Thursday, July 2, 2015

MAFUNDI SANIFU (TEMESA) WAFUNDWA KUHUSU USIMAMIZI NA UKAGUZI WA MAZINGIRA, MOROGORO

Mkurugenzi wa Idara ya Tathmini ya Athari ya Mazingira kutoka Baraza la Taifa la kuhifadhi Mazingira (NEMC), Eng. Ignance Mchallo akielezea kuhusu Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004 kwa mafundi sanifu wa Wakala wa Ufundi na Umeme TEMESA.
Mafundi Sanifu wakifanya tathmini na ukaguzi wa mazingira katika karakana ya TEMESA mjini Morogoro wakati wakiwa katika mafunzo ya tathmini, usimamizi na ukaguzi wa mazingira.
Ofisa Manunuzi wa Wizara ya Ujenzi, Bw. Shukuru Sikunjema akipokea cheti kutoka kwa Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Usalama na Mazingira kutoka Wizara ya Ujenzi, Eng. Melania Sangeu baada ya kuhitimu mafunzo ya tathmini, usimamizi na ukaguzi wa mazingira yaliyofanyika mkoani Morogoro.
Mgeni rasmi Bw. Melkizedeck Mlyapatali ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Ujenzi, Morogoro akiwa na wahitimu wa mafunzo ya tathmini, usimamizi na ukaguzi wa mazingira kwa mafundi sanifu wa TEMESA, kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania mjini Morogoro.

Mafundi sanifu wa Wakala wa Umeme na Ufundi (TEMESA), kutoka mikoa mbalimbali nchini wameaswa juu ya umuhimu wa tathmini, usimamizi na ukaguzi wa mazingira  katika maeneo  yao ya kazi ili kuweza kudhibiti athari za mazingira zinazowakabili na kusababisha mabadiliko ya tabia nchi.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Idara ya Tathmini ya Athari ya Mazingira kutoka Baraza la Taifa la kuhifadhi Mazingira (NEMC), Eng. Ignance Mchallo wakati wa mafunzo ya tathmini na usimamizi wa mazingira kwa mafundi sanifu yaliyofanyika mkoani Morogoro.

Aidha amewataka mafundi hao kutumia sheria ya mazingira ya mwaka 2004 kwa kuwa sheria hiyo si tu kulinda haki peke yake bali pia kuondoa vikwazo, kutoa mwongozo wa utendaji na kupunguza mzigo wa kiutendaji, pamoja na kuboresha uwajibikaji na ufanisi kwa ajili ya maendeleo endelevu ya nchi.

“Sheria ya mazingira ni sheria mama ya mazingira na yenye nguvu katika utekelezaji, na pia inaweza ikawa juu ya sheria nyingine pindi matatizo yanapojitokeza. Ni haki kwa kila mtu kuishi katika mazingira salama na safi, endapo mazingira yakaharibiwa unayo haki ya kuitumia sheria hii kwa kushtaki ukiukwaji wa utunzaji wa mazingira eneo husika”, alisisitiza Mkurugenzi Mchallo.

Mkurugenzi Mchallo aliongezea kuwa Sheria ya mazingira inahitajika kuzingatiwa na kutekelezwa na watu wote hususan wafanyakazi katika maeneo yao ya kazi ili kuhakikisha wanaboresha afya zao na kuweza kufanya kazi kwa ufanisi zaidi na manufaa ya Taifa kwa ujumla.  

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Usalama na Mazingira kutoka Wizara ya Ujenzi, Eng. Melania Sangeu amewataka mafundi sanifu hao kuzingatia mafunzo hayo na kutathimini mazingira katika maeneo wanayofanyia kazi kwa kuwa lengo ni kujenga uelewa wa masuala ya mazingira pamoja na mbinu za kufanya tathmini ya mazingira na utekelezaji wake.

“Mazingira salama ndiyo chachu ya ufanisi mzuri wa kazi, hivyo basi maeneo yenu ya kazi yawe katika mazingira safi kwa kufuata utunzaji mzuri wa mazingira unaotakiwa pamoja na kutengwa maeneo sahihi ya kumwaga mafuta machafu ya magari, maeneo ya kuchomea taka, mpangilio mzuri wa vifaa vya kufanyia kazi, na kuwa na vifaa vya kutosha vya usalama pamoja na kufahamu namna na wakati wa kuvitumia”, alisema Eng. Sangeu.

Kwa upande wake, Mhadhiri wa Taasisi ya Ufundi Dar es Salaam (DIT), Eng. Kinyawa Kirama ameipongeza Wizara ya Ujenzi kwa jitihada zake za kutambua umuhimu wa mazingira ambapo amesema kupitia mafunzo hayo mafundi sanifu hao watakuwa mfano kwa wengine katika masuala ya usimamizi na utunzaji wa mazingira katika maeneo yao ya kazi.

“Mkirudi katika karakana zenu mtathmini na kuangalia ni aina gani ya uharibifu wa mazingira ambao umekuwa ukifanyika na kutafuta mbinu zakufanya ili msiendelee kuharibu mazingira pamoja na kujikinga dhidi ya magonjwa na matatizo yanayoweza kuibuka kutokana na ukiukwaji huo”, alisema Eng. Kinyawa.

Ameongezea kuwa kumekuwa na tabia ya kutokuwa makini juu ya suala la mazingira katika maeneo yetu ya kazi na hivyo kusababisha ukiukwaji na uharibifu wa mazingira ambao athari zake ni kubwa na nyingine kushindwa kuzuilika.

Wito umetolewa kwa taasisi na makampuni mengine kuweka mifumo mizuri ya kutathimini na kusimamia utunzaji wa mazingira pamoja na ushirikishwaji kwa watu wote hasa katika sekta ya nishati ya umeme, kilimo, miundombinu ya barabara pamoja na afya, ili kupunguza athari za mazingira yanayopelekea mabadiliko ya tabia nchi.

No comments: