Tuesday, February 20, 2018

TAKUKURU TANGA YAPOKEA TAARIFA 204 ZA VITENDO YA RUSHWA

Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga,Christopher Mariba wakati akitoa taarifa za utendaji wao kwa waandishi wa habari kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba mwaka 2017.




Sehemu ya waandishi wa habari wakichukua matukio 
Sehemu ya wanahabari mkoani Tanga wakifuatilia matukio katika mkutano huo



TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoani Tanga (Takukuru) imepokea taarifa 204 za vitendo vya rushwa kutoka kwa wananchi wakizilalamikia idara mbalimbali za serikali na sekta binafsi.

Hayo yalibainishwa na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga,Christopher Mariba wakati akitoa taarifa za utendaji wao kwa waandishi wa habari kwa kipindi cha mwezi Julai hadi Desemba mwaka 2017.Alisema taarifa hizo ni ongezeko la taarifa 30 sawa na asilimia 17 ukilinganisha na kipindi cha miezi sita iliyopita ambapo taarifa zilizo pokelewa ni 174.

Aidha alisema katika taarifa hizo 52 zilihusu serikali za mitaa, ardhi/ mabaraza ya ardhi 33,vyama vya siasa 28,Polisi 23,Elimu 18,Mahakama 16,Afya 15,Kilimo 8,Tasaf 5,Bandari (TPA) 1,Maji 1,Ushirika 1,Uhamiaji 1,Tanesco 1 na Misitu 1.

Mkuu huyo alisema kati ya taarifa hizo 204 zilizopokelewa taarifa 92 zinaendelea kuchunguzwa wakati nyengine 66 uchunguzi wake ulikamilika na majalada kufungwa kutokana na kukosekana kwa ushahidi.Aliongeza kuwa taarifa 46 zilihamishwa kwenye idara nyengine kwa sababu zilikuwa zikihusiana na makosa chini ya kuzuia na kupambana na rushwa.

Hata hivyo alisema katika uendeshaji wa mashitaka takukuru mkoa wa Tanga imefanya uendeshaji wa kesi 18 mahakamani ambapo kati ya kesi hizo 9 zilifunguliwa kipindi cha Julai 2017 hadi Desemba 2017 na kesi 9 ni za kabla ya Julai 2017.

Alieleza pia katika kipindi hicho usikilizwaji wa kesi moja huko wilayani Lushoto kwa mshtakiwa aliyejulikana kwa jina la Ally Mgovi ambaye alikuwa Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Funta ambapo alifikishwa mahakamani kwa makosa ya ubadhirifu wa pembejeo za ruzuku zilizotolewa na serikali kwa ajili ya wakulima.

Alisema mshtakiwa huyo alipatikana na hatia alihukumiwa kifungo cha kwenda jela miaka mitatu au kulipa faini ya Tsh Milioni 1.9 ambapo alishindwa kulipa faini hivyo alipelekwa gerezani kutumikia kifungo cha miaka mitatu.

Akizungumzia fedha ambazo zimeokolewa na kazi za uchunguzi na udhibiti ambapo katika utekelezaji wa majukumu yao kwa kipindi cha Julai hadi Desemba 2017 kumekuwa na ongezeko la fedha walizookoa na kuzirejesha serikalini kutoka milioni 6,450,000 kwa miezi sita ya mwanzo hadi Milioni 52,508,260.

Alieleza fedha hizo zilikuwa kwa ajili ya malipo ya wanafunzi hewa ndani ya mpango wa elimu bila malipo katika shule za sekondari,mishahara hewa na gharama kwa ajili ya semina hewa(Habari kwa hisani ya Blog ya Kijamii ya Tanga Raha)

No comments: