Wednesday, August 28, 2013

AZIMIO LA BUNGE LA KUMPONGEZA MHESHIMIWA MHE. ANNE SEMAMBA MAKINDA (MB), SPIKA WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWA KUCHAGULIWA KUWA RAIS WA CHAMA CHA JUMUIYA YA MABUNGE YA NCHI WANACHAMA WA JUMUIYA YA MADOLA AFRIKA


[Limetolewa kwa mujibu wa Kanuni 53(1) na (2) ya Kanuni                             
za Kudumu za Bunge 2013]
_____________

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 17 - 27 Julai, 2013 ulifanyika Mkutano wa 44 wa Chama cha Mabunge ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola Afrika [Commonwealth Parliamentary Association (CPA)] uliofanyika Windhoek, Namibia na Bunge letu liliwakilishwa na Wabunge wafuatao:-
1.     Mhe. Anne Semamba Makinda, Mb, - Spika;
2.     Mhe. Mussa Azzan Zungu, Mb. - Mwenyekiti wa CPA Tawi la Tanzania;
3.     Mhe. Beatrice Matumbo Shellukindo, Mb - Makamu Mwenyekiti wa CWP Kanda ya Afrika Mashariki;
4.     Mhe. Kabwe Zubeir Zitto, Mb. – Mwakilishi wa Tawi na Mjumbe Kamati ya Mipango na Fedha;
5.     Mhe. Magalle John Shibuda, Mb;
6.     Mhe. Dkt Maua Abeid Daftari, Mb;
7.     Mhe. Magdalena Hamis Sakaya, Mb; na
8.     Mhe. Mhonga Said Ruhwanya, Mb.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mengine, katika Mkutano huo ambao lengo lake kuu lilikuwa ni kujadiliana na kuona namna gani nchi wanachama wanaweza kutumia umoja wao katika kutatua migogoro, pamoja na kustawisha maendeleo ya kiuchumi Barani Afrika, [Utilizing our Commonwealth partnership to promote Conflict Resolution and Econimic Development on the African Continent] kulikuwa na jukumu kubwa na zito la kumchagua Rais wa chama hiki atakayekuwa kiongozi wa nchi 19 na matawi 45 ya Afrika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua uwezo na sifa za viongozi wa Tanzania, Tawi la CPA Tanzania lilipendekeza jina na Mheshimiwa Anne S. Makinda (Mb), Spika kuwa mgombea wa nafasi hii, kwa kuamini kuwa ni mwadilifu, mwenye uzoefu wa kutosha  na  mchapakazi, na hivyo kuwa na sifa stahiki za kugombea nafasi hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada mbalimbali zinazofanywa siku zote na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho kikwete za kuitangaza nchi yetu kimataifa, zilisaidia sana katika mchakato wa kumnadi mgombea wetu kwa wajumbe wa mkutano ambao ndio walikuwa wapiga kura katika uchaguzi huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika uchaguzi huo Mhe Anne Semamba Makinda, Mb alichaguliwa kwa kishindo kuwa Rais wa CPA Kanda ya  Afrika kwa muda wa mwaka mmoja, jambo ambalo limeiletea nchi yetu heshima na  sifa kubwa kimataifa.
Mheshimiwa Naibu Spika,  kwa kutambua jambo hili, natumia fursa hii kuliomba Bunge kama chombo cha uwakilishi wa wananchi kuridhia Azimio la Kumpongeza Mhe Spika kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa CPA Kanda ya Afrika kama ifuatavyo:- 
KWA KUWA, Bunge la Tanzania ni Mwanachana wa Umoja wa Kibunge wa Jumuiya ya Madola [the Commonwealth Parliamentary Association] kwa muda mrefu sasa na imekuwa ikishiriki kikamilifu shughuli za Umoja huo na kutoa fursa sawa za uwakilishi  kwa raia wake wote bila kujali jinsia jambo ambalo limewezesha wanawake wengi kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi Kitaifa na Kimataifa;
NA KWA KUWA, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameonyesha jitihada mbalimbali za kuitangaza nchi nyetu kimataifa jambo ambalo limewezesha fursa nyingi kupatikana;
NA KWA KUWA, katika Mkutano wa 44 wa CPA- Afrika uliofanyika Windhoek, Namibia, Mhe. Anne S. Makinda (Mb), Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alichaguliwa kuwa Rais wa CPA Kanda ya Afrika;
NA KWA KUWA, Mheshimiwa Spika, ana uzoefu wa kutosha katika medani za siasa na uongozi kwa zaidi ya miaka 37, kwa kushika nyadhifa mbalimbali kama vile kuwa Naibu Spika na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Ardhi , Maliasili na Mazingira, Mwenyekiti wa Bunge, Waziri katika Wizara Mbalimbali, Makamu mwenyekiti wa SADC-PF nk jambo ambalo linaondoa shaka ya aina yoyote juu ya uwezo wake;
HIVYO BASI, Bunge hili katika Mkutano wake wa Kumi na Mbili linaazimia kumpongeza Mheshimiwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Anne Semamba Makinda (Mb) kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa Chama cha Mabunge ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola, (Commonwealth Parliamentary Association) kanda ya Afrika, na kwamba linamtakia kila la kheri Mheshimiwa Spika katika kutekeleza majukumu yake haya mapya na mazito kwa kuongoza nchi 19 na matawi 45 Afrika nzima.
          Naomba kutoa hoja.
  
Mussa Azzan Zungu, MB.
MWENYEKITI WA CPA - TANZANIA





No comments: