatimiza wajibu wao wa kulipa kodi na kuhamasisha wafanyabiashara wote nchini wanakwenda pamoja na Sera ya “Hapa Kazi Tu”.

No comments: