Tuesday, December 22, 2015

KIGWANGWALLA ATEMBELEA UJENZI WA HOSPITALI YA RUFAA KANDA YA KUSINI


Mganga Mkuu wa Hospitali ya Ligula ya mkoa wa Mtwara, Dkt. Shaibu Maarifa (katikati) akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, Dkt. Hamisi Kigwangalla (kushoto) alipotembelea eneo la Mikindani inapojengwa hospitali ya mpya ya kanda ya kusini, mkoani Mtwara.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, Dkt. Hamisi Kigwangalla (kushoto) akimuuliza swali Mganga Mkuu wa Hospitali ya Ligula ya mkoa wa Mtwara Dkt. Shaibu Maarifa (katikati) wakiwa eneo la Mikindani inapojengwa hospitali ya mpya ya kanda ya kusini, mkoani Mtwara.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, Dkt. Hamisi Kigwangalla (katikati) akipata maelezo kutoka kwa Mganga Mkuu wa Hospitali ya Ligula ya mkoa wa Mtwara, Dkt. Shaibu Maarifa (kushoto) inapojengwa hospitali ya mpya ya kanda ya kusini inayojengwa eneo la Mikindani mkoani Mtwara. 
Muonekano wa moja ya majengo ya Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kusini itakayohudumia mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma inayojengwa eneo la Mikindani mkoani Mtwara.(Picha na Eleuteri Mangi- MAELEZO).

Na Mwandishi wetu, Mtwara

UJENZI wa hospitali ya rufaa Kanda ya Kusini, unaofanyika mkoani Mtwara sasa upo katika majengo ya wagonjwa wa nje (OPD).

Ujenzi huo ulioanza mwaka 2009 kwa kusafishwa kwa eneo na kujengwa kwa uzio wa kilomita 2.7 mwaka 2011 kwa gharama ya shilingi milioni 840 na kuanza kujengwa kwa majengo ya OPD mwaka 2013 umelenga kuwezesha mikoa ya Kusini kuwa na hospitali kubwa yenye hadhi ya kisasa.

Akisoma taarifa ya maendeleo ya ujenzi kwa Naibu Waziri katika wWizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee Dkt. Hamisi Kigwangalla, Mganga Mkuu wa mkoa wa Mtwara alisema kwamba ujenzi wa mapokezi umetarajiwa kutumia shbilioni 4.8 na hadi sasa wametumia bilioni 1.8

Mganga huyo alisema mradi mzima unatarajiwa kujengwa kwa bilioni 78.

Alisema kuchelewa kuendelea japo sasa wana ghorofa 2 zilizoezekwa na wanapiga ripu kunatokana na upatikanaji wa fedha kutoka serikali kuu.

Alisema hospitali hiyo ni muhimu sana kukamilika kutokana na kukua kwa uchumi wa Mtwara na mikoa jirani na pia kuwapo kwa uhitaji kwa mikoa ya kaskazini mwa nchi jirani.

Naye Naibu Waziri Kigwangwalla alisema kwamba ni matumaini yake kuwa hospitali hiyo itakamilika mapema na kubakiza changamoto za matumizi ya wananchi kutoka nchi jirani ambao kwa sasa wanafaidika sana na hospitali ya Ligula.

Alisema wataalamu wanatakiwa kuangalia hali hiyo ili kuwepo na matumizi sahihi ya miundombinu hiyo iliyolenga kufaidisha wananchi wa Tanzania.

Aidha akiwa Mtwara Naibu Waziri huyo aliendelea kusisitiza watumishi wote kuwajibika na kuwahi maeneo yao ya kazi.

Alisema watumishi wa umma wanaofikia laki nne wamepata nafasi adimu ya kuutumikia umma wa watu takribani milioni 50 na hivyo ni lazima waheshimu watanzania kwa kuwatumikia ipasavyo.

Alisema wao waliomba nafasi ya kuhudumia watanzania kwa hiyo ni lazima wawahudumie watanzania na kila mmoja katika kitengo chake ni lazima kuhakikisha watumishi wanafanya kile walichoahidi katika mikataba yao.

No comments: