Friday, April 25, 2014

MAZUNGUMZO NJIA PEKEE YA KUREJESHA AMANI YA KUDUMU DARFUR - GEN-MELLA

Jenerali Mella, Kamanda wa Jeshi la UNAMID akibadilisha mawazo na Balozi Mwinyi, ambapo pamoja na mambo mengine, amesema wanajeshi kutoka JWTZ ambao ni sehemu ya UNAMID wameendelea kuonesha weledi na kujituma kwa hali ya juu katika eneo la ulinzi wa amani, ulinzi wa raia na usimamiaji wa misaada ya kibinadamu. Akasema kutokana na mapingano ya kikabili yanajitokeza mara kwa mara, na kuwa sehemu kubwa ya mapigano hayo yamekuwa yakitokea katika maeneo zilipo kambi za wanajeshi kutoka Tanzania, wanajeshi wetu wamejikuta wakilazimika kutoa huduma mbalimbali zikiwamo za kuwazalisha wanawake waja wazito. Utoaji wa huduma hiyo ya uzazi salama nje ya mamlaka yao imewafanya wazazi waliojifungua kuwapatia majina ya kitanzania watoto wao, kama shukrani yao kwa madaktari hao wa kitanzania kwa kuokoa maisha yao na ya watoto wao. Kushoto kwa Jenerali Mella, ni Luteni Kanali, Wilbert Ibuge, Mwambata Jeshi katika Uwakilishi wa Kudumu
Luteni Jenerali Paul Mella, Kamanda wa Jeshi la Mseto la Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa katika Darfur ( UNAMID) akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Balozi Ramadhan Mwinyi, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa ( hayupo pichani). Jenerali Mella alifika katika Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania kufuatia ziara yake ya kikazi ya siku tatu katika Umoja wa Mataifa ambapo alikuwa na mazungumzo na Wakuu mbalimbali wa UN. Akielezea tathmini yake ya miezi nane kama Kamanda wa UNAMID Jenerali Mella anasema njia pekee ya kupatikana kwa amani ya kudumu katika jimbo la Darfur ni kwa pande zinazopingana kukaa katika meza ya mazungumzo na kumaliza tofauti zao.

Na Mwandishi Maalum

Kamanda wa Jeshi la Mseto la Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa katika Darfur ( UNAMID) Luteni Jenerali Paul Mella, amesema, mazungumzo yatakayozihusisha pande zote zinazopingana katika mgogoro na machafuko yanayoendelea katika Jimbo la Darfur ndiyo suluhu pekee inayoweza kurejesha hali ya Amani, usalama na utulivu katika jimbo hilo.

Jenerali Mella, ameyasema hayo wakati alipokuwa akibadilishana mawazo na Balozi Ramadhani Mwinyi, Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, wakati Jenerali Mella alipoutembelea Uwakilishi wa Kudumu.

Kamanda wa Jeshi la UNAMID alikuwa hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kwa ziara ya kikazi ya siku tatu, ambapo alikutana na kufanya mazungumzo na Viongozi mbalimbali wa Umoja wa Mataifa.

“Katika kipindi changu za miezi nane sasa kama kamanda wa UNAMID yapo mambo mengi ambayo nimejifunza zikiwamo pia changamoto mbalimbali katika eneo zima la ulinzi wa Amani katika Jimbo la Darfur. Kubwa la msingi ambalo nimejifunza, ni kwamba, Amani ya kudumu haiwezi kurejea katika jimbo la Darfur kama pande zote zinazopingana hazitaweza kukaa katika meza moja na kufanya mazungumzo” anasema Jenerali Mella.

Na kuongeza “ kwa tathmini yangu , wanajeshi wanaounda UNAMID wapo pale kulinda Amani, kutoa ulinzi kwa wananchi na kusaidia usambazaji wa misaada ya kibinadamu. Lakini kwa kweli, hakuna Amani ya kulinda, kwa sababu moja kubwa, nayo ni kwamba pande zinazopingana hazijafikia makubaliano ya kusitisha mapigano na kurejea katika meza ya mazungumzo.”

Akielezea zaidi tathmini yake katika kipindi hicho ya miezi nane ambapo anaongoza zaidi ya walinzi wa Amani (wanajeshi)14,379 wanaounda UNAMID. Jenerali Mella, anaeleza kwamba, tangu achukue uongozi huo, kumekuwapo na mabadiliko katika mwenendo mzima wa mapigano katika jimbo hilo.

“ Changamoto kubwa niliyokumbana nayo ni kuwa katika miezi hiyo nane ya uongozi wangu, mwenendo mzima wa machafuko au mapingano umebadilika na kujikita zaidi katika mapigano ya kikabila” anabainisha na kuongeza.

“Mapigano hayo ya kikabili na ambayo chimbuko lake ni kugombea raslimali zikiwamo dhahabu mafuta na malisho, yamepelekea kuwapo kwa wimbi kubwa la wakimbizi wa ndani.

Jenerali Mella anasema, sehemu kubwa ya mapingano hiyo baina ya makabila yalikuwa yanatokea karibu na maeneo zilipo kambi zetu kwa maana ya wanajeshi kutoka Jeshi la wananchi wa Tanzania ( JWTZ). Ninafarijika sana kueleza kwamba wanajeshi wetu wameonyesha weledi na uhodari wa hali ya juu kwanza kwa kutoa ulinzi kwa raia waliokuwa wakikimbia machafuko na pili kuwapatia misaada ya kibinadamu zikiwamo huduma za afya”.

“Ni katika kipindi hicho cha mapigano ambapo licha ya utoaji wa huduma za kibinadamu kwa wakimbizi hao, walinzi wetu wa Amani ( JWTZ), walijikuta wakilazimika kutoa huduma za dharura kwa akina mama wajawazito zaidi ya saba waliojifungua salama watoto wao katika kambi zetu”.

“ Huduma hii ya kuwasaidia akina mama wajawazito kujifungua salama watoto wao, kuliwafanya wazazi wale kuwapa watoto wao majina ya kitanzania kama shukrani yao kwa msaada na huduma nzuri waliyopatiwa na madaktari wa kitanzania katika kipindi hicho kigumu. Kuna watoto wenye majina ya kitanzania” anasema Jenerali Mella kwa furaha.

Kwa upande wake, Balozi Mwinyi ameshukuru Kamanda wa Jeshi la UNAMID kwa kutenga muda wake na kufika Uwakilishi wa Kudumu. Akashukuru pia kwa maelezo yake ya kina kuhusu hali ilivyo katika jimbo hilo la Darfur na mchango mzima wa walinzi wa Amani.

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ina kikosi UNAMID kinacho kalia maeneo matatu ambayo ni Khor Abeche, Menawashe na Shangil Tobaya.

Tanzania inakuwa nchi ya tatu kongoza UNAMID , nchi nyingine ambazo zimewahi kuongoza ni Nigeria na Rwanda.

No comments: