Tuesday, January 27, 2015

Mama wa Mapacha sita anunuliwa nyumba

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Covenant Bank Balozi, Salome Sijaona(Katikati) akikata utepe, kuashilia uzinduzi Rasmi wa nyumba aliyokabidhiwa Salome Mhando ambaye alitelekezwa na mume wake baada ya kujifungua watoto mapacha mfurulizo hadi kufikia sita na kukosa Mahali pa kuishi, Covenant Bank imemkabidhi nyumba hiyo ambayo ataimiliki yeye mwenyewe pamoja na thamani za ndani na Bima ya Matibabu kwa Mwaka mzima. Anaeshuhudia ni mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Sabetha Mwambenja (wa kwanza kushoto) na Salome Mhando (wa kwanza kulia).
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Covenant Bank Balozi, Salome Sijaona (kushoto), Pamoja na Mkurugenzi wa benki Hiyo, Sabetha Mwambenja, wakimkabidhi hati ya kiwanja na Umiliki wa nyumba Salome Mhando, Mama alietelekezwa na mume wake baada ya kujifungua watoto mapacha mfurulizo, hadi kufikia sita, Benki hiyo imemkabidhi nyumba hiyo pamoja na Bima ya Matibabu kwa mwaka mzima.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Covenant Bank Balozi, Salome Sijaona(Katikati) akiwapokea watoto wa Salome Mhando wakati akiwasili kukabidhiwa nyumba yake. Pamoja nae ni Mkurugenzi Mtendaji wa Covenant Bank, Sabetha Mwambenja na Mjumbe wa Bodi ya benki hiyo, Margaret Kyarwenda.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Covenant Bank Balozi, Salome Sijaona (wa kwanza kulia) pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Covenant Bank, Sabetha Mwambenja na Mama Salome Sijaona, Wakimfurahia moja wa watoto wa mama huyo akipanda katika moja ya vitanda walivyokabidhiwa.

Baada ya kujifungua watoto mapacha mfululizo na kufuatiwa na kitendo cha kutelekezwa na mume wake huku akiwa hana sehemu ya kuishi, Hatimaye  Salome Muhando amenunuliwa na kukabidhiwa nyumba na Covenant Bank ambayo ataishi yeye na watoto wake.

 Salome , mwenye watoto sita mapacha alitelekezwa na mume wake baada ya kujifungua mapacha mara tatu mfululizo na kusababisha  kukosa sehemu maalum ya kukaa yeye pamoja na watoto wake ambapo baada ya kutelekezwa msamaria mwema alijitolea kumhifadhi katika shamba lake lililopo eneo la Mabwepande.

Baada ya kusikia kilio cha mama huyo kupitia vyombo vya habari Covenant Bank, ilijitolea kumnunulia nyumba mama huyo ambayo ataimiliki yeye moja kwa moja na kumpatia mtaji wa biashara ambao utamsaidia kuenesha maisha yake ya kila siku.

Akizungumza na waandishi wa habari, punde baada ya kukabidhi nyumba hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki hiyo Balozi, Salome Sijaona, amesema baada ya kuona mateso ambayo mwanamke huyo  amekuwa akiyapata kwa kukosa makazi , Chakula na mahitaji mengine ya kibinaadamu waliona ni vyema benki yake kujitolea kumsaidia ikiwa ni katika sehemu moja ya kutimiza majukumu yake ndani ya jamii.

“Tumeguswa sana na mateso ambayo amekuwa akiyapata Bi. Salome Mhando, yeye pamoja na watoto wake baada ya kutelekezwa na mume wake kwa kigezo ha kuzaa watoto mapacha mfurulizo, tuliguswa na kuamua kujitolea kumnunulia nyumba ambayo ataimiliki yeye mwenyewe.” Alisema Balozi, Sijaona na kuongeza kuwa.

“Nyumba hii tumemkabidhi pamoja na samani za ndani ya nyumba ambazo zitamuwezesha sasa kuishi maisha ya amani, na furaha akiwa kama wanawake wengine na kufurahi pamoja na watoto wake.”

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Sabetha Mwambenja amesema kuwa pamoja na kumkabidhi nyumba mama huyo pia Benki hiyo, imempatia Bima ya Matibabu kutoka AAR ambayo itamsaidia kupata Matibabu yeye pamoja na watoto wake wote.

“Pamoja na kumpatia nyumba Salome  pia tunampatia Bima ya Matibabu ambayo itamuwezesha yeye na watoto wote kutibiwa katiba Hopitali zote zilizo mahali popote nchini, Tuna uhakika sasa atakuwa na uhakika wa afya yake na watoto wake katika kipindi chote hivyo atakuwa na nafasi ya kufanya shughuli zake za uzalishaji kwa amani., Alisema Mkurugenzi huyo.

Kwa Upande wake Salome , aliwashukuru Covenant Bank kwa kujitolea kumsaidia na sasa ana uhakika wa maisha yeye pamoja na watoto wake.
“Ninawashukuru sana Benki ya Covenant kuniwezesha kumiliki nyumba yangu ninawashukuru sana na ninaomba waendelee na moyo huo wa kuwasaidia kina mama wenye matatizo kama haya kwa sababu siko peke yangu,” alisema  na kuongeza,

“Kina mama tumekuwa na wakati mgumu sana katika ndoa zetu hususai katika masuala ya uzazi, Ninawashukuru watu wote ambao walijitolea kunisaidia chakula na nguo katika wakati wote ambao nilikuwa sina sehemu maalum ya kukaa, hadi sasa ninamiliki nyumba yangu. Alihitimisha Salome.

1 comment:

Unknown said...

Haya ni mahendeleo na mfano mzuri kwa Tanzania siyo kwa mashirika ya makubwa kwa madogo mkitoa michango kama hii Tanzania tutafika mbali sana.Tuwe na moyo wa kuwasadia watanzania wenzetu especial kinamama na watoto.HONGERA SANA KWA BENKI YA COVENANT.
''Give back to the people''Tuwe na moyo huo watanzania