Friday, June 8, 2018

SERIKALI YASHAURIWA KUJENGA MAHABUSU ZA WATOTO KWENYE MIKOA NA WILAYA HAPA NCHINI





















 Mratibu wa Chama cha Wanasheria Wanawake Mkoani Tanga Latiba Ayoub akizungumza wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo ya siku moja iliyokuwa na lengo la kujaribu kujadili changamoto kwenye sheria za mtoto na kanunuzi zake hususani waliopo kwenye ukinzani nazo wakiwemo kama wadau iliyofanyika mjini hapa .
Mwanasheria wa Chama cha Wanasheria Wanawake Mkoani Tanga (Tawla) Mwanaidi Kombo akizungumza wakati wa warsha hiyo ya siku moja iliyofanyika ukumbi wa YDCP Jijini Tanga
Afisa wa Dawati Jeshi la Magereza mkoani Tanga ASP Halima Mswagilla akichangia jambo kwenye warsha hiyo 
Wakili wa Serikali Rebbeca Msalangi akisisistiza jambo kwenye warsha hiyo wakati akiwasilisha mada 
 Wakifuatilia hoja mbalimbali za wajumbe wa warsha hiyo 
 Sehemu ya washiriki wakiendelea kufuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwang’ombe Jijini Tanga Husna Abdi wa pili kutoka kulia akichukua baadhi ya dondoo kwenye warsha hiyo 




SERIKALI imeshauriwa kujenga mahabusu za watoto kwenye mikoa na wilaya hapa nchini ili kuwaweka watoto waliokuwa katika ukinzani wa kisheria ambao wamekuwa wakifanya vitendo viovu. 

Hatua hiyo itakuwa sehemu ya kuwaweka watoto happy wakiwa wanasubiri kesi zao kusikilizwa badala ya ilivyokuwa hivi sasa watoto hao wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na uhaba uliopo. 

Hayo yalisemwa juzi na Mratibu wa Chama cha Wanasheria wanawake mkoani Tanga (TAWLA) Latifa Ayoub wakati wa warsha ya siku moja iliyokuwa na lengo la kujaribu kujadili changamoto kwenye sheria za mtoto na kanunuzi zake hususani waliopo kwenye ukinzani nazo wakiwemo kama wadau iliyofanyika mjini hapa 

Alisema kutokana na uhaba wa mahabusu za watoto wamekuwa wakati mwengine wakikumbana na changamoto kadhaa wakati wakisubiri utaratibu wa kusikilizwa kesi zao wanazokabiliana nazo kabla ya kutolewa hukumu. 

“Hivi sasa kuna watoto wanakuwa kuzidi umri wao na wanafanya vitendo viovu huku wazazi wakiwa hawana uwezo hivyo kupelekea wimbi lao kuwa wengi na mahabusu yao ni chache hivyo kuna umuhimu wa serikali kuliangalia jambo hili kwa mapana kwa kuziongeza angalau mkoa na wilaya “Alisema 

Hata hivyo alisema pia sehemu hizo ambazo watakuwa wakiwekwa watoto hao itakuwa ni eneo ambalo watakaa wale ambao wapo kwenye ukinzani wa kisheria wakisubiri hitimisho la kesi zao ambazo wanatuhumiwa kuhusika nazo. 

Naye kwa upande wake Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwang’ombe Jijini Tanga Husna Abdi alisema watoto wanaokinzana na sheria wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo kuchanganywa na watu wazima watoto kutokupewa haki zao. 

Alisema kupitia warsha hiyo ambayo wamekutana wadau mbalimbali wakiwemo ustawi wa Jamii,Jeshi la Polisi,Mahakamani wawe chachu ya kuielimisha jamii kuhusu haki zao ili kuhakikisha haki inatendeka vema kwa mujibu wa sheria.(Habari kwa Hisani ya Blog ya Kijamii ya Tanga Raha)

No comments: