Saturday, November 22, 2014

Chuo IRDP Dodoma chaadhimisha mahali ya 28 kwa mafanikio.

Mkuu wa kwanza wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) Askofu Dkt. Saimon Chiwanga akitoa neno baada ya Mgeni Rasmi Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene kumaliza shudhuli ya kutunuku vyeti kwa wahitimu wakati wa mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) iliyofanyika jana mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene akitoa hotuba kwa niaba ya Waziri wa Fedha Saada Mkuya Salum wakati wa mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) iliyofanyika jana mjini Dodoma.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene akimtukuku Shahada ya Uzamili katika Uchumi wa Maendeleo Amina Salum Mwanja wakati wa mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) iliyofanyika jana mjini Dodoma.
Baadhi ya wahitimu wa mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) iliyofanyika jana mjini Dodoma.
Mwanafunzi wa mwaka wa pili anayesomea Shahada ya kwanza ya Mipango ya Usimamizi wa Mazingira katika Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) Azizi Mshau akimweleza Mgeni Rasmi Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene namna bora ya kundaa mipango miji inayokuwa rafiki kwa mazingira.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene akiagana na Mkuu wa kwanza wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) Askofu Dkt. Saimon Chiwanga mara baada ya sherehe ya mahafali ya 28 ya Chuo hicho.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene () akiwa katika picha ya pamoja na wahadhiri wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) mara baada ya mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) iliyofanyika jana mjini Dodoma. (Picha zote na Eleuteri Mangi- Dodoma)

Na Eleuteri Mangi- Dodoma
Serikali imesema  inaendelea kushirikiana na sekta binafsi kuweka mazingira rafiki kwa kuboresha mifumo ya ajira katika sekta ya umma na ile ya binafsi ili kujenga uchumi wa kisasa unaozalisha ajira pamoja na kuwawezesha vijana wasomi nchini kujiajiri.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara Janet Mbene kwa niaba ya Waziri wa Fedha Saada Mkuya Salum wakati wa mahafali ya 28 ya Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini (IRDP) yaliyofanyika jana mjini Dodoma.

“Ninafarijika sana kusikia vijana wa chuo cha Mipango ya Maendeleo Vjijini wameweza kuonesha njia kwa kuweka kwa vitendo waliyojifunza kwa kuanzisha miradi ya kiuchumi katika sekta ya kilimo kama njia ya kujiajiri” alisema Mbene.

Naibu Waziri huyo aliwahakikishia vijana hao kuwa Serikali ipo tayari kusaidia juhudi hizo kupitia fursa mbalimbali za kuwasaidia vijana na wajasiriamali kupitia fursa zinazoendelea kutolewa na Serikali.

Naibu Waziri Mbene alisema kuwa ili kutekeleza lengo hilo, Serikali inaendelea kuhamasisha uwekezaji katika kilimo, uchimbaji wa madini na uwezo wa kuongeza thamani mazao yetu yanayozalishwa.

Mbene aliongeza kuwa maeneo yote hayo yanatoa fursa nyingi kwa wahitimu vijana nchini kuajiriwa katika ngazi mbalimbali za Serikali, sekta binafsi na kujiajiri.

Akimkaribisha Mgeni rasmi kwenye mahafali hayo, Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo Dkt. Razack Lokina alitoa kilio cha chuo hicho cha kuomba kada ya mipango kupewa nafasi stahili katika mfumo wa ajira Serikalini.

Akifafanua suala hilo Dkt. Razack alisema kuwa kukosekana kwa kada ya Mipango kumesababisha kazi za kada hiyo kutotekelezwa ipasavyo kwa kiwango cha ufanisi unaotakiwa. 

Aidha, Dkt. Razack alisema kuwa taaluma ya Mipango inamtayarisha Afisa Mipango ambaye jukumu lake ni kubuni, kupanga, kufuatilia, kutathmini, kuratibu shughuli na rasilimali katika maeneo ya Mipango ili kufikia malengo ya maendeleo ya jamii kusudiwa tofauti na taaluma ya Uchumi ambayo inamuandaa Afisa kuwa na jukumu mahususi la kuchambua ili kutoa hali halisi ya mazingira ya kiuchumi kisekta.

Kwa upande wake Chuo hicho Constantine Lifuliro alisema kuwa wahitimu wa chuo chake wameandaliwa vya kutosha wapo tayari kutoa huduma katika nyanja mbalimbali kwenye maeneo waliyojifunza hasa katika kuandaa, kusimamia, kutekeleza, kufuatilia na kutathmini mipango ya maendeleo katika maeneo mbalimbali  watakayofanyia kazi.

Naye mhitimu Baltazar Ngeze, kwa niaba ya wahitimu wa mwaka huu wa chuo hicho aliushukuru uongozi wa chuo kwa kuwaandaa vema kwenda kutekeleza majukumu yao ya taaluma ya Mipango katika jamii watakayokuwepo.

Katika mahafali hayo jumla ya wahitimu 1,909 waliotunukiwa tuzo zao katika kozi mbalimbali zinazotolewa chuoni hapo.

Kati ya wahitimu hao, wapo wanaume ambao idadi yao ni 1,003 sawa na asilimia 52 ya wahitimu wote na wanawake idadi yao ikiwa ni 906 sawa na asilimia 48 ya wahitimu wote.

Idadi hiyo ya wahitimu wa mwaka huu inaonesha wameongezeka wahitimu 63 sawa na silimia 3.4 zaidi ya wale waliohitimu masomo yao mwaka jana 2012/2013 ambao walikuwa 1,846 kati yao wakiwa wanaume 1,037 sawa na asilimia 56 na wanawake walikuwa 809 sawa na asilimia 44.

No comments: