Thursday, August 17, 2017

WANAOGUSHI NYARAKA KUINGIZA KEMIKALI WAPIGWA MARUFUKU.

Na Jacquiline Mrisho na Bushiri 
Matenda - MAELEZO.

Serikali imewapiga marufuku mawakala wa forodha wanaogushi nyaraka kwa ajili ya kuingiza kemikali kwani ni kinyume cha Sheria na pia wanaipotezea Serikali mapato. 

Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA), Prof. Samwel Manyele alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu uingizaji wa kemikali nchini kutoka nje ya nchi.

Prof. Manyele amesema kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Udhibiti na Usimamizi wa Kemikali nchini kila anayeingiza kemikali anatakiwa awe amesajiliwa na kupewa hati ya usajili huo vile vile anatakiwa kupata idhini ya wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kabla ya kuagiza mzigo wa kemikali nchini.

“Natoa onyo kwa mawakala wote wa forodha wasiofuata taratibu zilizowekwa na Serikali hasa wanaogushi nyaraka zenye lengo la kukwepesha Sheria na kukwepa kulipa kodi na tozo mbalimbali za Serikali hivyo watakaokaidi hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao,” alisema Prof. Manyele.

Prof. Manyele amesisitiza kuwa kuanzia Leo Agosti 17, 2017 hakuna mtu atakayeruhusiwa kujishughulisha na shughuli za kemikali bila kuwa na hati ya usajili wa shughuli anayoifanya pia hakuna atakayeruhusiwa kuagiza mizigo ya kemikali bila kuwa na kibali. 

Aidha, Prof. Manyele alifafanua lugha elekezi zinazotakiwa kutumika katika kuweka lebo za kemikali husika kuwa ni Kiswahili na Kingereza tu hivyo hakuna kemikali itakayoruhusiwa kuingia nchini ikiwa imendikwa kwa lugha tofauti na hizo.Vile vile hakuna mdau atakayeruhusiwa kushiriki tenda za ununuzi kwa ajili ya kuuza kemikali bila kuwa na usajili kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.

Ofisi ya Mkemia Mkuu inaendelea kukabiliana na changamoto za wadau wa kemikali kwa kuendelea kuwaelimisha wadau kuhusiana na matakwa ya Sheria na Kanuni za uingizaji wa kemikali nchini, kuchukua hatua za kisheria kwa wale wanaokiuka matakwa ya Sheria na kanuni zake, kuboresha mifumo, vifaa na sehemu za kufanyia kazi pia wakala inaendelea kufanya kazi kwa masaa 24 katika siku saba za wiki.

No comments: